Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami jioni hii niweze kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu. Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha mimi na ninyi kuwepo hapa tukiwa na afya njema. Vile vile nachukua nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna alivyoweza kuiongoza nchi hii kwa miaka minne mfululizo na hii ni bajeti ya nne ambayo haina ukakasi, tunakwenda kifua mbele.

Mheshimiwa Spika, yaliyofanywa nchi hii ni makubwa sana. Vile vile nataka nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu wa timu yake yote. Mheshimiwa Waziri Mkuu, pongezi za pekee kwanza kwa kumudu speed ya Mheshimiwa Rais. Kwa sababu najua mlianza wengi, lakini wengine wameteremka, watu ambao speed iliwashinda, lakini wewe mwenyewe umebaki katika kiti hicho muda mrefu. Kwa hiyo, nakupa pongezi binafsi kwa kumudu kwenda na speed ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye hotuba hii naomba nijikite sana kwenye upande wa kilimo. Ni ukweli usiopingika, kwenye nchi yetu asilimia 65 ya Watanzania ni wakulima na hapa napenda kuipongeza Serikali, imechukua juhudi mbalimbali za kuimarisha kilimo hasa katika kuwekeza katika tafiti na kuwekeza katika upande wa pembejeo.

Mheshimiwa Spika, jambo kubwa ambalo naomba niendelee kuisisitiza Serikali, kuliangalia kwenye Sekta ya Kilimo hasa kwenye upande wa masoko, tunayo shida kubwa sana ya masoko ya mazao yetu. Nafikiri hapa hata Mheshimiwa Chegeni ametoka kusema hapa, kila mtu anayetoka huko Mwanza anazungumzia pamba na shida kubwa anayozungumzia ni upatikanaji wa fedha kwa wakulima wetu. Upatikanaji huu wa fedha unakwenda sambamba na upatikanaji wa masoko ya mazao yetu.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kwamba tunawekeza kwa kiasi kikubwa sana kwenye pembejeo na kwenye tafiti, lakini tusipokuwa na uhakika wa upatikanaji wa masoko ya mazao yetu, shida kwa wakulima wetu bado itakuwa kubwa sana. Ninapozungumzia soko, naomba nijielekeze vile vile kwenye ushirika. Kwenye ushirika kuna matatizo makubwa na mazito sana. Kuanzia kwenye sheria yenyewe ya ushirika. Hii ni mara ya pili nasema kwamba naiomba Serikali walete Sheria ya Vyama vya Ushirika ifanyiwe mapitio. Pamoja na kwamba hili ni Bunge la mwisho, basi hata kwenye Bunge lijalo hili jambo lifanyiwe mkakati. Sheria ya Vyama vya Ushirika bado ina upungufu mkubwa sana. Hata wenyewe Vyama vya Ushirika ukikaa nao wanakubali kwamba kweli kuna tatizo kwenye Vyama vya Ushirika.

Mheshimiwa Spika, siku moja nilikaa na Afisa Ushirika wa Wilaya, namwuliza vipi bwana, haya mambo yanakwendaje kwenye Vyama vya Ushirika? Mbona vinapoteza fedha za wakulima, wanapoteza mazao, inakuwaje? Anakwambia kwamba hata yeye hana mandate kubwa ya kuingia kwenye Vyama vya Ushirika na kukagua. Mwenye mandate hiyo ya kukagua ni COASCO. Sasa ni lini COASCO inavifikia vyama vya msingi? Ni lini COASCO inafikia vyama vikuu vya ushirika? Kwa hiyo, utakuwa COASCO yenyewe tayari ni mzigo.

Mheshimiwa Spika, hivi leo mimi ninavyozungumza hapa, katika Mkoa wa Lindi hasa Wilaya ya Liwale tuna tani 800 za korosho zimekosa soko, wakulima wanapeleka zile korosho mwezi wa Kumi na Moja, mpaka leo hawajui hatima yao. Kwa hiyo, naomba Serikali ichukulie jambo hili kwa umakini sana, kwamba Vyama vya Ushirika badala ya kuwa msaada kwa wakulima vimekuwa ni mzigo kwa wakulima. Kwa hiyo, naomba Sheria ya Marekebisho ya Vyama vya Ushirika yafanyike.

Mheshimiwa Spika, halafu kwenye hiyo hiyo sheria, Vyama vya Ushirika vimeruhusiwa kuanzishwa na watu 20, sijui watu15; matokeo yake unakwenda kwenye Halmashauri unakuta Vyama vya Ushirika lukuki na vyama vyenyewe vinafanya kazi wakati wa mazao tu. Ina maana wao wakati wa kununua mazao, wananunua mazao, yakiisha wanafunga milango na chama kinaishia pale. Wanasubiri msimu mwingine uje, wanafungua milango, wanachukua korosho za watu, wanauza, wanawaibia, msimu ukiisha wanafunga.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi vyama vya namna hii, sheria iansemaje? Hivi ni wakati gani chama kinatakiwa kifutwe? Yaani chama kisipofikia malengo yake, miaka mitatu, minne chama kinatangaza hasara, wakulima wanadaiwa, mpaka TAKUKURU wanaingia kwenda kudai fedha za wakulima, hicho chama kweli bado kina sababu ya kuishi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba nijike hapo kwenye Vyama vya Ushirika. Kwa kweli Vyama vya Ushirika sheria iletwe, viangaliwe ili kama kweli lengo la Vyama vya Ushirika ni kuwasaidia wakulima, zamani ilisemwa Vyama vya Ushirika vilikuwa vinaweza kusomesha mpaka vijana wa shule wanachama wa Vyama vya Ushirika, lakini leo Chama cha Ushirika kimekuwa ni mzigo kwa mkulima, ndiyo kinachomfanya ashindwe kusomesha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naiomba Serikali ilichukue hili, Vyama vya Ushirika ni mzigo. Pamoja na nia njema ya kuundwa kwake, lakini Vyama vya Ushirika kwenye sheria, inasema Vyama vya Ushirika vitasaidia wakulima kupata pembejeo na kupata masoko, lakini hivi vyama kweli vinafanya hiyo kazi?

Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri aje na tathmini. Lazima tufanye tathmini tuhakikishe vyama vingapi vinakidhi vigezo na vile ambavyo havikidhi vigezo vifutwe kwa sababu utitiri wa vyama hauna maana kwa wakulima kama wakulima watapoteza mazao yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili naomba nizungumzie suala la ardhi. Ardhi haiongezeki, wanadamu tunaongezeka. Ukienda kule kijijni kuna sheria kwamba kijiji kinaruhusiwa kuuza heka 50, lakini hao mliowapa hiyo mandate ya kuuza heka 50, elimu hiyo wanayo? Ardhi inauzwa sana nchi hii sasa hivi. Uuzwaji wa ardhi umekuwa ni wa holela sana. Ukienda huko vijijini, ardhi inaondoka kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuishauri Serikali, pamoja na kwamba tumeruhusu vijiji kuuza heka 50, lakini bado wataalam tulionao ni wachache hawakwenda kuwapa elimu wale wanaouza ardhi. Kule vijijini watu hawawezi kuona thamani ya ardhi, wanauza tu; lakini sisi tunaoishi mijini tunajua thamani ya ardhi.

Mheshimiwa Spika, naomba sana, kabla Taifa hili halijaingia kwenye janga la kupoteza ardhi, Serikali mtupie macho kwenye uuzwaji wa ardhi. (Makofi))

Mheshimiwa Spika, liko suala lingine huko kwenye ardhi. Kuna hili suala la urasimishaji. Ndugu zangu, urasimishaji ulikwenda Manzese, ulikwenda Kinondoni kwa sababu tulishindwa kuwapanga wale watu, tayari walishajazana. Leo urasimishaji uko mpaka vijijini. Watu wanakaa holela halafu mtu anakuja anakwambia kuna urasimishaji. Mji unakaa hovyo; hakuna mtaa, hakuna barabara; yaani kuna vijiji ambavyo havina hata sababu ya kuingia kwenye urasimishaji. Ni suala tu la mtendaji kuwahamasisha wananchi wajipange, wapimiwe maeneo yale wakae, kama ni kugawiwa; tena upimaji wenyewe siku hizi ni wa kuchangia.

Mheshimiwa Spika, mimi naomba tuachane na mambo ya urasimishaji hasa kwenye Halmashauri hizi za Wilaya na Vijijini. Tubaki na huu urasimishaji wa Dar es Salaam na Dodoma pengine kama tulichelewa kujipanga.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante, malizia.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba niunge mkono hoja. Napongeza sana Serikali kwa kazi kubwa tunayoifanya, inayotukuka na inayoonekana.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naunga mkono hoja.