Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kunipa nafasi ya kuchangia. Awali ya yote nimshukuru kwanza Mwenyezi Mungu ambaye amenipa afya na nguvu ya kuendelea kuwatumikia wananchi wangu wa Jimbo wa Kyerwa. Nichukue nafasi hii kwanza kukupongeza wewe binafsi kwa miaka hii kwa kweli umeonesha uchapaji kazi mkubwa kwenye Bunge letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na mimi kama unavyosema kama mchungaji naendelea kukuombea Mwenyezi Mungu akupe afya na nguvu ili urudi tena uendelee kuchapa kazi hii ambayo umeichapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na wasaidizi wake. Ni ukweli usiopingika Mheshimiwa Waziri Mkuu amechapa kazi kubwa na amekuwa msaada mkubwa kwa Mheshimiwa Rais kwa ziara nyingi ambazo amekuwa akizifanya hata kule kwetu Kagera, ziara ambazo amekuwa akizifanya wale ambao walikuwa wakionekana ni Mungu watu siku hizi wamekuwa wapole. Nampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichangie kwa upande wa sekta ya kilimo; kwenye hotuba ya Waziri Mkuu sekta ya kilimo ni muhimu sana na ndiyo sekta ambayo ina wazalishaji wakubwa. Niiombe sana Serikali imefanya mambo makubwa sana, lakini katika sekta hii bado hatujaweka nguvu kubwa. Tunasema hii nchi ni Tanzania ya viwanda, lakini hivi viwanda lazima vipate malighafi kutoka kwa hao wakulima, tusipowekeza nguvu kubwa tutaendelea kuleta malighafi kutoka nje na tutaendelea kunufahisha Mataifa mengine wakati hizi malighafi zingeweza kuzalishwa hapa kwetu. Kwa hiyo, niombe sana pamoja na jitihada za Serikali, lakini iongeze nguvu, kwa kweli bado kabisa hatujaona nguvu kubwa kama ambavyo tumewekeza kwenye maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie kwa mfano suala la mazao haya ya kimkakati. Haya mazao ya kimkakati naamini tukiweka nguvu kubwa yatatusaidia sana kuongeza pato la Taifa na ndiyo mazao ambayo ni muhimu lakini pia yanaweza kutuingizia pesa ya kigeni kwa mfano, niseme kahawa, hili ni zao la muhimu sana. Pamoja na jitihada za Serikali za kuturudisha kwenye ushirika bado bado, mimi niseme kama mkulima ambaye natoka kwenye mkoa ambo tunalima kahawa bado hatujaona jitihada kubwa sana kubwa sana ambazo Serikali imeweka.

Mheshimiwa Spika, niombe sana tuendelee kuweka jitihada ili huyu mkulima ambaye anazalisha aendelee kuongeza uzalishaji. Mimi naamini tusipoweka nguvu kubwa katika mazao ya kimkakati wakulima hawa watakata tamaa. Maeneo mengine hata kule kwetu Kagera watu wameanza kukata tamaa sehemu zingine ile mibuni wanaikata wanaweka mazao mengine.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe sana Serikali iongeze nguvu lakini ni pamoja na kuwa na soko la uhakika. Hawa wakulima wanapolima mazao yao wapate soko la uhakika lakini pia wapate bei nzuri.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa kahawa kumekuwa na sintofahamu. Majirani zetu Uganda inasemekana wana bei kubwa na hili limeleta changamoto kubwa kwenye Mkoa wa Kagera na hasa kwenye Jimbo langu. Alipokuja Mheshimiwa Naibu Waziri alipofika kule akasema wamefanya utafiti Uganda wamekuta wana bei kubwa. Sasa baada ya kusema wana bei kubwa nini kinafuata?

Mheshimiwa Spika, mimi nafikiri kama kweli wana bei kubwa kwa nini tusiwaruhusu hawa wananchi tukaweka utaratibu kahawa hii hawa Waganda wakaja wakanunua wakatupa bei nzuri kuliko kuja unawaambia wananchi halafu unaondoka. Hata hivyo, Naibu Waziri mwingine anasema tatizo la bei ya kahawa ni soko la dunia. Kwa hiyo, hii inawachanganya wananchi hata sisi ambao ni wawakilishi tunakosa majibu ya kuwaambia wananchi wetu. Kwa hiyo, kama Uganda kuna bei kubwa ambayo inaizidi ya Tanzania na changamoto kama sio soko la dunia niombe sana Mheshimiwa Waziri basi hawa Waganda wawekewe utaratibu waje wanunue kahawa yetu ili wakulime wapate bei nzuri na wasiendelee kulalamika na mwisho wa siku wakakata tamaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi kama mwakilishi furaha yangu ni kuona wananchi wangu wanapata bei nzuri ya kahawa na wanajengewa ambayo mazuri kuweza kuuza kahawa yao. Haijalishi ni nani atakayenunua hata kama anatoka Uganda au Ulaya, cha muhimu Serikali iweke utaratibu mzuri.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nataka kuliongelea ni suala la miundombinu. TARURA wana barabara nyingi ukilinganisha na TANROADS na ndiyo wako vijijini ambako ndiko kuna uzalishaji mkubwa. Hawa TARURA tunaendelea kuwapa asilimia 30 wahudumie mtandao mkubwa ambao hata TANROADS hawafikii nusu, hili kwa kweli halijakaa sawa. Niombe sana Mheshimiwa Waziri Mkuu aliangalie jambo hili na ikiwezekana msiwaachie hawa Mawaziri kwa sababu kila mmoja anavutia upande wake. Mheshimiwa Waziri Mkuu aingilie kati hili jambo TARURA wapewe pesa ya kutosha ili waweze kuhudumia barabara zetu. Vinginevyo wananchi hawa wanapozalisha hawatakuwa na miundombinu rafiki ya kusafirisha mazao yao kufika kwenye masoko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mikoa mingine ambayo kwa kweli tumejaliwa, ukiondoa hii mvua iliyokuja kipindi hiki lakini sisi kwetu Kagera, kwa mfano kwangu Kyerwa miezi karibu kumi yote sisi tuna mvua, sasa huku barabara zinaharibika sana. Niombe sana Serikali maeneo haya ambayo yana mvua kipindi kirefu yaongezewe pesa ili barabara ziweze kutengenezwa. Kwa kweli nipongeze kwani Serikali imejitahidi TARURA wanafanya kazi nzuri wakiongezewa pesa naamini watafanya kazi nzuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongelee suala la Corona. Mimi niipongeze kwa kweli Serikali imejitahidi sana na huyu mama yetu Mheshimiwa Ummy Mwalimu pamoja na msaidizi wake wanafanya kazi nzuri na tumeona Waziri Mkuu kazi anayoifanya. Hawa wanaobeza siku zote wanasema mpiga debe huwa si msafiri acha wanaosafiri waendelee kuchapa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada za Serikali lakini wengine walikuwa wanashauri sijui kuna kujifukiza na kadhalika, lakini mimi nije mbele yako na niombe hili neno kama litapata kibali chako lifanyike kwa sababu una mamlaka ya kuamua jambo lolote ukiwa kwenye Kiti chako. Ukisoma kwenye Maandiko Matakatifu magonjwa yote yaliporuhusiwa na Mungu ilikuwa ni dhambi. Dhambi ndiyo imesababisha magonjwa haya yaje yatupate kwa sababu Mungu hawezi kuruhusu watu wake waguswe na adui kama hawajatenda dhambi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mimi pamoja na juhudi hizi zinazofanyika niombe sana, sisi hapa Bungeni ni wawakilishi wa wananchi wa Watanzania wote, Kiti chako kama kitaridhia tutoe dakika hata tano tusimame mbele ya Bunge hili tukatubu kwa ajili ya Taifa la Tanzania. Mheshimiwa Rais alishaonesha mfano mzuri na akatoa Maandiko sasa niombe sana na wewe utupe kibali kutoka kwenye Kiti chako tusimame tutubu kwa ajili ya dhambi ya Tanzania. Ninaamini Mungu ataturehemu na ataliponya Taifa letu tutakuwa salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nataka kulizungumzia ni suala la NIDA ambalo kwa kweli halijakaa vizuri na limeleta vurugu. Wewe unawaambia wananchi simu zitafungwa wakati NIDA hawajatoa vitambulisho, hivi huyu mwananchi unayemfungia simu zake hujampa kitambulisho, hujampa huduma kosa lake ni lipi?

Mheshimiwa Spika, niombe hili jambo Serikali iliangalie na ikiwezekana wakae wajipange, halijakaa sawa. Kule kwetu limeleta mpaka rushwa, imekuwa ni biashara, anayekuwa na pesa nyingi ndiye anaweza kupata kitambulisho, haliko vizuri kwa ujumla. Niombe sana Serikali ijipange jambo hili iliangalie na ikiwezekana wafuatilie maeneo mengine waone linaendaje.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja. (Makofi)