Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Stella Ikupa Alex

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (WATU WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa nafasi awali ya yote ninaomba nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa ajili ya ulinzi wake katika kipindi chote cha miaka ambayo nimekuwa ndani ya Bunge lako tukufu toka 2015.

Mheshimiwa Spika, lakini pia nitumie kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuniamini kumsaidia kwenye eneo hili la watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia niendelee kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa jinsi ambavyo Serikali yake imeweza kumdhamini mtu mwenye ulemavu na kuhakikisha kwamba mambo mbalimbali ya watu wenye ulemavu yanashughulikiwa na hatimaye ustawi wa mtu mwenye ulemavu kuweza kuonekana iliwa ni pamoja na kumjumuisha kwenye maeneo mbalimbali. Mheshimiwa Rais hatuna kitu cha kukulipa sisi kama watu wenye ulemavu zaidi ya kuendelea kukuombea afya njema lakini pia ulinzi, pia baada ya hapa maisha ya hapa dunia ninaamini kuna maisha mengine basi usima wa milele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie kumshukuru sana Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu. Mheshimiwa Waziri Mkuu ninakushukuru sana kwa miongozo ambayo umeendelea kunipatia na hatimaye nimeweza kutekeleza majukumu yangu vizuri na kuendelea kukusaidia kwenye eneo hili la watu wenye ulemavu, Mheshimiwa Waziri Mkuu ninakushukuru sana nimeweza kufurahia vizuri maisha ndani ya ofisi yako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Jenista dada yangu kwa jinsi ambavyo ameendelea kuniongoza kwa jinsi ambavyo ameendelea kunielekeza sita koma kumshukuru kwa kweli amekuwa ni dada yangu mzuri sana na kuniongoza katika utendaji wangu wa kazi Mheshimiwa Jenista nakushukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia sambamba na hilo nikushukuru Mheshimiwa Angella Kairuki, dada yangu kwa jinsi ambavyo umeendelea kuniongoza na kunipa maelekezo mbalimbali niweze kukushukuru pia Mheshimiwa Naibu Waziri mwenzangu Mheshimiwa Antony Peter Mavunde kwa ushirikiano mkubwa ambao umenipatia katika kutekeleza majikumu yangu ndani ya ofisi ya Waziri mkuu nikushukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru wewe Mheshimiwa Spika wewe mwenyewe pamoja na Naibu Spika kwa jinsi ambavyo mmeweza kuliongoza Bunge letu, pia kwa jinsi ambavyo umeyashughulia masuala ya watu wenye ulemavu tunaona umehakikisha kwamba maeneo mbalimbali ndani ya viwanja hivi vya bunge yanakuwa ni rafiki kwa watu wenye ulemavu ninakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kuwashukuru sana makatibu wakuu ndani ya ofisi ya Waziri Mkuu, makatibu wakuu wako watatu, kipekee kabisa nikushukuru Adrew Masawe umenipatia sana ushirikiano mkubwa sana katika kutekeleza majukumu yangu. Ninaomba nikishukuru Chama changu Cha Mapinduzi za kuweza kutenga nafasi mbili za watu wenye ulemavu ambazo zimeniwezesha kuingia mimi na Mheshimiwa Amina Mollel pacha wangu Mbunge machachari hakika amekuwa akifuatilia vizuri utekelezwaji wa masuala ya watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwashukuru wakinamama UWT Mkoa wa Dar es Salaam lakini pia UWT ngazi ya mikoa yote ya Tanzania Bara pamoja na visiwani. Ninaenda haraka haraka kwa sababu ya muda naomba nijikite sasa kwenye hoja zilizotolewa na waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ambayo inaitaka Serikali kuweza kuimarisha kitengo cha watu wenye Ulemavu pia Baraza la Ushauri kwa watu wenye ulemavu, kushughulikia migogoro ya vyama vya watu wenye ulemavu. Serikali ya Awamu ya Tano tunaposema kwamba imetekeleza imetekeleza masuala ya watu wenye ulemavu imetekeleza kweli kweli na inaendelea kuyatekelez kwa kishindo.

Mheshimiwa Spika, katika eneo la kitengo cha watu wenye ulemavu tumeendelea kuhakikisha kwamba fedha zinatengwa rasilimali fedha zinatengwa kwa ajili ya kitengo hiki kupitia kifungu cha 2034, lakini pia tumeendelea kukipatia vitendea kazi vya kisasa kitengo hiki. Sambamba na hilo tumeongeza watumishi katika kitengo hiki ikiwa ni pamoja na kuteuwa kaimu mkurugenzi wa kitengo.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa baraza Serikali imeweza kulizindua Baraza la Ushauri kwa watu wenye ulemavu kwa kuwa lilikuwa limemaza muda wake. Mheshimiwa Rais aliteua Mwenyekiti na hatimaye Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana aliweza kuteua wajumbe wa baraza hili na baraza hili liliweza kuzinduliwa mwezi Juni, 2019 na linaendelea kutelekeza majukumu yake kwa mujibu wa sheria na pia tumeendelea kulitengea fedha.

Mheshimiwa Spika, pia kwa upande wa migogoro ya watu wenye ulemavu tumeendelea kuvifuatilia vyama hivi na kuvishauri kuhakikisha kwamba vinatekeleza katiba ambazo vimeweza kujiwekea vyenyewe. Katika hilo katika eneo la kutatua migogoro basi mfano mmoja wapo mzuri ni Chama cha Watu wenye Ulemavu wa Viungo (CHAWATA) ambacho kilikuwa kimeshindwa kufanya uchaguzi kwa takribani miaka kumi. Serikali iliweza kuingilia kati na kufuatilia mgogoro huu pia tulienda mbali zaidi kwa kuwapatia rasilimali fedha na hatimaye uchaguzi wao uliweza kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja pia ya kwamba Serikali iweze kutekeleza Mkataba wa Marakesh. Ikumbukwe kwamba 2019 Septemba, 11 Bunge lako liliweza kuridhia Mkataba huu wa Marakesh na hatimaye kusainiwa na Mheshimiwa Rais. Baada ya hapo ulipelekwa nchini Geniva ambapo kwenye Shirika la Hati miliki (World Intellectual Property Organization) ambako sasa umepelekwa kwa ajili ya uhakiki na hatimaye uweze kutelezwa kama ambavyo inatakiwa.

Mheshimiwa Spika, tunaposema kwamba Serikali yetu imetekeleza mambo mengi imetekeleza kweli kweli. Pamoja na hilo Serikali imeweza kuvifufua vyuo vitatu vya ufundi kwa watu wenye ulemavu. Vyuo hivi kimoja kipo Mkoani Tabora ambacho Ruwanzari, lakini pia Mkoani Tanga (Masiwani) na Mirongo Mkoani Mwanza na kupelekea kwamba idadi ya vyuo hivi kuwa vyuo vitano na pale mwanzoni vilikuwa viwili.

Mheshimiwa Spika, hili lilikuwa ni tamanio kubwa la watu wenye ulemavu kuhakikisha kwamba vyuo hivi vinafunguliwa na vinasaidia watu wenye ulemavu ambao wanashindwa kuendelea na masomo ya sekondari.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo Serikali imeweza kukamilisha uanzishwaji wa Mfuko wa Taifa kwa watu wenye ulemavu kwa kuufungulia akaunti katika Benki Kuu ya Tanzania. Sambamba na hilo Serikali imeweza kupendekeza Mfuko huu uweze kutengewa shilingi milioni mia mbili.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema haya machache ninaomba nitumie Bunge lako Tukufu hili kuwatakia Waheshimiwa Wabunge wote kila la kheri na upendeleo wa Mwenyezi Mungu na kibali kiendelee kuwa pamoja na sisi ili tuweze kurejea katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante nawasilisha na ninaunga mkono hoja. (Makofi)