Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya na uzima kujumuika hapa leo kwa pamoja kuchangia hoja hii muhimu ya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, pia nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kutoa mchango wangu lakini pia nikushukuru wewe binafsi kwa umahiri katika uongozi wako katika kipindi chote tukiwa hapa na hasa kwa ubunifu na mabadiliko ya matumizi ya Bunge Mtandao ambao umeturahisishia Wabunge utendaji wetu wa kazi ya kuwawakilisha wananchi wetu tunaowawakilisha.

Vilevile nichukue nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu na wasaidizi wake Mawaziri, Naibu Mawaziri pamoja watendaji wote wa Wizara wakiongozwa na Makatibu Wakuu kwa hotuba na kazi nzuri wanayofanya kuwaletea Watanzania maendeleo.

Mheshimiwa Spika, baada ya shukrani na pongezi hizo naomba kutoa mchango wangu wa ushauri kwa Ofisi ya Waziri Mkuu kwa maboresho madogo kwa kuwa hotuba imebeba mambo mengi mazuri kwa Watanzania.

Kwanza ni uwekezaji wa shamba la Mkulazi I kwa zao la alizeti. Shamba la Mkulazi I lililopo Kata ya Mkulazi, Tarafa ya Ngerengere, Mkoani Morogoro lina ukubwa wa hekta zaidi ya 61,000. Kutokana na tafiti mbalimbali za udongo, maji, hali ya hewa na kadhalika, eneo linalokubali kilimo cha miwa ni hekta 28,000 ambazo zitazalishwa sukari kupitia kampuni tanzu ya NSSF ya Mkulazi Holding Company Limited. Na eneo lililobaki zaidi ya hekta 33,000 zinafaa mazao mengi kama vile mahindi, mtama, mihogo na alizeti.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa lengo kuu la Kampuni ya Mkulazi kwa sasa ni kuendeleza eneo linalolimwa miwa na kwa kuwa tuna tatizo kubwa la upungufu wa mbegu za alizeti kwa malighafi ya viwanda vya ndani na upungufu mkubwa wa mafuta ya kula. Naomba kuishauri Serikali kupitia Wizara kuliazima eneo hili kwa vijana, kina mama na wakulima kwa ujumla kwa utaratibu wa kilimo cha kitalu katika vikundi vya wakulima au wakulima wakubwa wenye uwezo wa kulima maeneo makubwa kilimo cha alizeti ili kutosheleza mahitaji ya viwanda vyetu ya tani zaidi ya milioni mbili kwa mwaka tofauti na sasa wanapata tani laki sita tu na kulazimika kufanya kazi chini ya kiwango na kulazimu kutumia fedha za kigeni kuagiza mafuta nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu ukifanyiwa kazi kuanzia kilimo cha mwaka huu cha vuli utakuwa na faida kubwa kwa taarifa za kiuchumi na kijamii pia. Tutaongeza ajira kwa vijana, tutaongeza kipato na uchumi wa watu wetu, utainua uchumi wa tarafa, utaokoa fedha za kigeni tunazotumia sasa kuagiza mafuta ya kula nje ya nchi, tutaimarisha shughuli za kiuchumi na kuimarisha huduma za jamii katika eneo la uzalishaji.

Mheshimiwa Spika, pili vibali vya kazi kwa wawekezaji wakubwa toka nje; pamoja na nia nzuri ya Serikali kulinda ajira za Watanzania kwa kudhibiti ajira za wageni nchini kwa utoaji wa vibali, lakini kuna nafasi za ajira lazima zishikiliwe na wenyewe au watu wa karibu wao wanaowaamini. Kwa mfano nafasi za kuu kama CEO na Ukurugenzi Mkuu na Fedha hii nafasi wawekezaji wanapenda kuwa watu wao kwa vigezo zaidi hasa cha uadilifu, historia, mahusiano na maono ya mtumishi binafsi na ya kampuni badala ya kuangalia utaifa pekee.

Mheshimiwa Spika, kwa msingi huo naomba kuishauri Serikali kuangalia namna ya kuwapa na kuwaongezea muda wa vibali wenye makampuni hayo watu wao wa karibu wanawaamini kuendelea kubaki nchini kuendeleza makampuni yao, kinyume cha hapo inaweza kumlazimu mwekezaji kusitisha uwekezaji wake nchini na kuhamishia nchi nyingine kwa kutokuwa na mtu sahihi anayemuamini kumkabidhi kusimamia rasilimali zake alizowekeza hapa nchini.

Ushauri wangu waongezewe muda wa vibali kwa muda na haraka ili kuvutia uwekezaji nchini badala ya mtizamo hasi kuwa hatutaki uwekezaji wa watu kutoka nje.

Mheshimiwa Spika, ajira kwa vijana na ujasiriamali na biashara kwa mazao ya kilimo; vijana ni nguvu kazi kubwa sana katika Taifa letu na kwa takwimu zilizopo nguvu kazi ya Taifa zaidi ya 67% ni vijana na zaidi ya vijana, lakini kila mwaka wanaingia katika soko la ajira na uwezo wa Serikali na sekta binafsi kuajiri ni vijana laki moja na hamsini na tano tu kwa mwaka. Kwa muktadha huu sekta yenye uwezo wa kutoa ajira kwa wingi bila kubagua wala kuchagua ni sekta ya kilimo kwenye mnyororo mzima wa thamani kuanzia uzalishaji mashambani, biashara ya mazao ya kilimo, kutoa huduma ya pembejeo za kilimo, usafiri, vifungashio, zana za kilimo, fedha za mitaji, usafirishaji na kadhalika, lakini kutokana ni mifumo ya masoko ya mazao hasa kwa mazao ya kimkakati inawaondoa vijana katika kujihusisha na biashara ya mazao ya kilimo kwa wakulima kuwa kwenye soko la nje moja kwa moja au kuwa kwenye minada yenye wanunuzi wa nje ambao kimsingi ndio walikuwa wanunuzi wa wajasiriamali vijana katika kujiajiri.

Mheshimiwa Spika, mfumo huu ukiendelea tutaweza kutengeneza matajiri na wafanyabiashara wakubwa wa kesho wa Taifa hili kwa kuwa mazao ya kilimo ndiyo msingi wa kuwatengeneza kwa uzoefu na mitaji yao mikubwa na kubambia sekta nyingine baada ya mafamikio na kujenga uchumi imara kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, ili kukabiliana na changamoto hii naomba kushauri mfumo wa wanunuzi wa mazao ya wakulima wa stakabadhi ghalani na minada kufanyiwa mabadiliko na kuwa na masoko ya ngazi mbili. Ngazi ya kwanza ni soko la wakulima kuwa mazao yao kupitia vyama vya msingi ili kudhibiti ubora na bei kwa wakulima. Soko hili litawahusisha wakulima kwa maana ya wauzaji na wanunuzi wa ndani, wajasiriamali, wakulima wakubwa, vyama vikuu, wajasiriamali wadogo na wafanyabiashara pamoja wenye viwanda vya ndani vya kuchakata mazao ili kivipatia malighafi kwa bei himilivu ili kupunguza gharama za uendeshaji na kuweza kushindana katika solo la kimataifa na mataifa mengine. Hawa wote ndio wanunuzi katika soko la awali na kuwa katika solo la upili kwa ajili ya kuuza nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, soko la upili ni stakabadhi ghalani au TMX linalowakutanisha wafanyabiashara wa ndani, wakulima wakubwa na wanunuzi wa nje kwa mazao yanayosafirishwa nje ya nchi na yanayotumika kwa viwanda vya ndani.

Mheshimiwa Spika, utaratibu huu utasaidia kutatua changamoto zilizopo katika mfumo wa ushirika na masoko ya mazao kwa sasa. Wakulima watapata malipo taslimu na kwa wakati, utaondoa rushwa kwenye ushirika, ukosefu wa malighafi kwa viwanda vya ndani mfano viwanda vya korosho na kahawa, kutoa ajira kwa vijana kwa kujiajiri katika biashara ya mazao ya kilimo na kuongeza mapato ya Serikali kwa wajasiriamali na wafanyabiashara ya kununua katika soko la awali na kuuza katika soko la upili.

Mheshimiwa Spika, naomba kumshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa uongozi wake mahiri na miongozo yake kwangu katika kuwatumikia Watanzania kuwaletea maendeleo. Vilevile nimshukuru tena Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa usimamizi mzuri wa shughuli za Serikali na jinsi anavyotusimamia na kutuelekeza mara kwa mara katika kutimiza majukumu yangu.

Mheshimiwa Spika, aidha nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja muhimu ya hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, naomba kumpongeza na kumshukuru Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa kuridhia barabara kutoka Bigwa - Kisaki kujengwa kwa kiwango cha lami kwenye bajeti ya mwaka 2019/2020 kufuatia maombi ya watu wa Morogoro Kusini Mashariki kupitia mimi Mbunge wao hapa Bungeni na Bunge lake kupitisha.

Mheshimiwa Spika, baada ya bajeti hiyo kupita kwa barabara hiyo ya Bigwa - Kisaki kujengwa kwa lami na kuendelea kuomba Serikali na kushauri kuhimiza ujenzi kuanza haraka kutokana na umuhimu wa barabara hii kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, naomba Serikali yangu kutoa kibali cha ujenzi wa barabara hii ili mchakato wa kutafuta mkandarasi ukaanza ili kuanza ujenzi mwaka huu. Pia nashauri kwa kuwa nafamu Serikali ina majukumu mengi na tatizo la kukabiliana na Corona kwa sasa basi naiomba Serikali barabara yote ya kilometa 78 basi inaweza kutoa kwa awamu, kwa mwaka huu Serikali ikatoa kwa awamu hata kwa kilometa 40 na mwaka mwingine kutoa sehemu iliyobaki kilometa 38 ili ujenzi wa barabara mwaka huu.

Mheshimiwa Spika, umuhimu wa barabara hii kwa sasa umeongezeka sana pamoja na Makao Mkuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro, kupita katika tarafa tano kati ya sita za Halmashauri ya Morogoro lakini barabara hii inakwenda kwenye mbuga nyeti ya Hifadhi ya Nyerere, Mbuga ya Hifadhi ya Wanyama ya Selous kwenda kwenye Bwawa la Kisasa la Nyerere pamoja na kuunganisha mikoa ya Morogoro na Pwani.

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa barabara hii utarahishia ujenzi wa Bwawa la Nyerere, kuimarisha shughuli za utalii kwa kuboresha barabara pamoja na kukuza uchumi wa watu wetu kwa kurahisisha mawasiliano yao na kupunguza gharama za usafirishaji wa mazao na kuongeza kipato na uchumi wa watu wetu.

Mheshimiwa Spika, barabara hii kila mwaka Serikali inatumia zaidi ya shilingi bilioni mbili kwa mwaka kwa matengenezo kwa kiwango cha changarawe lakini bado inaharibika hasa kutokana na madhara ya mbuga.

Mheshimiwa Spika, naomba kwa mara nyingine Serikali kutoa kibali cha ujenzi mapema ili kuanza ujenzi wa barabara hii.

Mheshimiwa Spika, mwisho niwashukuru wapiga kura wa Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki kwa kuniunga mkono na ushirikiano wanaonipa na kuwatumikia kuwaletea maendeleo yanayoonekana jimboni kwa macho.

Mheshimiwa Spika, nakushuru wewe tena kwa kunipa nafasi na ahsante sana na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.