Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, naomba kuanza mchango wangu kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uhai.

Pili naomba nikushukuru wewe kwa namna unavyoliongoza Bunge hili la awamu ya tano kwa umahiri mkubwa na weledi wa kiwango cha juu. Pia nitumie fursa hii kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa John J. P. Magufuli kwa namna Mwenyezi Mungu alivyomjalia vipawa mbalimbali inavyomwezesha kuliongoza Taifa letu kwa weledi mkubwa. Na mwisho lakini si kwa umuhimu nitoe pongezi za pekee kwa Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa na unyenyekevu mkubwa aliouonyesha katika kumsaidia Mheshimiwa Rais katika kuliongoza Taifa hili. Pia nimpongeze yeye pamoja na wasaidizi wake katika ofisi yake kwa namna wanavyojituma kulitumikia Taifa hili.

Mheshimiwa Spika, baada ya utangulizi huo sasa naomba nianze mchango wangu kwa kuanza na sekta ya uwekezaji. Pamoja na mazingira mazuri ya uwekezaji nchini lakini bado kuna watendaji hawaendi na kasi ya Rais wetu. Tatizo lingine ni upatikanaji wa ardhi kwa wawekezaji hasa kwa wawekezaji wa mashamba makubwa, kodi nazo kwa wawekezaji sio tu zimekuwa kubwa pia zimekuwa nyingi zinazofanana. Hapa nina maana mamlaka za usimamizi ni nyingi mno zinazofanana kimantiki japo zina majina tofauti.

Mheshimiwa Spika, sekta nyingine ninayopenda kuchangia ni sekta ya ardhi, Taifa letu sasa linakumbwa na tatizo kubwa la uuzwaji holela wa ardhi. Huku vijijini watu wanauza sana bila ya utaratibu. Serikali za Vijiji zimepewa mamlaka ya kuuza si zaidi ya heka 50, lakini wajanja huenda huko vijijini na majina ya ukoo mzima ili wapate ardhi kubwa zaidi. Mfano Mkoa wa Lindi lindi hili la uuzwaji wa ardhi ni mkubwa sana kwa ajili ya mashamba ya korosho na ufuta. Hili linaenda sambamba na uharibifu mkubwa wa mazingira unaosababishwa na ukataji hovyo wa miti kwa kigezo cha kufungua mashamba makubwa.

Mheshimiwa Spika, lingine katika hili ni suala la mipango miji, idara hii ina uhaba mkubwa wa wataalam wa mipango miji jambo linalosabisha miji yetu isipangike na badala yake tunakuja na sera ya urasimishaji. Katika Halmashauri zetu urasimishaji huu unatuongezea matatizo badala ya kutatua tatizo. Naomba kuishauri Serikali kuongeza wataalam wa upimaji na upangaji miji katika Halmashauri zetu nchini.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ninaloomba kuchangia ni juu ya taasisi au idara za Serikali zile zilizotengewa fedha zake kwa mujibu wa sheria, kama vile REA, maji UCSAF na kadhalika. Fedha hizi ni bora zikaenda kwa wakati mara zinapokusanywa kutoka Serikali Kuu kwani iko miradi inayokwama au kuchelewa katika taasisi hizo kwa kigezo cha ukosefu wa fedha na kwa kuwa fedha zilitengwa mahususi kwa kazi hizo basi Serikali ione umuhimu wa kupeleka fedha hizo haraka.

Mheshimiwa Spika, lingine ni kuhusu wastaafu; kumekuwa na ucheleweshaji mkubwa kwa wastaafu kupata mafao yao, kwa sasa muda mfupi zaidi kwa mstaafu kupata mafao yake ni miezi sita. Naiomba Serikali kupunguza muda huu kwani wastaafu hawa huwa ni kama adhabu kustaafu kwao, wakati wengine kama si wote wamelitumikia Taifa hili kwa weledi utumishi uliotukuka. Hivyo basi Serikali ione umuhimu wa watu hawa kupewa stahiki zao mapema iwezekanavyo.

Mheshimiwa Spika, naiomba pia Serikali ifanye utafiti wa kina kuona kama ni Mkoa gani, una umri gani, Wilaya gani ina umri gani au ni Halmashauri gani ina umri, hili litaisaidia Serikali inapojenga majengo yake ya kitaasisi yawe uwiano wa kitaifa zaidi. Mfano ziko Wilaya au Halmashauri za muda mrefu hazina majengo ya Kiserikali, wakati ziko Wilaya mpya au Halmashauri mpya zimekamilika kwa majengo hayo.

Mheshimiwa Spika, Liwale ni miongoni mwa Wilaya za Mkoa wa Lindi, Wilaya hii ni ya tangu mwaka 1975 lakini hadi leo hii Wilaya hii haina jengo hata moja lenye hadhi ya Wilaya. Wilaya ya Liwale, haina ofisi ya Mkuu wa Wilaya, haina jengo la Mahakama ya Wilaya, haina jengo la Polisi la Wilaya, haina jengo la Hospitali ya Wilaya, haina jengo la Halmashauri ya Wilaya. Hii ni mifano michache niliyoamua kuitoa kusisitiza hoja yangu.

Naiomba Serikali kuzingatia ushauri wangu ili kuimarisha umoja wa Taifa letu katika kugawana keki yetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema hayo naomba nirudie tena kuishukuru tena Serikali ya awamu ya tano kwa niaba ya Wanaliwale kwa kuendelea kutupatia umeme vijijini, kutujengea vituo viwili vya afya, kutupatia miradi ya maji katika kata nne, Wanaliwale wanamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa yote tuliyotendewa na Serikali yake ya CCM.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.