Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii nami nichangie katika hoja hii iliyopo mezani. Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai, lakini pia nawashukuru sana wapiga kura wa Urambo ambao wananipa ushirikiano wa hali ya juu. Nawashukuru, nawaomba waendelee kuniunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii pia kumshukuru sana Rais na Jemedari wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya. Hii siyo mara ya kwanza, nimeshasema mara nyingi na ninaomba nirudie hapa, katika mambo ambayo nimejifunza kwa Rais huyu, kwanza nikuthubutu. Anathubutu; pili, anaamua, anafanya maamuzi na tatu, anatekeleza. Nampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza pia na Mheshimiwa Makamu wa Rais na Mheshimiwa Waziri Mkuu ambao wote kwa pamoja kwa kweli wametusaidia katika awamu hii kuleta maendeleo makubwa sana wakisaidiana na Waheshimiwa Mawaziri na wananchi kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nami nitumie nafasi hii pia kuwashukuru sana viongozi wote waliopo TAMISEMI. TAMISEMI kazi mnaifanya, hongereni sana. Mheshimiwa Jafo unafanya kazi kubwa sana ukisaidiwa na Mheshimiwa Kandege, Mheshimiwa Waitara, Mtendaji Mkuu, Nyamhanga; wote akina Dkt. Gwajima; Dkt. Bakari na Engineer Seif, wote tunawajua wanafanya kazi, hongereni sana. Mheshimiwa Jafo endelea kuchapa kazi na kundi lako lote unalofanya nalo kazi. Kazi wanaiweza; ukiiangalia TARURA, Afya, wote wanafanya kazi kubwa sana upande wa Afya na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasi Urambo tumenufaika, tunashukuru. Tumepata Vituo vya Afya viwili, lakini naomba na hapo hapo mtuongezee tupate na cha tatu tupate kwa sababu tuna Kata 18. Kwa kweli mmefanya kazi kubwa sana. Barabara tumeziona, maji tunategemea kutoka Lake Victoria; mambo mengi tumeyaona lakini tunategemea kutakuwa na mengi yanayokuja. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nilete maombi yafuatayo: la kwanza kabisa naomba mwaangalie wafanyakazi. Ndugu zangu wafanyakazi wana tatizo moja kubwa ambalo naiomba Serikali inayoongozwa na Chama Cha Mapinduzi, wafanyakazi kupanda madaraja sasa hivi ni kazi. Wakipanda madaraja, kuwarekebishia mishahara ni tatizo kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba waangaliwe sana wafanyakazi ambao wako karibu na kustaafu. Hakuna ambacho Serikali yetu haiwezi kukifanya. Naomba Utumishi na waajiri ambao ni Wakurugenzi na mfuko ule unaohudumia walimu pamoja na wafanyakazi wa afya, ule unaoitwa PSSSF wakae pamoja waone jinsi gani ya ku-coordinate ili wafanyakazi wanapopandishwa mishahara, basi na mishahara yao irekebishwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, mimi nina walimu 30 ambao wamestaafu, lakini mishahara yao haikurekebishwa baada ya kupanda madaraja, wamepata matatizo. Jambo hili linaweza kufanyiwa kazi kwa kuhusisha hayo maeneo matatu kama nilivyosema; Waajiri, Mfuko na Utumishi mkaweka utaratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hali kadhalika kama walivyoongea wenzangu, kuna uhamisho mwingine kwa kweli ni wa lazima. Naomba suala la uhamisho kwa wafanyakazi liangaliwe. Kwa mfano, mtu mume wake amestaafu, amekwenda Tanga. Unamwambia wewe mwalimu tafuta mtu wa Tanga anayekuja Urambo, ambayo ni kazi kubwa sana. Kwa hiyo, kuna uhamisho mwingine kwa kweli kuna haja ya Serikali kuangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali iangalie; Utumishi na Wakurugenzi jambo gani ambalo mnaweza kufanya likawasaidia walimu wanaotaka kuhama kwa genuine issues? Kuna wengine ambao kwa kweli ni genuine, kwa mfano, anafuata familia yake na mambo ya namna hiyo au maradhi. Naomba masuala haya mawili yaangaliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu, naomba tuangalie suala la upungufu wa wafanyakazi. Sisi kwa mfano Urambo tuna upungufu wa Walimu wa Sayansi 230, walimu wa Msingi 458 na wafanyakazi katika sekta ya afya 124. Naomba masuala haya pia yaangaliwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia itakumbukwa kwamba Serikali yetu ilikuwa na nia nzuri, ilipeleka fedha za maboma katika Halmashauri zote. Kwa bahati mbaya sana, sijui computer ili-skip Urambo! Tunaomba Mheshimiwa Waziri ukaangalie Urambo peke yake sijui ilifanyaje yenyewe ikarukwa hatukupata fedha za maboma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati huo huo, tuna shule nzuri na kubwa sana inaitwa Uyumbu High School, ni ya sayansi, inachukua wanafunzi kutoka nchi nzima, lakini kwa bahati mbaya sana hali yake siyo nzuri, ina upungufu wa mabweni na madarasa. Naomba Uyumbu iangaliwe kwa jicho la huruma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati huo huo nirudi kwa Waheshimiwa Wabunge. Waheshimiwa Wabunge tulicheza ngoma kwa ajili ya vyoo. Vyoo ambavyo ni vya mfano wa chumba kuwahifadhi watoto wa kike, lakini pia chumba cha kuhifadhi watoto wenye ulemavu. Kazi tuliifanya, lakini kwa ubunifu uliotokea baadaye tukaamua kwamba basi tuje na Shule ya Sekondari. Mmeona kwenye magazeti. Karibuni mkaone shule ambayo tunategemea itaitwa Bunge Girls High School, mkipata nafasi mkaione. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge wanawake tupige makofi kazi tulifanya kubwa tukaungwa mkono na wanaume. Naomba sana siku tukipanga mkaangalie Bunge High School ambayo natumia nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Spika na ofisi yake na Mheshimiwa Naibu Spika, ambao wanaisimamia ile shule. Sasa hivi imefikia hatua ya kuwekwa mabati. Basi tumuunge mkono Mheshimiwa Spika, tukipata nafasi tukaone kule kazi kubwa inayofanywa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, msifikiri tulipoteza muda, hatukupoteza muda. Kwa taarifa iliyoletwa na Mheshimiwa Jafo kwenye Kamati yetu imesema kwamba sasa hivi TAMISEMI wamechukua zile ramani na tayari wameshajenga majengo 1,233 kwa kufuata yale maelekezo ambayo tuliwaomba wayafuate. Kwa hiyo, tunamwomba Mheshimiwa Jafo na uongozi mzima wa TAMISEMI, mmefikia 1,233; tunajua mnaweza kufanya zaidi ili watoto wetu wa kike na wenye ulemavu wapate hifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kama mnakumbuka TWPG, yaani Wabunge Wanawake kwa kusaidiana na ofcourse Wabunge wanaume wakiwemo akina Mheshimiwa Mwalongo na wengine, tulizungumzia sana umuhimu wa taulo za kike. Kama alivyoongea Mwenyekiti wetu Mheshimiwa Rweikiza kwenye taarifa yake, amepongeza Mkoa wa Mara.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka huu wa fedha unaoisha 2019/2020 tayari wameshatoa taulo za kike 33,000 na mwaka huu 2020/2021 wameweka lengo la kutoa taulo za kike 43,000 kwa kutumia fedha zao za ndani. Ni jambo la kupongeza sana TAMISEMI. Mheshimiwa Jafo umehimiza Wakuu wa Mikoa wamelihimiza hili, naomba tu uendelee kwa kweli kwa sababu watoto wa kike kwa taarifa ya UNICEF ya mwaka 2008 ni kwamba tunapoteza watoto wa kike asilimia 10 kwa kutokwenda shule kwa kuogopa kutokupata hifadhi wanapokuwa shuleni. (Makofi)

Kwa hiyo, mimi nakupongeza Mheshimiwa Jafo, mnachapa kazi, endeleeni kuchapa kazi na niseme tu, kwa kweli lipo hili jambo ambalo wenzangu wameongea sana, TARURA inafanya kazi kubwa. Mwaka huu ndiyo mvua imetuadhiri, nakwambia barabara huko kwetu zinahitaja makalavati. Wananchi wanaweza kujitolea kwa kusaidiana na TARURA, lakini wanahitaji makalavati. Kwa hiyo, tunaomba kwa kweli TARURA iangaliwe kwa jicho la huruma, iongezewe fedha. Tunajua TANROAD wanafanya kazi nzuri sana lakini pia na TARURA waongezewe fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, narudia tena kuwapongeza sana TAMISEMI kwa kazi kubwa wanayoifanya na tunaomba mwendelee kufanya kazi kubwa sana chini ya Jemedari wetu Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli ambaye kama nilivyosema ni mtu anayetufundisha sisi tuige viongozi kuthubutu, ubunifu na kutekeleza. Naogopa kuishia kusema CCM oyee! (Makofi)