Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia kwa maandishi na nitachangia hotuba hii ya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu katika maeneo mawili ya afya na maji.

Mheshimiwa Spika, kabla sijaanza na maeneo hayo mawili, naomba kuipongeza Serikali ya awamu ya tano chini ya uongozi mahiri wa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli pamoja na wasaidizi wake wakuu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais pamoja na Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu kwa makubwa wanayowatendea Watanzania hususan wakulima, wafugaji na wavuvi wadogo wadogo pamoja na wafanyabiashara-wamachinga nchini. Ahsanteni sana kwa kuwatetea na kuwasitiri utu wao kwa namna iliyotukuka, ni Mwenyezi Mungu pekee ndiye atakayewalipa.

Mheshimiwa Spika, Job Yustino Ndugai pamoja na msaidizi wako Mkuu Dkt. Tulia Ackson, Naibu Spika hongereni sana kwa kulisimamia na kuliendesha Bunge hili la Kumi na Moja kwa ustadi wa hali ya juu. Mmetupitisha salama katika majaribu mengi na sasa mmeendelea kutudhihirishia uwezo wenu mkubwa katika kipindi hiki kigumu cha janga la dunia la maambukizi ya Covid-19. Kwa kweli mlistahili nafasi hizo na mnastahili kuendelea kuliongoza Bunge la Kumi na Mbili ili nchi hii ya Tanzania iendelee kuwa tulivu na yenye amani.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Ummy Mwalimu, Waziri anayehusika na afya kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya ya kusimamia kudhibiti maambukizi ya virusi vipya vya Corona nchini kwa ustadi mkubwa. Kwa kweli ni muhimu kufuata miongozo ya WHO katika vita hii ya dunia nzima. Nilitaka kuiomba Serikali ijiandae na kukabiliana na mlipuko utakapoingia kwenye jamii mapema ikiwa tutafikia hatua hiyo itakayolazimu kuwa na wahudumu wa afya wengi na vifaa tiba na vitendanishi kwa wingi sana. Ni bora kujiandaa hata kama Mwenyezi Mungu atatuepusha na janga hilo na kwa kweli tuendelee kumuomba Mwenyezi Mungu atuepushe na janga hili.

Aidha, naomba tusilisahau tatizo la UKIMWI, na naomba Serikali izingatie mapendekezo ya Kamati ya UKIMWI hususan kuutunisha Mfuko pamoja na kutenga fedha zetu za ndani za kutosha kuwezesha kazi za kudhibiti maambukizi mapya na kuwahudumia wanaoishi na VVU zifanyike kwa ufanisi mkubwa.

Mheshimiwa Spika, naomba sasa niongelee eneo moja la sekta ya maji ambalo ni matumizi ya force account katika kutekeleza na kusimamia miradi ya maji nchini. Uamuzi huu uliofanywa na Serikali ya awamu ya tano na kusimamiwa na Mheshimiwa Makame Mnyaa Mbarawa, Waziri wa Maji pamoja na timu yake yote ya Wizara ya Maji ni uamuzi wa kihistoria unaotuondolea dhulma waliyokuwa wanaipata wananchi hasa wa vijijini ya kutopata huduma stahiki ya maji na kwa wakati. Nikitolea mfano miradi ya maji ya Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo, tulikuwa na wakandarasi wanne, (Ockra, Elegance, Vibe na Kipera) pamoja na mhandisi mshauri, Norplan. Baada ya Waziri wa Maji kuachana nao kwa sababu za mikataba, miradi hiyo sasa inatekelezwa kwa force account na gharama za miradi yote kwa ujumla imeshuka kwa zaidi ya asilimia 45! Hiyo ni faida kubwa sana, imeokoa rasilimali fedha.

Mheshimiwa Spika, wasiwasi wangu ambao ningependa Serikali iniondolee ni rasilimali watu kwa upande mmoja wa TARURA na kupotea kwa kazi na ajira kwa upande wa wakandarasi. Ushauri wangu ni kuwa wakandarasi wajirekebishe kwa kushirikiana na wahandisi wa Wizara wanaoandaa BOQs, waache kuifilisi Serikali na kuwadhulumu wananchi wanaokosa huduma ya maji wanayostahili na kwa wakati na TARURA waongezewe uwezo wa kuwasimamia wakandarasi kwa miradi mikubwa na uwezo wa kutekeleza miradi wao wenyewe kwa miradi midogo na ya kati.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba kutamka kuwa naunga mkono hoja kwa asilimia 100 na naomba kuwasilisha.