Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (UWEKEZAJI): Mheshimiwa Spika, awali ya yote, nami niendelee pale ambapo wameishia wenzangu, kumshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uongozi wake shupavu unaotufikisha katika hatua hii kwa kishindo na kwa mafanikio makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo mara kadhaa alikutana na wawekezaji mbalimbali wa ndani na nje ya nchi na amekuwa akitoa maelekezo kwetu wasaidizi wake na watendaji kuhakikisha kwamba changamoto za wawekezaji zinatatuliwa ili kuharakisha maendeleo ya nchi yetu. Nampongeza pia kwa uamuzi wake mzuri na makini wa kuliweka jukumu la kusimamia uwekezaji chini ya Mheshimiwa Waziri Mkuu jambo ambalo limewezesha kupata mafanikio makubwa katika kusimamia uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampongeza kipekee Makamu wa Rais pamoja na Rais wa Zanzibar kwa maelekezo mbalimbali ambayo wamekuwa wakitupatia kwa namna ambavyo tunatekeleza majukumu tuliyokabidhiwa na Mheshimiwa Rais. Nichukue nafasi hii pia kumpongeza sana na kumshukuru Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu kwa hotuba yake mahiri ambayo imeweka msingi na mwelekeo wa utekelezaji wa majukumu ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2020/2021. Kwa hakika hotuba hii pamoja na mambo mengine tumeshuhudia namna ambavyo imegusa masuala ya uwekezaji ambayo ninayasimamia chini ya uongozi wake madhubuti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana dada yangu, pacha wangu, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Mheshimiwa Jenista kwa namna ambavyo tumeshirikiana kwa pamoja katika ofisi hii katika masuala mazima ambapo ametusaidia katika uratibu wa shughuli za kiserikali lakini masuala ya uwekezaji. Pia namshukuru sana ndugu yangu Mheshimiwa Mavunde pamoja na Mheshimiwa Ikupa kwa namna ambavyo tumefanya kazi kwa karibu. Nimshukuru sana Katibu Mkuu Mama Mwaluko, Katibu Mkuu Nzunda na Bwana Masawe pamoja na watumishi wote Wakuu wa Taasisi na Wakurugenzi kwa namna ambavyo wameweza kutoa ushirikiano mkubwa katika kutekeleza majukumu tuliyonayo katika Ofisi ya Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitakuwa sijatenda haki nisipochukua nafasi hii kukushuru sana wewe binafsi kwa namna ambavyo umetulea na kutuongoza. Vilevile namshukuru Naibu Spika pamoja na Wenyeviti wote wa Bunge kwa namna ambavyo mmekuwa na usimamizi mzuri na uwezeshaji wa shughuli za Bunge lakini kwa kuanzisha huduma za Serikali mtandao. Kwa hakika na Serikali naamini haitatuchukua muda mrefu kwani itatusaidia pia na sisi katika kutoa huduma kwa wawekezaji kupunguza urasimu na gharama kwa wawekezaji wetu. Tunaamini pia kuwa mfano ambao umeuonyesha itakuwa ni chachu kubwa kwa matumizi ya Serikali mtandao pia kwa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee nishukuru sana Kamati yetu ya Bunge ya Katiba na Sheria kupitia kwa Mheshimiwa Mchengerwa (Mwenyekiti), Mheshimiwa Najma Giga (Makamu Mwenyekiti) na wajumbe wote kwa namna ambavyo wametupa ushirikiano mkubwa lakini kwa ushauri wao mzuri ambao kwa hakika umetuwezesha sana kuongeza ufanisi katika uhamasishaji, usimamizi na kufanikisha uwekezaji nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwashukuru sana TNBC TIC, TPSF, TCCIA, CTI, Jumuiya wa Wafanyabiashara Tanzania na CEO Roundtable. Pia sitasahau Balozi zetu za Tanzania nje ya nchi ambazo kwa hakika wamekuwa na mchango mkubwa wa kufanikisha uwekezaji na biashara nchini.

Mheshimiwa Spika, pamoja na shukrani zangu kwa sekta binafsi, napenda kutoa salamu za pole kwa msiba wa aliyekuwa Mwenyekiti wa Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF), Ndugu Shamte uliotokea hivi karibuni. Mwenyezi Mungu ailaze roho ya Marehemu mahali pema peponi, amen.

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua pia uwekezaji unafanyika katika wilaya na mikoa, sina budi kutambua na kuwashukuru Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa wote, Wakuu wa Wilaya na Wenyeviti wetu wa Halmashauri, Madiwani na viongozi mbalimbali kwa namna ambavyo wamefanya kazi yangu ya kuhamasisha uwekezaji kuwa nyepesi na rahisi na kwa namna ambavyo tumeshirikiana nao. Niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na Watanzania tutaendelea kukutana na wawekezaji na wafanyabiashara ili kuweza kusikiliza kero na changamoto mbalimbali zinazowakabili na kuzitatua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa umuhimu wa pekee kabisa nimshukuru sana sana mume wangu kipenzi, Mheshimiwa Balozi Mbelwa Kairuki pamoja na watoto wangu Kemilembe, Kokubelwa pamoja na Mwesigwa kwa mapenzi yao na kwa uvumilivu wao kwangu wakati wote na kwa kunipa egemeo muhimu linaloniwezesha kuhimili majukumu yangu niliyokabidhiwa na Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawashukuru UWT, Mkoa wa Dar es Salaam, UWT - Baraza Kuu Taifa pamoja na TUCTA kwa ushirikiano mzuri waliyonipatia napotekeleza majukumu yangu. Kwa hakika sina cha kuwalipa zaidi ya kuwahakikisha kwamba sitowaangusha. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Same.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (UWEKEZAJI): Mheshimiwa Spika, naambiwa nishukuru na Same hapa, Same nakuja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa naomba kipekee nielezee machache kuhusiana na wepesi wa kufanya biashara Tanzania.

Mheshimiwa Spika, napenda kuwapongeza wote ambao wamechukua wajibu wao katika kuhakikisha kwamba tunapanda nafasi tatu katika Tathmini ya Wepesi wa Kufanya Biashara. Nishukuru Wizara zote zinazosimamia yale maeneo 11 ambayo tunapimwa kwa mchango wao mzuri ambao kwa hakika ndiyo umepelekea kupata mafanikio haya.

Mheshimiwa Spika, niendelee kuwahakikishia kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu na Wizara mbalimbali 11 zinazosimamia maboresho, tutaweza kufanya vizuri zaidi mwaka huu mwezi wa 10 lakini na katika miaka mingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa melengo yetu kwa mwaka 2025 ni kuhakikisha kwamba tunafikia nafasi ya digit 2. Mwaka huu tulikuwa na nafasi ya 141 na tunaamini kwamba ndani ya miaka hiyo mitano ijayo tutaweza kufikia malengo hayo.

Mheshimiwa Spika, nitaje maeneo matatu ambayo tayari tumeshaweza kufikia nafasi ya tarakimu 2 ikiwemo suala la upatikanaji wa mikopo. Namshukuru sana Waziri wa Fedha na BoT tumefikia nafasi ya 67 kati ya 190. Nimshukuru sana Mheshimiwa Mahiga pamoja na Jaji Mkuu kwa upande wa usuluhishi wa migogoro ya kibiashara na kulinda mikataba.

Mheshimiwa Spika, eneo la tatu ni suala la upatikanaji wa umeme kupitia kwa Mheshimiwa Kalemani ambapo tumefikia nafasi ya 85 kati ya 190. Naamini kupitia Mawaziri hawa, tunayo nafasi ya kufanya vizuri zaidi na nitoe rai kwa Mawaziri wengine na kwa Makatibu Wakuu kwenye maeneo yale mengine nane yaliyobakia kuona namna gani tutafanya maboresho ili kuwa nafasi nzuri zaidi kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nishukuru sana sekta binafsi kwa uamuzi wao wa kuwekeza nchini na kwa namna ambavyo wanaendelea kuwekeza mitaji. Nawaomba waendelee kuwa na imani wakitambua kwamba nafasi ya Tanzania katika biashara na uwekezaji itaendelea kuimarika zaidi, waendelee kutuamini wakitambua kwamba tutatekeleza majukumu yetu mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, niendelee kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge tutaendelea kutekeleza mpango wetu wa blueprint, kuhuisha mpango wa kuboresha mazingira ya uwekezaji, kuanzisha utaratibu wa kuwapa Ubalozi wa Heshima katika masuala ya uwekezaji; kuimarisha Kituo chetu cha Uwekezaji Tanzania na kuimarisha mfumo wa kupokea na kutatua changamoto za wawekezaji.

Mheshimiwa Spika, vilevile tutaboresha sera na sheria ya uwekezaji, kuimarisha miundombinu ya kiuchumi kama vile nishati ya umeme, maji, mawasiliano na miundombinu, kuimarisha huduma za kifedha ili kuwezesha upatikanaji wa mitaji kwa wawekezaji wa ndani na kuimarisha upatikanaji wa ardhi kwa ajili ya uwekezaji kwa kuendelea kuzihimiza Mamlaka za Serikali za Mitaa kutenga maeneo ya uwekezaji. Pia tutalinda wawekezaji wa ndani dhidi ya ushindani usio na haki unaotokana na uingizaji wa bidhaa za magendo.

Mheshimiwa Spika, sitaweza kujibu hoja zote lakini nishukuru sana kwa michango mizuri ya Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia. Tunatambua nia yenu ni kuweza kuona kwamba nchi yetu inakuwa na mazingira mazuri ya biashara na uwekezaji. Ni imani yangu watumishi mbalimbali katika Wizara zetu na taasisi za Serikali wataendelea kubadilika kwenda na wakati kulea wawekezaji na kufanikisha uwekezaji ili kuhakikisha kwamba uwekezaji Tanzania unaendelea kukua, kuimarika na kuchangia zaidi katika pato la taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa, napenda kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia na niwahakikishie kwamba majibu yao watayapata kwa maandishi na tutaendelea kutekeleza yale yote waliyoshauri.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)