Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Saashisha Elinikyo Mafuwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hai

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, kwanza nakushukuru kwa kunipa nafasi hii na ninashukuru sasa umetaja vizuri jina langu ni jepesi tu Saashisha Elinikyo Mafuwe.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ndiyo nimepata nafasi ya kuchangia na kupata fursa ya kuweza kusema neno la shukrani kwa ajili ya wananchi wa Hai walionipa heshima kubwa sana ya kunichagua kuwa Mbunge wa Hai. Pia wametupa heshima kubwa sana kumchagua Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wetu kwa kura nyingi za kutosha 92%, lakini wametuchagulia madiwani wa kutosha sana. Nawashukuru sana wananchi wa Hai. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kuunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Rais aliyotoa kwenye Bunge lako Tukufu. Hotuba hii ya Mheshimiwa Rais inatoa mwanga na mwelekeo wa Serikali kwa kipindi cha miaka mitano. Ukisoma kitabu hiki kinajibu matarajio ya wananchi wa Jimbo la Hai na wananchi wa Tanzania. Hii ni ishara kwamba Mheshimiwa Rais ni zawadi ya Watanzania, mambo anayoyafanya kwa nchi yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni mambo ambayo katika historia ya nchi hii hayatasahaulika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunayo sababu ya kumshukuru sana Mwenyezi Mungu aliyetuletea zawadi ya Dkt. John Pombe Magufuli. Miradi mikubwa inayotekelezwa na Ilani ya Chama cha Mapinduzi iliyopita na hii ambayo tunaandaliwa tena ya miaka mingine mitano inaonyesha kwa kweli Mwenyezi Mungu ametupa zawadi ya Rais mwema. Nichukue nafasi hii kuendelea kumwombea Mungu ampe afya njema ili haya yote yaliyoandikwa na yaliyosomwa kwenye hotuba yake yaweze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja ya jambo ambalo limenigusa sana ni habari ya kilimo. Kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais amesema sasa tutaenda kupandisha thamani ya mazao kwenye kilimo ambacho tunafanya. Kwetu kule Hai 78% tunategemea shughuli za kilimo. Nashukuru sana hotuba hii miongoni mwa mazao ya kimkakati yaliyotajwa, zao la kahawa limetajwa kama zao la taifa la mkakati.

Mheshimiwa Spika, sasa niseme kidogo, kule kwetu Hai zao la kahawa limepunguza tija kidogo kwa sababu ya utitiri wa vyama vingi vilivyopo kabla ya zao hili kufika sokoni. Pia zao hili limepunguza uzalishaji kwa sababu ya kukosekana kwa maji ya kumwagilia.

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie nafasi hii kuunga mkono hoja hii na kuiomba Serikali ihakikishe tunapata maji ya kumwagilia ili tuweze kufufua zao hili la kahawa. Ikumbukwe kwamba mbegu za kahawa au chanzo na utafiti wa kahawa unafanyika ndani ya Jimbo la Hai. Taasisi ya Uchunguzi wa Zao la Kahawa (TaCRI) iko ndani ya Jimbo la Hai. Nashangaa utaona maeneo mengine zao hili linapandwa lakini pale Hai limefifia. Niombe sana Serikali yangu sikivu, tumeomba na nimepeleka ombi maalum la kupatiwa mito ya umwagiliaji mitano inayopatikana ndani ya Jimbo la Hai. Tukipata mifereji hii mitano itatusaidia sana kufufua zao hili la kahawa.

Mheshimiwa Spika, lakini siyo hilo tu, Jimbo la Hai Mungu ametujalia tunavyo vyanzo vikubwa sana vya maji lakini tatizo ni namna ya kuvifikisha kwa wananchi. Tunayo ardhi nzuri ya kilimo lakini tatizo ni namna gani tuitumie.

Mheshimiwa Spika, nilianza kwa kuomba wenzetu wa TARI Mlingano wafanye utafiti wa udongo, kazi ambayo imekwisha kukamilika. Kwa hiyo, kazi iliyobaki ni kuiomba Serikali iweze kutuletea maji kwa ajili ya kumwagilia maeneo haya mazuri.

Mheshimiwa Spika, niseme kilimo cha mazao ya mbogamboga katika Jimbo la Hai ni biashara ambayo Serikali tukiwekeza tutakusanya kodi nyingi sana, tunaweza tukafanana na wanaochimba madini. Sasa hivi ukiangalia mazao mengi yanaenda nchi nyingine sisi Hai tunazalisha lakini wanapeleka nchi nyingine kwa ajili ya kwenda kuongezewa thamani na thamani yanayoongezewa ni kufanyiwa packing tu. Kwa hiyo, naiomba Serikali sasa kule Hai tumekubaliana kuwa na ari mpya ya kilimo na viwanda, tupatiwe msaada wa packing, baada ya wananchi kulima tuweze kuyaongezea thamani kwa kufanya packing. Bahati nzuri tunao uwanja wa ndege tutaweza kusafirisha nje ya nchi ambapo kuna mahitaji makubwa ya chakula cha ziada kinachozalishwa katika Jimbo la Hai.

Mheshimiwa Spika, hotuba hii imezungumza pia habari ya kuendelea kujenga miradi ya maji. Nashukuru sana Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, namshukuru Mheshimiwa Rais, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu kwa kutuletea Naibu Waziri wa Maji pale Hai. Tulikuwa na tatizo kubwa sana la maji; moja katika Jimbo letu la Hai huduma ya maji inasimamiwa na Bodi za Maji kulikuwa na shida kubwa sana. Nashukuru Naibu Spika alifika pale dada yangu akafanya kazi kubwa na nzuri ya kurekebisha matatizo yaliyokuwepo kule. Kwenye bodi hizi kulikuwa na shida amezinyoosha vizuri mno.

Mheshimiwa Spika, lakini pia nasimama hapa kushukuru kwamba tulikuwa na mradi wetu wa Kikafu ambao ulishathaminiwa siku nyingi wa shilingi bilioni 3.6. Nimepewa taarifa tayari Serikali ya Dkt. John Pombe Magufuli imetupelekea shilingi milioni 500 kwa ajili ya mradi huo, nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kule Lundugai tumepata shilingi milioni 200, hii ndiyo raha ya kuchagua CCM. Nataka niwaambie wananchi wa Hai walifanya maamuzi sahihi kabisa ya kuchagua Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kule Romu tumepata shilingi milioni 200. Naomba sana Serikali mradi huu wa Kikafu Chini utatusaidia kuondoa tatizo la maji. Pale Hai tunashida kubwa ya maji ya kunywa ukanda huu wa tambarare. Boma Ng’ombe, Mnadani, Weruweru, KIA hawana maji. Naomba sana Serikali fedha hizi shilingi bilioni 3.6 zikija kwa wingi zitatusaidia kuondoa tatizo hili.

Mheshimiwa Spika, lakini pia nashukuru sana Serikali kulikuwa na mradi wa visima 18 vilikuwa vinapeleka maji Arusha imesema sasa kwa kuheshimu Sera ya Maji ni vizuri pia Hai baadhi ya maji yakabaki pale. Nashukuru sana kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema mchangiaji mwenzangu mama Anna Kilango Malecela, kwa kweli tunatakiwa kuongezea TARURA fedha ili waweze kufanya kazi. Miundombinu imeelezwa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais lakini bado tunayo changamoto na mimi kule kwenye Jimbo la Hai hali si njema kwa habari ya barabara. Bado hatujafikia kiwango cha kukidhi matarajio ya wananchi.

Mheshimiwa Spika, hapa niombe Mheshimiwa Waziri anayehusika, tunayo barabara moja ambayo inalalamikiwa sana sana na wakati Mheshimiwa Rais ananiombea kura pale aliwaambia nileteeni Saashisha hii barabara nitaitengeneza, ni kilometa 13. Barabara hii iliitwa barabara ya ng’ombe, jambo hili linawachukiza sana wananchi kwamba ile barabara tuliambiwa ni ya ng’ombe. Sasa hii barabara ni ya watu, tunaomba barabara ile iweze kuwekwa lami, ni kilometa 13 tu kuanzia mferejini kupita TaCRI, Lyamungo kwenda kutokea Makoa.

Mheshimiwa Spika, lakini tunayo barabara nyingine ambayo hata ninyi mkishuka kwenye ndege pale KIA mkiwa mnaenda Moshi ni rahisi, inakuwa ni barabara mchepuko inaweza kutumika kilometa 25 tu inaanzia Boma ya Ng’ombe kwenda TPC. Ziko barabara nyingi ambazo kwa kweli kama TARURA itaongezewa uwezo wataweza kufanya kazi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia tumepeleka maombi maalum ya kupandisha hadhi barabara tano zilizoko ndani ya Jimbo la Hai kutoka TARURA kwenda TANROADS. Nashukuru sana kikao cha RCC kilipitisha barabara hii. Naiomba Serikali iongeze spidi kwenye mchakato huo ili barabara hizi ziweze kuhudumiwa chini ya TANROADS.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo limezungumziwa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais ni kuhusu umwagiliaji. Naomba sana, kwa kuwa nimeeleza hapo awali Jimbo la Hai linaweza kutumika kukusanya kodi nyingi kwenye mazao haya miradi hii ya umwagiliaji iweze kufanyiwa kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini iko changamoto, niombe sana Mheshimiwa Waziri wa Maji na TAMISEMI tunayo miradi iliyoko kwenye kata yetu ya Weruweru na pale Kikafu Chini, ni Jumapili tu nimetoka kwenda kutembelea miradi hii, iko shida. Serikali imeleta fedha pale shilingi milioni 91 lakini ule mradi umetulia, hakuna kinachoendelea. Tayari Serikali imeshaweka fedha ziko shilingi milioni 700 kwenye Kata yetu ya Weruweru kule Mijengweni, Serikali imeweka mashine zimefungiwa kule, naomba sana Serikali itoe pesa ili miradi hii iweze kukamilika wananchi waweze kunufaika. Hii ni miradi ya muda mrefu, Kikafu Chini ni miaka nane lakini huu mwingine wa Mijengweni ni miaka 15 mashine zimefungiwa kule na bado zina uwezo wa kufanya kazi. Naomba sana Serikali itusaidie ili kuweza kukidhi matarajio na shauku kubwa aliyonayo Mheshimiwa Rais ya kuweza kuisaidia nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo limezungumzwa kwenye hotuba hii ni ahadi ya Mheshimiwa Rais kupata umeme kwenye vijiji vyote. Wakati wa kampeni Mheshimiwa Rais alitoa ahadi ya kwamba maeneo ambayo hayajafikiwa na umeme wa REA yaweze kufikiwa. Niombe sana kwa kuwa Serikali imeshafanya kwa kiwango cha 84% hii asilimia iliyobaki Mheshimiwa Waziri ni ndogo sana. Wewe unafahamu na asubuhi nimezungumza na wewe kwamba yule mkandarasi pale Hai anatupa shida. Mimi naomba sasa Serikali mfanye maamuzi ili ile ahadi ya Mheshimiwa Rais iweze kutokea.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ni kengele ya kwanza?

SPIKA: Tayari muda wako umeisha.

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, haya naomba kuunga mkono hoja.