Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. DKT. STEPHEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba kuungana na Wabunge wenzangu waliopata fursa ya kuchangia hoja iliyoko mezani ya Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu kuipongeza Serikali yetu ya Awamu ya Tano kwa kazi kubwa na nzuri iliyofanyika hadi sasa katika kuliendeleza Taifa letu kijamii na kiuchumi. Kwa hakika chini ya uongozi madhubuti wa Rais wetu mpendwa, Dkt. John Pombe Magufuli na Serikali yake yote ikiweko Ofisi ya Waziri Mkuu na Wizara zilizoko chini yake imefanyika kazi iliyotukuka ya kuijenga nchi yetu na kila sekta ni shahidi wa miradi ya kimkakati iliyotekelezwa (afya, ardhi, elimu, habari, kilimo, maji, maliasili, mawasiliano, mifugo, uvuvi, nishati, ustawi wa jamii na kadhalika).

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi hizi, naomba nichangie hoja moja inayohusu suala la kazi na ajira.

Mheshimiwa Spika, tuna tatizo kubwa katika Halmashauri zetu za ukaimishaji wa watendaji wa nafasi mbalimbali za ajira kwa muda mrefu suala ambalo linadhoofisha utekelezaji wa majukumu na upitishaji maamuzi kwa kiwango kikubwa. Kwa mfano katika Halmashauri ya Wilaya ya Longido karibu asilimia 50 ya Watendaji wa Vijiji ni watumishi wanaokaimu nafasi hizo tena wengi ni kwa miaka mingi hadi sasa.

Naiomba Serikali kuanzia bajeti hii ihakikishe kuwa nafasi za ajira zinawekewa ukomo wa kukaimu na Serikali itoe pesa za kuajiri na vibali vya kuajiri kwa wakati kwenye Halmashauri husika.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha mchango wangu wa maandishi kwenye Hoja ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Hotuba ya Waziri Mkuu imeangazia kwenye ukurasa wa nane kuhusu hofu inayoendelea kutanda duniani kufuatia kuenea kwa homa kali ya mapafu inayoletwa na virusi vya Korona (COVID 19).

Mheshimiwa Spika, naomba kuishauri Serikali iwaagize viongozi wote wa ngazi zote katika vijiji vyetu, Kata, Tarafa, Wilaya na Mikoa isambaze habari ya kuwaelekeza na kuziagiza kaya zote zenye watu wao wanaoishi au kufanya kazi nchi za jirani ambazo nazo zimeshaingiliwa na janga hili la virusi vya Korona, watu hao wabakie huko huko hadi janga hili lidhibitiwe na wasijaribu kurudi bila kupitia mipaka rasmi (border posts) wapimwe kabla ya kuruhusiwa kwenda makwao.

Mheshimiwa Spika, hofu yangu kubwa ni kwa wale wanaoweza kuamua kurudi nyumbani kwa kupitia njia zisizokuwa rasmi (njia za panya) na kuvuka mipaka na kwenda hadi manyumbani kwao bila kupimwa na ikitokea akaja mtu ambaye ameathirika; atakuja kuambukiza jamii yetu nzima ambayo kama mjuavyo hatuna miundombinu toshelevu na rasilimali za kupambana na gonjwa hili ambalo bado halina dawa wala chanjo.

Mheshimiwa Spika, pia naiomba Serikali iwekeze katika kuweka vifaa vya kupima na kuzuia maambukizi mapya katika vituo vyetu vyote vya kutolea huduma za afya nchini zikiwemo zahanati, vituo vya afya na hospitali zetu za Wilaya na Mikoa ili kuepuka uwezekano wa kutokea kwa mlipuko wa gonjwa hili kama ilivyotokea kwa wenzetu wa mataifa kama China, Italy, Spain na kwingineko.

Mheshimiwa Spika, mwisho napenda kupongeza juhudi zinazoendelea kufanywa na viongozi wetu wa ngazi za Taifa tukiongozwa na Rais wetu mpendwa Dkt. John Joseph Magufuli, Waziri Mkuu, Mheshimiwa Majaliwa Majaliwa na viongozi wetu wa Mikoa, Wilaya, Tarafa, Kata na hata Vijiji katika kuhakikisha kuwa tunafanya kila liwezekanalo kuzuia kuenea kwa homa hii mbaya ya Corona.

Mheshimiwa Spika, pamoja na juhudi hizi nawasihi Watanzania wenzangu tuendelee kumlilia Mwenyenzi Mungu atuondolee janga hili.

Mheshimiwa Spika, kwa haya machache nashukuru kwa kupokea mchango wangu wa maandishi na ninaunga mkono hoja.