Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Spika, napenda kutoa mchango wangu kama ifuatavyo; kwanza nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Makamu wake pamoja na Waziri Mkuu pamoja na Naibu wote wawili kwa utekelezaji mzuri wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015/2020.

Mheshimiwa Spika, pamoja na utekelezaji huo mzuri naomba kutoa mchango wangu kama ifuatavyo; kwanza ni usambaji wa umeme vijijini. Nipongeze dhamira ya dhati ya Serikali ya kusambaza umeme na kufikia zaidi ya vijiji 9000, ombi langu kwenye usambazaji umeme kuangalia yale maeneo ambayo bado usambazaji wa umeme kama ilivyo kwenye Jimbo la Tunduru Kusini ambapo kati ya vijiji 65 ni vijiji vitano ndio vina umeme tena kwa mitaa michache sana kama kijiji cha Mchuruka, Azimio,Umoja,Chiwana na Airport pamoja na kijjiji cha Mbesa. Hivyo ninaomba Serikali kupitia mradi wa REA III sehemu ya pili kutoa kipaumbele maeneo ambayo yapo nyuma kama ilivyo Jimbo la Tunduru Kusini.

Pili ni usambazaji wa maji vijijini; ninaishukuru Serikali kutupatia miradi ya maji mitano katika vijiji vya Amani, Mtina, Mbesa, Lukumbule na miradi midogo midogo ya Namasakata, Nalasi, Chiwana, Semeni.

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwa Serikali ni kuongeza kiwango cha fedha kwenye maji vijijini kwani vijiji vingi havina maji kutokana na tabianchi, mito mingi imekauka hivyo kuna mahitaji ya visima vifupi na visima virefu. Kutokana na uwezo mdogo wa wananchi wetu kulipia maji huko vijijini ni vyema miradi hiyo iwekewe umeme wa jua kupunguza gharama za uendeshaji, hasa kwenye mradi wa Nalasi, Lukumbule na Mtina. Serikali imetumia fedha nyingi sana lakini haifanyi kazi kama ilivyotarajiwa na Serikali.

Mheshimiwa Spika, tatu ni kuhusu barabara za vijijini na mijini. Kutokana na hali ya mvua nyingi zilizonyesha mwaka 2019/2020 ninaiomba Serikali kuangalia uwezekaji wa kuongeza fedha TARURA ili iweze kukarabati barabara na madaraja zilizoharibika na mvua. Kuna haja ya kuongezea TARURA fedha kutoka Mfuko wa Barabara kutoka 30% mpaka 40% ili kutengeneza barabara nyingi zaidi kwani mazao mengi ya chakula na biashara yanatoka huko vijijini.

Mheshimiwa Spika, nne ni suala la elimu ya msingi na sekondari. Ninaomba Serikali kutenga fedha nyingi za kujenga madarasa ya shule ya msingi na sekondari kukabiliana na wingi wa wanafunzi ili kuondokana na idadi kubwa ya wanafunzi wanaosoma katika darasa moja.

Mheshimiwa Spika, katika Jimbo la Tunduru Kusini wananchi walifyatua tofali zaidi ya laki moja kwa ajili ya kujenga miundombinu za shule za msingi na sekondari lakini Halmashauri imekosa fedha za kujenga miundombinu hiyo. Hivyo ninaiomba Serikali kutoa fedha kuunga mkono juhudi hizo za wananchi ili kupunguza adha ya madarasa na vyoo pamoja na nyumba za walimu. Vilevile shule nyingi za kata hazina maabara ya sayansi pamoja na upungufu wa walimu wa sayansi. Ni vyema Serikali ikaitupia jicho.

Katika Jimbo la Tunduru Kusini hakuna sekondari ya high school, hivyo ninaiomba Serikali kuweka high school katika kila tarafa ili kuongeza usihofu wa watoto kwenda high school.

Mheshimiwa Spika, tano, ujenzi wa vituo vya afya na zahanati. Nipongeze Serikali kwa kutupa vituo vitatu katika Halmashauri ya Tunduru, pamoja na pongezi ninaomba Serikali iongeze kukarabati Kituo cha Afya Mtina ambacho hazikupata majengo ya ziada ya kuboresha kama ilivyo Nkasale na Mchoteka. Vilevile ninaiomba Serikali kutimiza ahadi ya Mheshimiwa Rais ya kujenga Kituo cha Afya Nalasi, Mbeya ambapo kuna vijiji sita na kata mbili na wakazi zaidi 30,000.

Vilevile ninaomba ongezeko la kasi ya ujenzi ya zahanati kwani bado idadi ya zahanati na vituo vya afya ni ndogo ukilinganisha na idadi ya watu.