Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Justin Lazaro Nyamoga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilolo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, pia nami nitumie fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ananiwezesha kwa mara ya kwanza kusimama hapa Bungeni na kuchangia. Nikushukuru wewe, lakini pia niwashukuru wananchi wa Jimbo la Kilolo ambao waliniamini na kunituma niwawakilishe.

Mheshimiwa Spika, nitajielekeza kwenye suala zima la kilimo na mnyororo wa thamani, lakini kabla sijaenda huko, napenda kupongeza na kuunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Rais ambayo ilijaa hekima, busara, mwongozo na maono ambayo naamini katika miaka mitano ijayo tutakuwa na story au hadhithi ya kusimulia ya mabadiliko.

Mheshimiwa Spika, pia niipongeze Tume ya Uchaguzi, kwenye hotuba ilionesha wazi kwamba walifanya matumizi mazuri ya hela hadi kuwa na albaki ya karibu bilioni 69, kiwango cha uadilifu mkubwa ambacho walikionesha.

Mheshimiwa Spika, tukielekeza macho yetu kwenye suala zima la kilimo hasa kwenye suala la uwekezaji, napongeza hotuba hiyo kwa sababu ukurasa wa 29 unataja chai pamoja na mazao mengine kuwa mazao ya kipaumbele. Naomba nijikite kwenye hili suala la chai hasa mawazo na maoni ya wananchi wa Kilolo.

Mheshimiwa Spika, pale Kilolo kuna jumla ya hekta 3,600 ambazo zina rutuba kwa ajili ya kilimo cha chai. Siyo hivyo tu, kuna zaidi ya hekta 184 zimepandwa chai tangu miaka ya 1990 na kuwekewa kiwanda feki. Ile michai hivi tunavyozungumza, ile miti imekuwa inatosha hata kujinyongea. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, tangu miaka ya 1990 imekuwa ni kutafuta mwekezaji. Sasa najiuliza, pamoja na nia na dhamira ya Mheshimiwa Rais, ikiwa tutachukua zaidi ya miaka 30 kutafuta mwekezaji kwa ajili ya shamba na kiwanda cha chai kimoja, tutafika ndani ya miaka mitano?

Mheshimiwa Spika, lazima kuna mahali tunakwama. Nami napenda sana kumwomba kaka yangu, Waziri anayehusika na uwekezaji pamoja na viwanda na biashara ambao wanalijua jambo hili walitilie mkazo kwa sababu uzalishaji wa chai katika Wilaya ya Kilolo ambapo ardhi yake inafanana na Wilaya ya Mufindi yenye zaidi ya viwanda saba, hiyo ingeweza kukuza uchumi kwa kiwango kikubwa na wananchi wale waliopanda ile michai wanataka kuanza kung’oa kubadilisha mazao.

Mheshimiwa Spika, napenda kulizungumzia hili kwa mkazo kwa sababu watu ni lazima wajue kwamba moja ya sababu ya kupanda ile chai ilikuwa ni zao linaloweza kulinda vyanzo vya maji ambayo ndiyo yanayoenda Mtera na hata Kidatu. Kwa hiyo, tutakapobadilisha na kulima zao lingine pia tutavuruga vile vyanzo vya maji ambavyo vinalindwa kutokana na kulima lile zao la chai.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, nizungumzie zaidi kuhusu tafiti zinazofanywa na uelekezaji wa mazao. Hivi karibuni nilimwona Mheshimiwa Waziri Mkuu akiwa kule Kigoma akihimiza sana utafiti wa mbegu na uzalishaji wa zao la mchikichi ambalo linalimwa katika mkoa ule.

Mheshimiwa Spika, napenda kutoa taarifa kwamba watu wa Kilolo wanalima maparachichi; na siyo Kilolo tu, ni Mkoa mzima wa Iringa na sehemu ya Mkoa wa Njombe. Changamoto yake ni aina ya miche wanayopanda, hiyo mbegu wanayolima; je, ni ile ambayo itapata soko wakati watakapoanza kuvuna?

Mheshimiwa Spika, hapa napenda kutoa ushauri kwamba ipo hii Taasisi ya Utafiti inayoitwa TARI, napenda waelekeze nguvu kwenye utafiti wa mazao ya matunda na mbogamboga kwa kuweka kituo kabisa katika Mkoa wa Iringa au Njombe kwa ajili ya kuhakikisha haya mazao kama parachichi yanapolimwa, wakulima wanalima mazao sahihi ambayo yatapata soko wakati wa kuvuna utakapofika.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi kila mtu anakuza miche, anaokota mbegu huko, wakulima wanauziwa, wakati mwingine wanaambiwa ndani ya miaka mitatu wataanza kuvuna, ikifika miaka mitatu mti unarefuka tu na hakuna mazao kwa sababu hawakujua kama hiyo mbegu wanayotaka kuilima ni bora ama siyo bora. Udhibiti wa mbegu hasa miche, ni changamoto kwenye uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda pia kuzungumzia umuhimu wa mnyonyoro wa thamani katika mazao yanayolimwa kwenye maeneo yetu. Kwa sababu tuna nia ya kuwa na nchi ya viwanda, ni lazima kuangalia ni jinsi gani tunaboresha mnyororo wa thamani. Nitatoa mfano wa zao la nyanya ambalo linalimwa sana katika baadhi ya maeneo kwenye Jimbo langu pia. Maeneo hayo ni Ilula na Ruaha Mbuyuni yote ambapo baadhi ya Waheshimiwa Wabunge hapa huwa wanapita na kununua nyanya.

Mheshimiwa Spika, wakati unapita mara ya kwanza unaweza ukanunua tenga moja kwa shilingi 10,000/= lakini upo wakati utakaonunua kwa shilingi 90,000/=. Sababu ni kwamba hakuna namna nzuri ya uongezaji wa thamani kwa mazao yetu. Kwa hiyo, wakati fulani wananchi wanalima kwa gharama kubwa na wanashindwa kuvuna na kuuza kwa bei kubwa kwa sababu thamani yake haijaongezwa.

Mheshimiwa Spika, nafikiri haujafanyika utafiti wa kutosha wa masoko kwa sababu nafahamu ziko nchi ambazo hazilimi nyanya lakini zinauza nje. Wakati mwingine tumesikia baadhi ya mazao yanasafirishwa kwenda nchi nyingine na kule yanapofika ndipo yanapouzwa. Mfano mmojawapo ni parachichi; ukifanya utafiti utakuta bandari zetu bado hazi- pack na kupeleka nje, wala viwanja vyetu vya ndege; lakini zipo nchi ambazo tayari zinafanya hivyo kwa kuchukua mazao hayo kutoka kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, hili tusipolifanyia kazi maana yake ni kwamba tunazinufaisha hizo nchi jirani. Pamoja na ujirani mwema, lakini siyo kwa kufikia kiwango cha sisi kulima parachichi, miti ya mbao, zikauzwe kupitia nchi jirani. Napendekeza suala hili lifanyiwe utafiti wa kutosha na Wizara zinazohusika ili mazao yanayolimwa na wakulima kwenye maeneo yetu yaweze kuongezewa thamani na wananchi wale waendelee kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia ukurasa wa 33 unaoelezea kuhusu ubora wa mifugo na vitu vingine mbalimbali. Tukizungumzia mifugo, tunazungumzia uboreshaji wa thamani. Katika hili napenda kupongeza maana ndani ya hotuba hii imetaja baadhi ya machinjio yanayoboreshwa. Katika Mkoa wa Iringa iko machinjio moja ambayo naamini ni mojawapo itakayoboreshwa.

Kwa kuwa machinjio hizi baadhi yake zimechukua muda mrefu; na kwa kuwa baadhi ya watu wanaoishi katika maeneo yetu ya Jimbo la Kilolo na maeneo mengine ya Mkoa wa Iringa ni wafugaji, napendekeza kasi ya uboreshaji wa machinjio hizi iweze kuwa ya kwenda mbele ili wananchi hao waweze kufaidika mapema.

Mheshimiwa Spika, wakati huu ninapozungumzia hili, napenda pia nizungumzie kuhusu vyanzo vya utalii hasa katika Mkoa wa Iringa na hususan Jimbo la Kilolo ambalo natoka. Moja kati ya utalii unaohimizwa ni utalii wa kihistoria. Pale kwenye Jimbo langu la Kilolo, Kihesa Mgagao pale waliishi wapigania uhuru wa maeneo mbalimbali, hata Rais Mstaafu wa Afrika Kusini, Marehemu Nelson Mandela alishafika pale. Pia pana kumbukumbu nyingi za wapigania uhuru hao, kumbukumbu ambazo kwa sasa lile eneo limegeuzwa kuwa gereza.

Mheshimiwa Spika, sisi wananchi wa Kilolo hatusemi kwamba hatufanyi makosa; tunafanya, lakini gereza lile idadi ya wafungwa wake hawafiki 20. Pia pale ni sehemu ya kumbukumbu za kihistoria. Wanafunzi wa Kilolo na maeneo mengine ya Mkoa wa Iringa hawawezi kwenda kujifunza pale kwa sababu ya ulinzi uliowekwa mahali pale.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo yote, napenda kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)