Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA NA AJIRA): Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii, kwanza kabisa napenda kuchukua nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema aliyeniwezesha kusimama siku ya leo.

Mheshimiwa pia, nachukua fursa hii kipekee kabisa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa imani na heshima kubwa aliyonipa ya kuendelea kuhudumu katika eneo hili kama Naibu Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nachukua fursa kumshukuru sana Mheshimiwa Makamu wa Rais, pamoja na Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa miongozo yao ambayo imetusaidia sana katika utendaji kazi katika Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nisingependa sana kurejea maneno ya Waheshimiwa Wabunge waliotangulia lakini niseme tu kwa kipekee kabisa tunamshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa upendo wake, uvumilivu na namna ambavyo ametuongoza katika ofisi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia nichukue fursa hii kumshukuru kipekee sana Mama yangu mpendwa, Mheshimiwa Mama Jenista Mhagama pamoja na Dada yangu Mheshimiwa Angela Kairuki kwa namna ambavyo mmendelea kutulea katika Ofisi ya Waziri Mkuu na kutupa ushauri lakini na upendo wenu wa dhati ambao umefanya kazi hii iwe nyepesi sana kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nichukue fursa hii kuwashukuru sana Makatibu Wakuu wote chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Watendani wote kwa ushirikiano mkubwa sana walionipatia lakini bila kumsahau Mheshimiwa Naibu Waziri mwenzangu dada yangu Ikupa Stella Alex kwa namna tulivyoshirikiana kwa pamoja kutekeleza majukumu chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee kabisa nichukue fursa hii kukupongeza sana wewe mwenyewe kwa namna ambavyo umeleta mapinduzi makubwa ya kiteknolojia ndani ya Bunge letu. Hii ni kuonesha kwamba kuna uhusiano mkubwa sana kati ya maendeleo na teknolojia na watu wenye asili ya Mkoa wa Dodoma. Hongera sana kwa kazi kubwa ambayo umeifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, niwashukuru sana wananchi wangu wa Jimbo la Dodoma Mjini kwa heshima kubwa waliyonipa. Niwaambie tu kwamba mwili wangu bado una nguvu na akili yangu ina nguvu ya kufanya kazi ikiwapendeza niko tayari kuendelea kuwatumikia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema hayo, sasa naomba nijielekeze katika hoja za msingi ambazo zimewasilishwa. Hoja ya kwanza ilikuwa ni ushauri ambao ulitolewa kwa WCF (Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi), namna bora ya kuendelea kutoa elimu kwa waajiri ili waendelee kujiandikisha na kutimiza wajibu wao kisheria. Tumepokea ushauri huu na WCF wanaendelea kutoa elimu kwa waajiri, wafanyakazi na wadau wote kuhakikisha kwamba takwa hili la kisheria linafanyiwa kazi kwa sababu ni jambo ambalo linawasaidia sana wafanyakazi wanaopata madhara wakiwa kazini kupata fidia.

Mheshimiwa Spika, suala la pili ambalo lilizungumzwa ni Serikali kuendelea kuwapa mafunzo ya ujuzi waraibu wa madawa ya kulevya ambao wameachana na madawa ya kulevya na hivyo kukosa shughuli ya kufanya. Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Fungu 65 tumeendelea kutekeleza ushauri huu kwa kuwahusisha waraibu wa madawa ya kulevya katika shughuli mbalimbali za ukuzaji ujuzi. Hivi sasa tunavyozungumza katika Programu ya Kukuza Ujuzi ambayo inaendeshwa chini Fungu 65 - Ofisi ya Waziri Mkuu, tumewaingiza pia watu ambao walikuwa wanatumia madawa ya kulevya kama sehemu ya kuwajengea ujuzi na kuwafanya wapate shughuli ya kufanya na waache kuendelea kutumia madawa ya kulevya.

Mheshimiwa Spika, nchi nzima tuna takribani watu 5,875 ambao wameshaingia katika Program ya Kukuza Ujuzi katika eneo la ufundi stadi. Kati yao watu 1,020 ni waraibu wa madawa ya kulevya. Hii ni kuonyesha kwamba ni kwa namna gani kama Serikali tuliona kwamba lazima tuwashirikishe pia na wenyewe ili waweze kupata ujuzi.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ambayo ilizungumzwa ni kuhusiana na vikundi vya vijana kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana ambapo ilitolewa rai na Waheshimiwa Wabunge kwamba idadi ya vijana kukusanyika kuunda kikundi ni kubwa sana na wakashauri pia twenda katika hatua hata ya kumfanya kijana mmoja aweze kukopeshwa. Kama Serikali kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana tuliliona hilo na kupitia Mwongozo wa mwaka 2013 ambao tumeufanyia marekebisho, hivi sasa tunakamilisha taratibu za kumfanya hata kama ni kijana mmoja ambaye anaweza kuleta tija na kuajiri vijana wengine pia anaweza kukopesheka pasipokuwa kwenye kikundi ili kuweza kuwasaidia vijana waweze kupata fursa hiyo ya kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia ilijitokeza hoja ya kuboresha Programu ya Kukuza Ujuzi. Ofisi ya Waziri Mkuu inaendesha Programu ya Kukuza Ujuzi yenye lengo la kumjengea ujuzi kijana wa Kitanzania ili kupitia ujuzi huo aweze kujiajiri na kuajiri vijana wengine. Kazi hiyo tumeifanya mwaka huu lakini pia katika mwaka ujao wa fedha tutaifanya kazi hii kwa ukamilifu. Tutaendelea na Programu ya Kitalu Nyumba ambayo itafikia vijana wengi zaidi mikoa yote 14 ambayo imebaki katika awamu ya pili. Tutaendelea pia na Programu ya Kurasimisha Ujuzi kwa Vijana wenye ujuzi ambao hawajapitia mafunzo rasmi ya ufundi. Programu hii tunafanya na VETA na vijana wengi wamenufaika.

Mheshimiwa Spika, pia tunaendelea na Programu ya Mafunzo ya Vitendo Kazini (Internship) ambapo hivi sasa kwa kushirikiana na sekta binafsi tunawachukua vijana wahitimu wa vyuo vikuu tunawapeleka katika taasisi mbalimbali za kibiashara, iwe ni viwanda au makampuni wanakaa kwa miezi 6 - 12 wakipata uzoefu kwa fani waliyoisoma na baadaye wanapewa Hati ya Utambulisho kwa maana ya Certificate of Recognition. Ikitokea siku anakwenda kuomba kazi akiulizwa uzoefu basi anaweza akatoa ile Hati kuonyesha kwamba amewahi kufanya kazi kwa vitendo kwa muda wa miezi 6 - 12 ili tuwe tumeondoa changamoto hiyo ya uzoefu.

Mheshimiwa Spika, la mwisho kabisa katika eneo langu ilikuwa ni hoja ambayo ilisemwa na Waheshimiwa Wabunge ya ushiriki wa vijana katika kilimo. Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo tunatekeleza mpango mkakati wa pamoja wa kuwahusisha vijana kwenye kilimo ambapo tunaanza na hatua ya kwanza ya kuwapa elimu na kuwaondolea fikra hasi kwamba kilimo ni shughuli ya mwisho ya kufanya mtu akikosa shughuli zote. Kwa hiyo, tumeanza na awamu hii ya kwanza ya kutoa elimu, tumezunguka karibuni kanda zote za nchi nzima kuwaelimisha vijana. Hatua ya pili tumeendelea kuwaweka vijana hawa katika makundi ilhali tukiendelea kusisitiza maelekezo ambayo Mheshimiwa Waziri Mkuu aliyatoa ya kila mkoa kutenga maeneo maalum kwa ajili ya shughuli za kilimo na uzalishaji mali. Baada ya hapo hatua ya tatu ni kwenda kuwaunganisha na Benki ya Kilimo ili waweze kupata fursa ya mikopo na mitaji ili waendeshe shughuli hizo za kilimo.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema haya, naunga mkono hoja nashukuru sana kwa nafasi hii. (Makofi)