Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Prosper Joseph Mbena

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. PROSPER J. MBENA: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa yote anayotutendea sisi viumbe wake hapa duniani. Hata tunayopitia hivi sasa ya COVID-19 ni matakwa yake yeye Mola wetu, tunamuomba atuepushe na janga hilo la kimataifa na kutupatia hali ya furaha, amani na upendo, Amen.

Mheshimiwa Spika, nampongeza kiongozi wetu wa nchi, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutuongoza vema wananchi wake na kuletea maendeleo makubwa katika kipindi cha miaka minne iliyopita ya uongozi wake. Miradi mikubwa mikubwa ya maendeleo imeandaliwa na kuanza kutekelezwa. mradi wa ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kimataifa (standard gauge railway), ujenzi wa bwawa la kufua umeme la Julius Nyerere, ununuzi wa ndege nane na ya tisa inakuja kwa ajili ya shirika letu la ndege (Air Tanzania), ujenzi wa Hospitali za Wilaya kwa nchi nzima, ujenzi wa Vituo vya Afya nchi nzima.

Mheshimiwa Spika, Jimbo langu la Morogoro Kusini tumenufaika kwa kupata Hospitali ya Wilaya inayojengwa Mvuha, vituo vitatu vya afya kwenye Kata za Duthumi, Kisemu na Kisaki. Ujenzi wa majengo yote matano kwa kila kituo katika vituo viwili vya afya vya Duthumi na Kisemu, vimekamilika. Tunasubiri vifaa na mashine zipelekwe pamoja na madaktari na wauguzi na wafanyakazi wengine ili vituo hivyo vianze kufanya kazi ya kuwahudumia wananchi.

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya cha Kisaki fedha zake za ujenzi zimekwishatolewa na Serikali, kwa kweli kwa maagizo ya Mheshimiwa Rais mwenyewe alipotembelea Kisaki na maandalizi ya ujenzi umeshaanza. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa moyo wake wa huruma, upendo na kututhamini. Tunasema asante.

Napenda pia kumshukuru Mama yetu mpendwa Mheshimiwa Janeth Magufuli, kwa upendo mkubwa alionao moyoni mwake kwa kutupatia baiskeli kumi kwa ajili ya watoto walemavu katika jimbo langu la Morogoro Kusini. Namshukuru sana mama yetu Mwenyezi Mungu amzidishie, Amen.

Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Kassim M. Majaliwa (Mb), kwa hotuba yake nzuri aliyoiwasilisha hapa Bungeni kuhusu mapitio na mwelekeo wa kazi za Serikali na makadirio ya mapato na matumizi ya fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa mwaka 2020/2021. Mheshimiwa Waziri Mkuu ameeleza kwa ufasaha na ustadi mkubwa mafanikio yaliyopatikana katika Awamu ya Tano chini ya kiongozi wetu mkuu, Mheshimiwa John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mheshimiwa Waziri Mkuu, kazi kubwa na nzuri umefanyika, hongera sana.

Mheshimiwa Spika, nakupongeza wewe binafsi na wasaidizi wako kwa kutuletea Bungeni maendeleo ya kidijitali. Mheshimiwa Spika umekuwa mstari wa mbele kwenye mabadiliko haya ya kisayansi ndani ya Bunge la Tanzania lakini pia umekuwa mfano wa kuigwa wa kuimarisha mahusiano mazuri kati ya Bunge na mihili mingine miwili hapa nchini; Serikali na Mahakama. Kuwepo kwa mahusiano haya mazuri kati ya mihimili yetu mitatu hapa nchini kunatuletea uhakika wa kuwepo maendeleo, amani na ufanisi mzuri katika jamii yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Spika, hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu imeelezea mambo mengi yanayomgusa kila mwananchi. Mvua zinazonyesha kwa nguvu nchini kote jimboni kwangu imeleta madhara makubwa kwenye miundombinu ya barabara, mashamba na nyumba za wananchi. Kwa bahati mbaya mafuriko haya kwenye maeneo kama Kata ya Selembala huwaibua mamba wanaotoka Mto wa Mvuha na kuwadhuru wananchi. Mwanafunzi wa miaka kumi na moja anayeitwa Rahma Ramadhani Nemelagani wa darasa la nne wa shule ya Msingi Kiganila aliuawa kwa kuliwa na mamba. Mwenyezi Mungu amuweke mahala pema peponi, Amen.

Mheshimiwa Spika, barabara yetu ya Bigwa - Mvuha - Kisaki kujengwa kwa kiwango cha lami, Serikali inasubiri nini? Naomba tuanze kujenga. Barabara za ndani la Jimbo la Morogoro Kusini ambazo ndizo zinakwenda kwa wananchi vijijini kwenye mashamba zimeharibiwa na mvua. Tunaomba Serikali itusaidie fedha za kutengeneza barabara hizi kwa kiwango cha kustahimili mvua hizi. Pengine wakati umefika sasa Serikali ifanye tathmini kama gharama za kila mwaka za kuweka vifusi vya udongo katika baadhi ya barabara zetu za vijijini kuna tija ikilinganishwa na gharama ya mara moja ya kuweka lami.

Mheshimiwa Spika, janga la COVID-19 Wabunge wenzangu wameeleza na Serikali imetoa maelezo muhimu ya jinsi ya kujikinga. Mungu azidi kutusimamia. Ni ugonjwa hatari. Niombe tu jamii yetu kutopuuza maelekezo yanayotolewa na Serikali ikiwa ni pamoja na kuheshimu na kutii masharti ya quarantine. Wanaoambukizwa ugonjwa huu sio kwa makusudi hivyo tusiwaone kama ni watu wahalifu bali wapelekwe hospitali na kwa kweli tunahitaji kuwaonesha upendo na kuwaombea kwa Mwenyezi Mungu wapate nafuu na kurudi kwenye afya zao za kawaida.

Mwisho, Jimbo la Morogoro Kusini linakumbushia ombi la kutupatia chuo cha ufundi - VETA na kinaweza kujengwa katika mojawapo ya Kata za Lundi, Duthumi au Kisaki. Vijana wengi wanamaliza masomo yao ya msingi na sekondari na wakipatiwa mafunzo hayo ya ufundi wataingia katika mfumo wa uchumi wa viwanda na kutoa mchango wao mkubwa. Naunga mkono hoja.