Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Anatropia Lwehikila Theonest

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi. Nami nisiwe mbali na wasemaji wengi kuongelea juu ya janga la Corona. Kusema ukweli sisi kama Serikali Kivuli hatujaona initiative za kutosha, siwezi kusema hakuna ambacho kinafanyika lakini initiativezilizopo bado zinatutia mashaka iwapo changamoto itakuwa kubwa, kama nchi za wenzetu, je, sisi tutasalimika? Kama Italia, Hispania wanalia na China wameumia sisi tutasalimika?

Mheshimiwa Spika, tunaamini bado kuna njia ambazo zinapaswa kuwa za nguvu zaidi. Siyo kwamba watu wapigwe, walazimishwe kuingizwa ndani, walazimishwe kufungwa lakini bado kuna mechanism ambapo Serikali inaweza ikasaidia kama ambavyo wanafanya Rwanda. Unaweza ukasema Rwanda ni mfano mdogo mzuri wa initiative zinazofanyika.

Mheshimiwa Spika,naamini bado tuna nafasi ya kufanya kitu kabla janga hili halijawa kubwa unless tuendelee kuamini kwamba hamna kitakachotokea. Lazima twende na global trend, kama tunaona challenge ni kubwa sisi tunajiandaaje? Waswahili wanasema ni afadhali ujue Mungu yupo uishi vizuri kuliko uishi vibaya halafu ugundue yupo utakosa pa kukimbilia. Huo ndiyo wito wangu kwenu.

SPIKA: Huko Rwanda kuna nini kizuri kinafanyika?

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, Rwanda unaweza ukaona wametagaza total lock down, lakini kama haitoshi, wamewagawia vyakula watu ambao wana changamoto ya maisha.

SPIKA: Haya, basi nimekuelewa. Endelea na mchango wako, kumbe ni total lock down.

MBUNGE FULANI: Endelea.

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Ndiyo, nimekusikia Mheshimiwa Goodluck.

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Spika, nataka nimpe taarifa mzungumzaji anayezungumza kuwa Serikali hatua ambazo imechukua, siyo zote ambazo imezitangaza. Nataka nimpe mfano mmoja tu; agizo la Waziri Mkuu kwa Wakuu wa Mikoa wote, likaenda mpaka kwa Wakuu wa Wilaya, kila Wilaya katika Hospitali ya Wilaya imetengeneza withholding rooms na treatment unit. Hiyo treatment unit imegawanyika katika sehemu mbili; high risks na low risk.

Mheshimiwa Spika, vile vile kila wilaya ambayo iko mpakani, kuna sehemu maalum wametenga kwa wale wageni wanaoingia. Kwa mfano, Tunduma kuna wageni 84 mpaka sasa hivi wameifadhiwa mpaka zipite siku 14 ndiyo wataingia. Kwa hiyo, vitu vingine vizito siyo vya kuzungumzwa hadharani. Ahsante sana.

SPIKA: Taarifa hiyo Mheshimiwa Anatropia.

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, naendelea. Kwa sababu kama mambo hayazungumzwi hadharani, yatajulikanaje sasa? Si lazima yazungumzwe ili watu waweze kuchukua hatua! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee changamoto ya zao la kahawa. Zao la kahawa linachangia katika pato la Taifa zaidi ya asilimia tano, lakini ni moja kati ya mazao ambayo siyo tu yamesahaulika bali kuna mkakati unaonekana kama linataka kusukumwa pembeni. Changamoto ambazo wakulima wanapitia na hususan wakulima wa Mkoa wa Kagera, specifically Wilaya ya Kyerwa na Karagwe, yale ndiyo maeneo ambayo tunazalisha kahawa sana; na inaajiri karibia kila kaya. Almost kila kaya ni wakulima wa kahawa. Kipato chao kila siku ni kahawa.

Mheshimiwa Spika, changamoto ambayo imewakuta wakulima ni kwamba soko limekuwa gumu. Wanalima bila kujua wanauza wapi? Wanalima bila Serikali kuonyesha initiative ni kiasi itaweza kusaidia ili waweze kuzalisha zaidi?

Mheshimiwa Spika, nimeipitia Report ya Agricultural Non-State Actors Forum, inaonyesha ni kiwango gani licha ya research kufanyika na kuainisha changamoto za kimfumo zinazowakuta wakulima wa zao la kahawa, bado changamoto hizo hazijatatuliwa ikiwa ni pamoja na Bodi ya Kahawa kuiwezesha kuwa msimamizi wa zao la kahawa.

Mheshimiwa Spika, pia Shirika la TaCRI ambalo linajihusisha na kufanya utafiti wa magonjwa yanayosumbua kahawa, kuzalisha kahawa mpya na mbinu za uzalishaji bora, limekuwa halipewi fedha au fedha za kutosha kwa ajili ya kufanya hiyo kazi. Utaona kwamba ni juhudi za makusudi za kuhakikisha zao la kahawa mbali na kukosa soko, linazidi kudidimia.

Mheshimiwa Spika, pili, changamoto kubwa ambayo wananchi wamezidi kuiona, sijui ni kuzuia au nini kimefanyika mpaka Vyama vya Ushirika ndiyo vinaonekana kuwa mnunuzi pekee wa zao la kahawa. Mheshimiwa Waziri Mkuu ameenda Wilaya ya Karagwe na Kyerwa mara kadhaa, lakini sasa ametusaidiaje kutatua changamoto ambayo tunaona chama cha msingi hakijawezesha wananchi kuuza mazao yao kwa thamani ambayo waliitarajia? Msimu uliopita walikuwa wananunua kilo moja kwa shilingi 1,100/=. Msimu huu ambao ni msimu mdogo, tunaita Ndagasa, walipaswa kununua kwa shilingi 700/= lakini vile vile hawajanunua.

Mheshimiwa Spika, watu wana mazao, hawawezi kuuza kokote, mashirika au makampuni binafsi hayawezi kununua, watu wako stranded, watu wanapaswa kupata fedha ya kupeleka watoto shule, wanapaswa kujiendeleza katika maisha yao, hayo mambo yote yamekuwa ni magumu. Changamoto ni kwamba watu wamezidi kuwa masikini na kuna msemo unasema, watu wa huku wanajikuta wanabaki kuwa masikini, masikini na wa mwisho katika trend ya ranks za maendeleo yamekuwa Tanzania Bara.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, sasa tunaweza kuona ni Serikali inafanya deliberatively kuhakikisha tunazidi kuwa masikini licha ya kwamba tuna nyenzo ya kujikwamua kama wakazi au kama wananchi wa Mkoa wa Kagera.

Mheshimiwa Spika, nimepitia bajeti ya Chama cha Ushirika kwa estimates zao za mwaka 2020/2021…

SPIKA: Mheshimiwa Anatropia, umesema Serikali inafanya makusudi!

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kushindwa kubadilisha mifumo ambayo inaendelea kukandamiza wakulima wa kahawa ni sawasawa na kufanya makusudi ili wananchi wazidi kuwa masikini. Hakuna namna nyingine nitakayoitumia kwa sababu kama tutaondoa vikwazo, kama tutajaribu ku-encourage…

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Unapewa taarifa Mheshimiwa Anatropia. Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, tafadhali.

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza zao a kahawa, ni kweli kabisa wakulima wa Kagera wanalima vizuri sana na wanajitahidi sana kulima, Serikali kwa kuona changamoto za masoko ilichukua hatua za dhati kabisa za kuimarisha Vyama vya Ushirika ikiwa ni pamoja na kuwapatia fedha Vyama vya Ushirika ili viweze kununua kwa wakulima na kuhakikisha wanapata bei nzuri. Hii imefanyika vizuri sana na vyama vingi vimefanikiwa katika hilo eneo.

Mheshimiwa Spika, pia tuliweza kuhakikisha kwamba tunazuia wale walanguzi ambao walikuwa wanachukua kahawa na kwenda kuipeleka nchi jirani. Zaidi ya hapo, tumeiwezesha Bodi ya Kahawa kuisimamia vizuri sana na ndiyo maana uzalishaji umeongezeka na bei imeimarika.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, haya anayoyasema kwamba Bodi ya Kahawa imesahaulika, Vyama vya Ushirika havijasaidiwa, havina uwezo, labda atuambie ni chama gani ambacho hakina uwezo? Kwa sababu kwa takwimu za Serikali ni kwamba tumeviwezesha vya kutosha na kuna mchango mzuri sana ambao unaendelea.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba kumpa hiyo taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Anatropia unapokea taarifa hiyo?

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, kwa mujibu ya ripoti niliyoisoma ambayo ukitaka nitakupatia na iko online inasema...

SPIKA: Ripoti hiyo kutoka wapi yaani? Ili tuweze kufuatilia wote maana hii ni ya Serikali. Hiyo yako ni ya kutoka wapi?

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, ni ANSAF ambao ni wadau.

SPIKA: ANSAF ndio…

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, wanaita Agriculture Non Sector Actors Forum.

SPIKA: Sasa forums hizo, yaani wewe una...

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, wamefanya utafiti, wana data…

SPIKA: Sasa upande huu umepewa taarifa halisi za Kiserikali.

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nami ndiyo nataka niseme, utafiti walioufanya umeonyesha kwanza vyama vyenyewe vimekuwa havina wataalam hata wa kukidhi mahitaji ya vyama husika. Hiyo nitasema. Nilitaka niunganishe na taarifa ambayo niliyosoma estimate ya Chama cha Ushirika.

SPIKA: Huo utafiti umekuwa vetted na TBS? Bureau of Statistics?

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, imekuwa published. Kwa hiyo, kama iko published, assumption ni kwamba imekuwa satisfied. (Makofi)

SPIKA: Haya bwana, kama hao ANSAF unawaamini, endelea tu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ni kengele ya kwanza eeh!

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Ni kengele ya kwanza.

SPIKA: Ni ya kwanza.

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nilitaka nimjibu, wameonyesha changamoto iliyopo kwenye management halisi ya Vyama vya Ushirika, lakini hiyo imeonekana hata kwenye bajeti husika. Bajeti ya Chama cha Ushirika ambayo inaonekana estimate zaidi ya shilingi bilioni 1.5 itaenda kwenye Managerial Activities kulipa fidia, kuhamisha kutoka eneo moja kwenda lingine na hii naweza nikakupatia, ambayo inaonekana fedha nyingi inatumika kwenye Managerial Activities na siyo kulipa wale wakulima wenyewe.

Mheshimiwa Spika, hii inaonyesha kwamba activities za ku-run au activities za kuandaa zao la kahawa, cost moja ya kilo itakuwa ni zaidi ya shilingi 1,700/= wakati wakulima wanaweza kuuza kwa shilingi 1,300/=. You can imagine kwamba anayelima kwa zaidi ya miaka mitano...

SPIKA: Hiyo ni bajeti ya Chama cha Ushirika cha Kagera ambako na wewe unatoka.

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Ndiyo.

SPIKA: Nanyi ndio wanachama wa hicho Chama cha Ushirika.

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Ndiyo, ndiyo, ndiyo.

SPIKA: Sasa unamlaumu nini Waziri wa Kilimo katika hilo kwa mfano?

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika ninaiambia Serikali na huo ndiyo wito ninaoenda kuutoa kabla sijamaliza. Serikali ni lazima ifanye study kuona ni namna gani inaweza ikasaidia kwenye kuimarisha zao la kahawa badala ya mbinu tulizonazo leo za kutumia Vyama vya Ushirika ambavyo vimekuwa havina uwezo na uzoefu. Hiyo ya kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ya pili, tunaposubiri madalali, middle men watoke Ulaya au wapatikane hapa katikati waende Ulaya watutafutie soko ili sisi tuuze, ni lazima Serikali iangalie, tunawezaje ku-penetrate kwenye soko husuka ili tuweze kuuza; Mheshimiwa Rais anasema win win situation. Kwa nini win win situation tunazitaka kwenye madini; tunazitaka kwenye dhahabu; hatuzitaki kwenye kahawa? Sasa ni lazima tutengeneze mkakati hata wakulima wetu wafaidike kama ambavyo tunataka wafaidike kwenye mazao mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wito wangu mwingine, kwa nini minada ifanyike kwenye Mikoa ya Kilimanjaro? Hii nairudia kwa mara nyingine. Hii ikifanyika kwenye mkoa husika kama Kagera, itasaidia kuondoa gharama za usafirishaji zinazohusika kwa ajili ya kufuata mnada wa Kilimanjaro.

MHE: INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Unapewa taarifa na Mchungaji.

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba nimpe taarifa mchangiaji anayechangia kwamba kuna jambo ambalo amesema kuwa Vyama vya Ushirika ndiyo wanunuzi wa kahawa. Vyama vya Ushirika siyo wanunuzi wa kahawa, ni wasimamizi; na suala la mnada limekuwa likifanyika Mkoa wa Kagera. Mwaka 2019 limefanyika na wanunuzi wote waliwatangazia wenye bei nzuri wakanunue. Pamoja na hizo changamoto zilizopo kwenye kahawa, lakini minada imefanyika Kagera, lakini Vyama vya Ushirika siyo wanunuzi, ni wasimamizi.

Mheshimiwa Spika, ahsante.

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nadhani anaji-contradict.

SPIKA: Anakwambia Jimbo limejaa. (Kicheko)

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nami nataka kukwambia hii ni pressure ya Jimbo na nimelikalia hasa! (Makofi/Kicheko)

Hiyo ni pressure ya Jimbo na ninalikalia hasa!

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Tukutane kazini. (Makofi/Kicheko)

SPIKA: Malizia, malizia, bado dakika moja.

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Spika, bado kama Serikali mna nafasi ya kuwasaidia wakulima wa Mkoa wa Kagera. Msiwaletee fedha, msiwaletee dhahabu, tusaidieni kwenye zao letu la kahawa, tupatieni soko, lakini ruhusuni biashara huria. Mbona maeneo mengine biashara huria inafanyika? Bodi ya Kahawa itabaki kama refa iangalie nani anacheza rafu; na lengo kubwa ni kuwasaidia wakulima wetu waweze kufaidika kwa mazao yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)