Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Spika, hotuba ya Waziri Mkuu ni hotuba kiongozi kwa Wizara zote Serikalini, Mheshimiwa Waziri Mkuu amefafanua kwa upana juu ya vipaumbele vya Serikali ya awamu ya tano ikiwemo masuala ya elimu, afya, miundombinu ya mawasiliano na uchukuzi, kilimo, ujenzi, bandari, reli ya kisasa, ununuzi wa ndege mpya, ujenzi wa viwanja vya ndege, kilimo na mifugo, maji, ujenzi wa bomba la mafuta kutoka nchini Uganda kwenda Tanga, ununuzi wa meli mpya na vivuko,ujenzi wa madaraja makubwa nchini, umeme na ujenzi wa mradi mkubwa wa umeme wa maji wa Mwalimu Nyerere Hydropower Station pamoja na uzalishaji wa umeme kutoka katika vyanzo vingine kama vile gesi, makaa ya mawe, umeme jua na joto ardhi. Miradi hii itasaidia kuliwezesha Shirika la Umeme nchini TANESCO na Wakala wa Umeme Vijijini (REA) kusambaza umeme nchini.

Mheshimiwa Spika, Serikali ya awamu ya tano imeleta mapinduzi makubwa katika kupeleka Tanzania kuwa nchi ya viwanda, huu ni mwanzo mzuri katika kulijenga Taifa letu.

Kuhusu ujenzi wa reli ya kisasa ya Standard Gauge (SGR) huu ni ukombozi katika kuhakikisha kwamba barabara zetu za lami na changarawe ziweze kudumu kwa muda mrefu na kuokoa fedha za walipa kodi.

Mheshimiwa Spika, Serikali yetu ya awamu ya tano imefanya kazi kubwa sana katika kuleta mageuzi makubwa ya uchumi nchini ambapo tumeshuhudia mapambano dhidi ya madawa ya kulevya, masuala la mapambano dhidi ya rushwa yameimarishwa ambapo fedha nyingi zimeokolewa. Pia Serikali yetu imeimarisha ukusanyaji wa mapato ya kodi, tunaipongeza sana Serikali yetu ya awamu tano kwa kuimarisha makusanyo ya mapato, niombe Serikali iendelee kuimarisha na kupanua wigo wa ukusanyaji wa kodi.

Mheshimiwa Spika, kufunguliwa kwa shirika letu la ndege la ATCL ni jambo kubwa na la kujivunia, ndege mpya zimenunuliwa na hivyo kuinua sekta ya utalii nchini na kuleta fedha za kigeni nchini na kuchangia katika ukuaji wa uchumi wetu.

Mheshimiwa Spika, kuhusu vyombo vya ulinzi na usalama vinachangia pakubwa katika kuhakikisha utulivu na usalama wa nchi, hivyo nashauri Serikali ivipatie vitendea kazi vya kisasa ili kufanya vyombo vyetu viende na wakati.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.