Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Jenista Joackim Mhagama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika,
kwa kudra za Mwenyezi Mungu, naomba kwanza nichukue nafasi hii na mimi niungane na Waheshimiwa Wabunge wote kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutufikisha kwenye mkutano huu wa Kumi na Tisa. Huu ni mkutano wetu wa mwisho katika kipindi cha miaka mitano. Inshallah Mwenyezi Mungu ametupa uhai tumeweza kufika siku hii ya leo. Kwa vile tunakwenda kwenye uchaguzi, naomba nianze kwa kukutakia wewe binafsi kila la kheri katika uchaguzi mkuu ujao. Tunaamini utapita kwa kishindo na dua za kupita bila kupingwa zikaanguke juu yako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini naomba nimtakie Mheshimiwa Waziri Mkuu kila la kheri. Bosi wetu, kiongozi wetu mkuu na yeye akapite bila kupingwa ili kuonyesha ni namna gani tunaweza kufanya kazi nzuri. Siwezi kuacha kusema nakitakia kila la kheri Chama changu cha Mapinduzi kikashinde kwa kishindo. Hizo lugha za kushindwa zinazotoka upande mwingine zishindwe na zilegee na tutakwenda kushinda kwa kishindo kabisa. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi ya kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu na kuweza kujibu hoja za Waheshimiwa Wabunge. Sambamba na kukushukuru kwa kunipa nafasi kwa dhati ya moyo wangu nakupongeza sana, wewe umeunganisha sifa za Maspika wote. Kama ni standard wewe umekuwa na standard iliyopitiliza, kama ni kutumia utaratibu na mifumo wewe umepitiliza, kwa kweli unastahili sifa zote na pongezi. Vilevile nipongeze timu ambayo imekusaidia sana Naibu Spika, tumemwona hapa amefanya kazi nzuri, Wenyeviti wa Bunge na viongozi wote wakiongozwa na Katibu wa Bunge kama Mtendaji Mkuu ndani ya Bunge. Kwa kweli tunawashukuru mmefanya kazi vizuri, mmetusaidia sana Serikali kuweza kutekeleza majukumu yetu na hasa yale yanayohusiana na shughuli za kibunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niungane na Mawaziri wenzangu na Wabunge wote ambao wamempongeza Rais wetu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania. Wamempongeza sana inajieleza wazi hotuba ya Waziri Mkuu kwa nini Rais huyu anastahili hizo pongezi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, upande wangu naomba niongeze mambo machache kwa nini tunampongeza Rais huyu. Rais huyu ni Rais mwenye msimamo thabiti pale yanapokuja maslahi ya Taifa la Tanzania. Rais wetu huyu ana sifa nyingine ya kutokuyumba wala kuyumbishwa kwenye maamuzi ambayo yanakwenda kuleta maendeleo kwa Watanzania na nchi yetu. Tumeshuhudia Rais wetu ni shujaa na jasiri kweli kweli na mmeona katika mambo magumu ambayo Taifa hili lilitakiwa lipite Rais wetu amesimama kuwa jasiri na shujaa hakutetereka anastahili pongezi sana. Rais huyu anasifa ya kuwa mwenye kujali, mmeona katika ziara zake anavyojali maisha ya Watanzania na anavyoumizwa na maendeleo ya nchi hii nani Rais kama Magufuli? (Makofi)

WABUNGE FULANI: Hakuna. (Makofi/Vigelegele)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, Rais wetu ni namba moja na anastahili sifa zote kwa kweli.

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kusema Rais huyu amejipambanua kuwa ni Rais mnyenyekevu lakini ni msikivu na mstahimivu. Haya yote unayaona, hasemi mwenyewe matendo yake ndiyo yanajidhihirisha. Ukimkuta Kanisani anadhihirisha hayo matendo yote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ni kwa nini amekuwa msikivu na mnyenyekevu, amebezwa na watu ambao yeye ndiyo anawaletea maendeleo. Rais wetu Mwenyezi Mungu akubariki na akuongezee miaka mingi. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, nadiriki kwa kumaliza eneo hili la Rais wetu kwa kusema, tumepata Rais bora mwenye maono ya dhati kabisa, msimamo thabiti, mkweli, anayewajali wananchi wake na aliyekubali kuwa tayari kufia Taifa letu la Tanzania, Mwenyezi Mungu ambariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kunipa fursa na nafasi ya kuweza kutumikia katika Serikali yake na leo tunaingia kwenye bajeti ya tano tukiwa tunamaliza miaka mitano. Nakushukuru sana Mheshimiwa Rais kwa imani uliyonipa mpaka kufika hatua hii ya siku ya leo. Pia nimshukuru sana Makamu wa Rais, mama yetu Mama Samia, kwa kazi nzuri, na hasa kumsaidia Rais wetu. Tumemuona amekuwa msaada mkubwa kwa Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kwa dhati niungane na Waheshimiwa Wabunge kumshukuru sana Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa. Kwangu Mheshimiwa Waziri Mkuu alitumia taaluma yake ya ualimu kunifundisha mwalimu mdogo Jenista, lakini Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kweli amejidhihirisha katika kutusaidia kutenda kazi zetu ndani ya Serikali kwa sababu amefanya kazi kwa weledi mkubwa sana.

Naomba nichukue nafasi hii nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu; tunakushukuru, tunakuombea kwa Mwenyezi Mungu kila la heri katika maisha yako yote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siwezi kuacha kutoa shukrani za dhati kwa Mheshimiwa Angellah, pacha wangu, mdogo wangu, Waziri mwenzangu, lakini nawashukuru sana wadogo zangu, vijana shupavu; Mheshimiwa Antony Mavunde na Mheshimiwa Stella Ikupa. Hawa kwa kweli kama ni uteuzi ulipata mahali pake, ni vijana wachapakazi kwelikweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kuwashukuru sana washirika wangu katika kazi ya utatu, Vyama vya Wafanyakazi, Vyama vya Waajiri na tasisi zote zinazosimamia masuala ya kazi. Mambo haya yasingewezekana kama sio Makatibu Wakuu watatu ndani ya Ofisi ya Waziri Mkuu ambao walikuwa ni mhimili mkubwa sana wakiwaongoza watendaji wote, Wakurugenzi na Wakuu wa Idara na Taasisi zote ndani ya Ofisi ya Waziri Mkuu, tumefanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sasa niwaambie Wanaperamiho, nawapenda na nawashukuru sana. Wameendelea kuniamini, naomba waendelee kuniamini, wembe ni uleule na mwaka huu wa 2020 kitaeleweka tu. Nawashukuru sana wananchi wa Jimbo la Peramiho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, shukrani zangu za dhati katika kipindi hiki cha miaka mitano zimuendee Mwenyekiti wa Kamati ya Katiba na Sheria, kaka yangu, Mheshimiwa Omary Mchengerwa na Makamu Mwenyekiti, dada yangu Mheshimiwa Najma Giga, Wajumbe wa Kamati ya Katiba na Sheria wamesoma hotuba yao hapa, wameipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu imefanya kazi vizuri sana, ni kwa sababu wao walitushauri vizuri, nawashukuru sana.

Mheshimiwa Spika, namshukuru sana kaka yangu, Mheshimiwa Oscar Mukasa na Mheshimiwa Dkt. Tisekwa na Kamati nzima ya UKIMWI, tumefanya kazi kubwa sana kwa pamoja, nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawashukuru sana Kamati ya Bajeti ikiongozwa na kaka yangu, Mheshimiwa Mashimba Mashauri Ndaki na hasa kwenye Mfuko wa Bunge. Kamati hii iliisaidia kuiambia Serikali mahitaji ya Bunge ili Bunge liweze kutekeleza kazi zake za Kibunge; nawashukuru sana Kamati ya Bajeti.

Mheshimiwa Spika, siwezi kumaliza shukrani zangu bila kumtaja Mheshimiwa Mtemi Chenge na ndugu yangu, Mheshimiwa Ngeleja, Kamati ya Sheria Ndogo na Wajumbe wa Kamati hiyo tumefanya nao kazi sana sisi ndani ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Ninawashukuru sana Wajumbe hao wote.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa pia shukrani za dhati kwa Wabunge wote. Kazi hii ya kuwa Chief Whip hapa mbele isingewezekana kama Wabunge wote upande wa Upinzani na Chama Tawala wasingenipa ushirikiano. Nawashukuru sana na Mwenyezi Mungu aendelee kuwabariki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niendelee kutoa msisitizo kwamba pongezi zetu na shukrani hizi tunazozitoa zinatoa fursa kwetu sisi kama Serikali kuweza kujifunza mambo mengi, lakini katika kipindi hiki pia tumepata taarifa za misiba, majanga ya mafuriko na vitu mbalimbali ambavyo vimepoteza baadhi ya wenzetu. Nitoe pole kwa Chama cha CUF kwa kupotelewa na kiongozi wa chama; nitoe pole kwa TBC kwa kumpoteza mtangazaji mahiri aliyesaidia kuihamishia Serikali hapa Dodoma, tunawapa pole sana. Vile vile tunawapa pole na wengine waliokumbwa na majanga ya namna moja ama nyingine.

Mheshimiwa Spika, naomba nimalize eneo hilo la kwanza kwa kusema yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, tunaingia kwenye Uchaguzi Mkuu, tunapoingia kwenye Uchaguzi Mkuu watu wamekuwa wakitafakari na kuomba uchaguzi huu uwe huru na uwe uchaguzi wa haki. Naomba kuwaomba sana Vyama vya Siasa vyote nchini, wadau wa demokrasia na wadau wengine wote, ili uchaguzi huu uishe salama, naomba sana tufuate sheria bila kushurutishwa, tutii kanuni na taratibu na miongozo itakayotolewa na Tume ya Uchaguzi. Kwa kufanya hivyo ndiyo tutakuwa na uchaguzi huru na uchaguzi wa haki na sio vinginevyo.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa mujibu wa Kanuni ya 99(2) nitaendelea kujibu hoja kadhaa na zile ambazo sitapata nafasi ya kuzijibu naomba tutazileta kwa maandishi na zitaingia kwenye Hansard ya Bunge lako tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya kwanza kutoka Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria, kama nilivyosema pale mwanzo walitupongeza sana kwa kazi nzuri ambayo imefanywa na Ofisi ya Waziri Mkuu na hasa katika kukusanya maduhuli. Idara moja tu ya Mpigachapa Mkuu wa Serikali kwa muda mfupi sana waliweza kuvuka lengo la maduhuli ambayo walikuwa wamepangiwa na tukaweza kufikia zaidi ya asilimia 80 kabla mwaka haujaisha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunaomba kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge Ofisi ya Waziri Mkuu ni Ofisi Kiongozi, ndiyo inayotakiwa kuonesha njia. Tutajitahidi kuhakikisha hii standard ambayo tuko nayo tunailinda ili tusimwangushe Waziri Mkuu na tusiiangushe Serikali kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, hoja ya pili ilizungumzwa sana na Wabunge wa Upinzani, alizungumza sana Mheshimiwa Masoud Abdallah Salim, Mheshimiwa Mwakajoka, Mheshimiwa Susan, Mheshimiwa Bungara, Mheshimiwa Sophia Mwakagenda na hii ilikuwa inahusu Tume Huru ya Uchaguzi; hoja hii imezungumzwa sana. Tumekuwa tukijibu hoja hii mara kadhaa hapa Bungeni na tumekuwa tukiendelea kueleza ipasavyo kwamba Tume hii ya Uchaguzi kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ukienda Ibara ya 74(7) imetamkwa kabisa kwamba taasisi hii ya Tume ya Uchaguzi ni taasisi huru; imetamkwa kabisa. Pia ukienda Ibara ya 11 inaonesha kabisa Tume ya Uchaguzi haitaingiliwa na mtu yeyote, hata vyama vya siasa, katika kufanya maamuzi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachotaka kujua ni jambo moja; ninao hapa mfano wa tume hizo ambazo zina jina la tume huru ambazo ziko katika nchi mbalimbali kwenye regions ambazo na sisi ni wanachama, lakini tume hizi zote zinazoitwa ni tume huru ni lazima tujiulize misingi yake kwanza ya tume yoyote ya uchaguzi ni ipi ambayo inatakiwa kuangaliwa ili kuweza kuipima tume hiyo?

Mheshimiwa Spika, jambo kubwa la kwanza ni kuangalia muundo wa tume hiyo. Tume hizi zote zimewekwa kwa mujibu wa Katiba ya kila nchi, hata tume yetu sisi imewekwa kwa mujibu wa Katiba ya Nchi yetu ya Tanzania. Lakini tume hizi zinapimwa kwa utendaji wake katika misingi ya kufuata sheria na kanuni; Tume yetu hii pia imewekwa kwa mujibu wa sheria na inafuata sheria na kuweka utaratibu wa kikanuni wa kuendesha mambo yake; huo ni msingi mwingine.

Mheshimiwa Spika, Tume yetu imeendelea kupimwa kwa mwenendo wake unaoakisi weledi wake katika kufanya na kusimamia chaguzi. Hili linapimwa namna gani; tunaipima tume ndani ya nchi lakini viko vyombo vya kimataifa vinaipima Tume yetu ya Uchaguzi kama inafuata weledi na inazingatia sheria. Hao wote wamefanya hiyo kazi na hakuna hata mara moja waangalizi wa kimataifa wamesema Tume hii sio tume bora na haifai kuendelea kusimamia uchaguzi katika Nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Spika, nilisema pale mwanzo; tume hii imeundwa kwa mujibu wa Katiba na tume hizo nyingine zilizopewa majina ya huru zinakuja kujifunza kwenye tume yetu. Sasa nimesema kama imewekwa kwa mujibu wa Katiba ina maana hii ni tume inayowawakilisha Watanzania na imewekwa na Watanzania wenyewe kwa sababu Katiba ni document ya Watanzania wenyewe.

Mheshimiwa Spika, nimeendelea kujiuliza; ninayo hapa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Bunge la Jamhuri ya Muungano linawekwa na Sura ya Tatu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanznaia, naomba nisome kifungu cha 63(2) kwamba; 63.-(2) Sehemu ya Pili ya Bunge itakuwa ndicho chombo kikuu cha Jamhuri ya Muungano ambacho kitakuwa na madaraka, kwa niaba ya wananchi, kuisimamia na kuishauri Serikali ya Jamhuri ya Muungano na vyombo vyake vyote katika utekelezaji wa majukumu yake kwa mujibu wa Katiba hii.

Kwa hiyo sisi hapa Wabunge tuna madaraka kwa niaba ya wananchi, lakini tunatekelezaji majukumu yetu kwa madhumuni ya madaraka hayo tuliyopewa? Kifungu cha 63(3)(a) kinasema tunaweza kutekeleza majukumu yetu kwa niaba ya wananchi kwa kuuliza maswali kuhusu mambo ya umma katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo yako katika wajibu wetu wa kila siku.

Mheshimiwa Spika, mimi ni Chief Whip katika Bunge lako hili, nimefanya utafiti mdogo; mpaka hapa tulipofika tumeuliza maswali ya msingi 3,545; tumeuliza maswali ya nyongeza 9,317. Maswali hayo na naomba niendelee kusema nimefanya utafiti mdogo ambao wewe ndio unaweza ukasema vizuri zaidi kwa sababu ni utafiti wa Bunge; Mbunge wa Upinzani ambaye ameongoza kwa kuwa na maswali mengi ya msingi na ya nyongeza ana maswali 52; na Mbunge wa Chama cha Mapinduzi ambaye ameongoza kwa kuwa na maswali mengi, huu ni utafiti wangu mdogo, unaweza kufanya zaidi – ana maswali 103.

Mheshimiwa Spika, nimefuatilia, kati ya maswali hayo yote 9,317 yaliyoulizwa kwa mujibu wa Katiba iliyotupa madaraka ni maswali mangapi yameulizwa kuhusu Tume huru ya Uchaguzi, maswali hayo hayafiki hata asilimia moja ya maswali yote yaliyoulizwa ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Baada ya hapo nimejiuliza ajenda ya Tume Huru ya Uchaguzi ni agenda ya Watanzania ama ni ajenda ya watu wachache? Kwa hiyo hayo mambo ni lazima tuyaangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeendelea kufuatilia, hotuba zinazosomwa wakati wa hotuba ya Waziri Mkuu kutoka upande wa Upinzani, nimeendelea kufanya huo utafiti; mwaka 2014 hotuba wakati wa hotuba ya Waziri Mkuu ndani ya Bunge hili ilibeba hoja ya Katiba Mpya; 2015 hotuba ya Kiongozi wa Upinzani wakati wa Hotuba ya Waziri Mkuu ilibeba ajenda ya Katiba Mpya; mwaka 2016 hotuba ya Kiongozi wa Kambi ya Upinzani ilibeba hati idhini ya Mawaziri kufanya kazi kutoka kwa Rais; hotuba ya mwaka 2017 ilibeba dhana ya kesi za Wabunge wa Upinzani. Sasa najiuliza hivi kipaumbele cha wale ambao wanasema sasa ni lazima tupambane kwa ajili ya Tume huru ya Uchaguzi badala ya yale ambayo ni matakwa ya wananchi; wananchi wanataka maji, barabara, kilimo, elimu, afya, na hayo tumeyafanya vizuri sana katika kipindi chetu chote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja ya pili ilikuwa tuhakikishe kwamba uchaguzi wa mwezi Oktoba, 2020 usibague vyama vya siasa, wote twende tukiwa na haki sawa. Tunapokea ushauri wao lakini tunataka tukumbushe kidogo; vyama vingi vya siasa vilianza toka mwaka 1992 katika Nchi yetu ya Tanzania. Tume ya Uchaguzi hii ambayo ni tume huru kwa mujibu wa Katiba imeanza toka mwaka 1993 ikaanza kusimamia uchaguzi wa mwaka 1995.

Mheshimiwa Spika, mwaka 1995 wagombea urais katika Uchaguzi Mkuu walikuwa wanne, Vyama vya Upinzani na Chama cha Mapinduzi, kwa hiyo tume haikujali nani anagombea ilitekeleza wajibu wake. Wabunge 186 walishinda wa Chama cha Mapinduzi na Wabunge 46 wa Upinzani. Mwaka 2000 wagombea urais walikuwa wanne, mchanganyiko wa vyama, Wabunge walioshinda 202 CCM, 29 Upinzani.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2005 wagombea urais walikuwa 10, wapinzani tisa CCM mmoja, wote waligombea na Tume hiyo ya Uchaguzi haikujali misingi ya vyama. Wabunge walioshinda walikuwa 206 CCM, 26 walikuwa kutoka Upinzani. 2015 wagombea urais pia walikuwepo, Wabunge walioshinda 195 walikuwa wa Chama cha Mapinduzi, 65 walikuwa wa Upinzani. Hao ni Wabunge kwenye Majimbo.

Mheshimiwa Spika, kama hivyo ndivyo, naomba kuwahakikishia Watanzania uchaguzi huu utasimamiwa vizuri, vyama vyote vitapata haki sawa, vitashiriki ipasavyo, lengo letu liwe moja; kulinda amani na utulivu wa nchi yetu ili uchaguzi uweze kuisha vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ilikuwa ni kuhusu UKIMWI. Kwenye suala la mapambano dhidi ya UKIMWI ilikuwa ni Mfuko wa ATF. Tulikuwa tumeulizwa kuhusu fedha za wafadhili, tuliulizwa kuhusu masuala ya ukusanyaji wa data na uwezo wetu wa ndani katika kukabiliana na tatizo hili la UKIMWI. Tunamshukuru sana Mwenyekiti wa Kamati ya UKIMWI, Makamu wake na Wajumbe, walitushauri vizuri sana na sisi tumeanza kutekeleza

Mheshimiwa Spika, kwanza, ili kuifanya ATF ijitegemee bodi imekamilisha mpango mkakati wa kuhakikisha tunakusanya rasilimali za kutosha za ndani lakini Bodi ya Mfuko huo pia imeshafanya kazi ya kumwajiri Resource Mobilization Manager ili aweze kukusanya uwezo wa kuhakikisha Mfuko huu unakuwa na kazi. Tumepata Mshauri Elekezi wa kutusaidia kuhakikisha fedha za mfuko huu zinakusanywa. Hata hivyo, tunaishukuru Kamati na tunaendelea na majadiliano kati ya Kamati na Serikali kuwa na vyanzo vya uhakika vya Mfuko wa UKIMWI Tanzania.

Mheshimiwa Spika, vilevile tunawashukuru wafadhili, wameendelea kutoa commitment yao. PEPFAR kwa mwaka 2020/2021 wameongeza bajeti ya UKIMWI katika nchi yetu kwa asilimia nane, kwa hiyo tunawashukuru sana. Kwa hiyo tutaendelea kufanya hizo kazi vizuri.

Mheshimiwa Spika, tumeanza mradi Serikali, TACAIDS na shirika ambalo linatusaidia katika mapambano dhidi ya UKIMWI nchini la Umoja wa Mataifa UNAIDS, tumeamua kutengeneza mradi wa pamoja wa ku-train utaratibu na mfumo mzuri wa ku-collect data kutoka katika maeneo mbalimbali yanayohusiana na UKIMWI. Kwa hiyo tunayafanyia kazi hayo yote.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja kuhusu Mamlaka ya Kudhibiti Dawa za Kulevya Nchini. Hoja ya kwanza ilikuwa ni kwa nini hakuna mradi wa maendeleo; tumepokea ushauri huo, lakini kwa kuanzia tumeamua kutumia Fungu 65 kwenye Mradi wa Skills Development kuanza kuwafundisha wale wote wanaoacha kutumia dawa kuwapa mafunzo ya ufundi ili waweze kujiajiri. Nadhani jambo hili litawasaidia sana vijana wetu na wataondokana na matumizi ya dawa za kulevya.

Mheshimiwa Spika, tuliagizwa tukamilishe maabara ya kitaifa ya kuhakikisha tunakuwa na maabara ya kupima sampuli za dawa za kulevya, hasa kesi zinavyotokea na ukamataji. Hiyo maabara tumeanza kuifanyia kazi, vifaa vyote tumekwishanunua, tunachosubiri sasa hivi ni kupata miongozo ya TBA ili jengo letu liweze kutengenezwa vizuri na hayo yote yaweze kufanyika.

Mheshimiwa Spika, wametusaidia kutushauri Kituo chetu cha Itega kiwe ni kituo cha kitaifa kitakachokuwa na combination ya kazi kuhusu waraibu. Kwa hiyo pale itakuwa ni medication center, itakuwa ni vocation center lakini itakuwa ni counseling center. Tunataka kukigeuza Itega iwe ni model ya vituo vyote vitakavyoanza kujengwa katika Nchi ya Tanzania. Kwa hiyo tunazingatia jambo hilo na tunalifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, tumeweza kudhibiti matumizi ya dawa za kulevya nchini kwa asilimia 90 na sasa hivi bei ya dawa ya kulevya Tanzania kwa kilo moja imefika Dola za Kimarekani 12,000, lakini kwa nchi nyingine ambazo udhibiti bado haujawa mkubwa bado kilo moja inauzwa kwa 4,000 tu. Kwa hiyo hiyo ni kazi nzuri iliyofanywa na nadhani tuwapigie makofi sana na tuwapongeze wenzetu kwa kazi nzuri waliyoifanya.

Mheshimiwa Spika, tulikuwa na hoja za Bunge. Bunge limepewa pongezi sana kwa kazi nzuri uliyoifanya wewe mwenyewe na hasa kuanzisha Bunge Mtandao. Sisi Serikalini tunakushukuru, umeokoa fedha za Kitanzania zisizopungua shilingi bilioni mbili kwa makaratasi yaliyokuwa yanazunguka hapa Bungeni. Tunakushukuru sana.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja ya Ofisi za Wabunge, unafahamu kwamba mjadala huu tunao ndani ya Tume ya Huduma za Bunge, kwa hiyo, inshallah Mwenyezi Mungu akituridisha, basi jambo hili litazungumzwa ili lipatiwe muafaka ndani ya Tume. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja ya michezo ya Wabunge kwa mwaka huu wa 2020. Bado tunashawishika kuendelea kutii utaratibu na sheria. Nchi ambayo inakuwa na uchaguzi, haishiriki mashindano hayo. Kwa hiyo, tunaomba mtukubalie tuendelee kuzingatia hiyo sheria na tusishiriki mashindano hayo.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na maswali kuhusu OSHA, tutaendelea kufanya ukaguzi wa afya na usalama mahali pa kazi. Tumeshatengeneza mfumo wa work place inspection management, kaguzi za kisekta na kupunguza tozo ili kuwavutia waajiri wengi wajisajili. Hiyo yote tunafanya.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Maige aliuliza kuhusu Workers Compensation Fund kuona ni namna gani tunaweza kuhakikisha kwamba tunafanya kazi ya kupunguza tozo kwenye private sector. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Maige kwamba tumefanya acturial mwaka 2018, mfuko unaendelea vizuri. Wataalam wametushauri tufanye acturial nyingine mwaka 2021, matokeo yake sasa ndiyo yatupeleke kwenye kubadilisha viwango vya tozo katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na ushauri mwingine kwamba mifuko ya hifadhi ya jamii iwekeze kwenye miradi ya kimkakati. Tumeshaanza kufanya hivyo. PSSSF muda siyo mrefu watafungua kiwanda kikubwa sana cha bidhaa za ngozi pale Karanga Moshi. Kwa hiyo, ni kazi ambayo tumeamua kujikita nayo. Mfuko wa NSSF umebadilisha matumizi ya nyumba zake kuwa ni hostel za vijana wetu wa Vyuo Vikuu na wanafunzi wapatao karibu elfu nane na kitu wamepata nafasi na fursa ya kupata makazi bora katika nyumba za NSSF na tumegeuza mradi huo umekuwa ni mradi wa kimkakati.

Mheshimiwa Spika, tulisikia malalamiko ya Mheshimiwa Goodluck:-

Mheshimiwa Spika, nitaomba tukutane naye ili tujue kule PSSF tunaweza tukafanya nini kuondoa hilo tatizo. Kama Mkurugenzi ananisikia hapa, basi aanze kujipanga ili tuendelee kufanya kazi kwa weledi, tuwasaidie wastaafu wetu wasipate matatizo katika masuala yote ya pension.

Mheshimiwa Spika, maswali ni mengi, lakini ninaona kwa muda ambao umenipatia, haya yanaweza kutosha kujibiwa kwa siku hii ya leo, lakini tutaendelea kuyajibu yote kwa maandishi na tutayaleta katika ofisi yako. Ninawahakikishia Wabunge, Serikali imejipanga, Tume ya Uchaguzi itasimamia uchaguzi vizuri na tutakuwa na uchaguzi wenye matokeo ambayo ni halali kwa mshindi na ni halali kwa yule ambaye atakuwa ameshindwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya, nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Ninawashukuru Waheshimiwa Wabunge wote, ninamshukuru kila mtu kwa kunisikiliza na ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)