Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Joseph Osmund Mbilinyi

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mbeya Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa hii ni bajeti ya mwisho katika miaka mitano. Naomba nimpongeze sana Mwenyekiti wa CHADEMA na Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Mheshimiwa Mbowe kwa Uongozi wake imara wa kujenga upinzani credible na sio upinzani magumashi pamoja na yote anayokutana nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia nawapongeza Wabunge wenzangu wote wa CHADEMA tuliovuka, ambao hatukuunga mkono kwa sababu tumevumilia sana miaka mitano hii Awamu ya Tano haikuwa rahisi, siasa zilikuwa zinahusika na magereza kushambuliwa, kupigwa risasi na mambo mengine mengi tu ambayo tumeweza ku-survive mpaka hapa tulipofika kwa kweli nawapongeza sana Wabunge wenzangu kwa kuvuka uvuli wa mauti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa suala la Corona lipo chini ya Waziri Mkuu, naomba nianzie huko. Kwanza lazima tuelewane hapa, suala la Corona sio suala la kiimani ni suala la sayansi. Na ndio maana hata Papa mwenyewe, mimi ni

mkatoliki amefunga Vatican na Italy yote hawaendi kanisani hata St. Peters Basilika ambapo kila jumapili maelfu kwa makumi ya maelfu ya watu duniani kote na Waitaliano wanasali pale juzi Papa amesali peke yake kwa sababu ya kuchukulia umakini wa suala hili. Hili suala sio la kiimani na imani tunayo kwa mfano sisi Wakatoliki tuna imani lakini tunaamini sayansi na ndio maana kila unapokuta Kanisa Katoliki lazima utakuta shule ya Chekechea na Zanahati kwa sababu tunaamini katika Sayansi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Corona ni pandemic, wakishasema kuna epidemic, ilianza kama epidemicsaa hizi inaitwa pandemic hakuna suala la kutishana hapa, ni suala la ku-discuss kwa kina. Corona inaua na itaua mamilioni, ndivyo wanasayansi wanasema hivyo tusipochukua hatua. Tushirikiane kukabili na hili, tusilete siasa kwenye hili na niwapongeze sana Zanzibar kwenye hili Zanzibar wamechukua hatua sana wamefanya vizuri sana, unamuona pale yule Waziri wa Afya, yupo on point kila time kujaribu ku update hali ya mambo inavyokwenda. Corona sio tatizo la Ummy Mwalimu na Wizara ya Afya, maana yake watu Ummy, Ummy, Waziri wa Fedha anahusika, Waziri wa Biashara anahusika Waziri wa Uwekezaji anahusika kwa sababu biashara zinakufa.

Mheshimiwa Spika, BOT wako kimya tu kwa hiyo tunaangalia tu upande wa vitanda matibabu tutakufa ni kweli huko tupo ovyo lakini njia pekee ya kuidhibiti korona kwa nchi maskini kama sisi Tanzania ni kudhibiti isisambae. Sasa nyinyi mnasema mbona hamwagi nini ile hamsanitize miji, kama Arusha, mgonjwa wa kwanza tulitakiwa tuone hata yale magari ya polisi basi yale ya washawasha, wekeni dawa yamwage maji mitaani, mnasubiri mpaka muwamwagie maji CHADEMA wazee! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, m-sanitize miji angalau ile ambayo imeanza kupata shida ndugu zangu, hiyo ndio njia ya pekee ya ku-contain ili isisambae sana, Ikisambaa sana hatuwezi ventilators tunazo mia moja na hamsini tu. Tunavyoambiwa tunazo mia moja na hamsini tu, wakati Jiji la New York wanahangaika zifike laki moja na nusu, sisi kama Taifa la watu milioni hamsini na saba tunazo mia moja hamsini tu, Itakuwa balaa hapa. Spain wanafikia time wanasema wazee wa miaka themanini wasipewe vitanda vya ICU kwa sababu vitanda vimeisha hapa tutatumia vigezo gani au kukata, shika laki mtoe Sugu muweke Mheshimiwa Jenista na kadhalika, kwa sababu tutafanyaje. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hili suala la korona ni serious, hata kama sisi sio UK hata kama sisi sio Italy, hata kama sio US lakini tuangalie wenzetu wa sub-Sahara wanafanya nini, sub-sahara in Africa, Kenya. Basi tusiwaambie wenye nyumba wasitoze kodi kwamba nyumba nyingi hapa ni za watu binafsi na ni masikini wanategemea hizo kodi kusomesha watoto. Lakini watoto si hawaendi shule, elimu si bure, okay tusifike huko tuweke unafuu kwenye yale ya Serikali, hii Serikali si ina hela hii mara ya mwisho Mheshimiwa katuambia tuna akiba ya dola za kutumia miezi sita. Where is that money, bring that money tupange bajeti hela ya bajeti ya Mwenge, bajeti ya Mwenge haitoshi kwenye corona. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haitoshi watu wanapanga bajeti za kufa mtu, bajeti kubwa na mikakati. Kenya Serikali inatoa miongozo, umeme, maji hivyo ni vya Serikali. Mseme bwana tuko vizuri nchi hii tajiri umeme, maji iwe bure kwa wananchi ili kuwaletea unafuu kuanzia sasa ili pale anapopanga ule mchango wa LUKU, mchango wa maji usiwepo tutakuwa tumewapa unafuu wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini mabenki Kenya yamesitisha marejesho ya mikopo kwa biashara na makampuni. Hili sio suala la wananchi maskini, hili suala ni la kitaasisi, Mheshimiwa Dkt. Mpango this is yours na BoT, sitisheni wekeni breki kwenye marejesho kwa sababu bila hivyo hizi biashara zitakufa Corona inakuja kupita Mungu anatusaidia tutashindwa kunyanyuka kwa sababu hakuna biashara itakayonyanyuka na Serikali haiwezi kuajiri watu wote na itakuwa shida sana kwetu sisi sote.

SPIKA: Mheshimiwa Sugu naona kila jambo una copy and paste from Kenya.

MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Spika, hapana nitakupa mfano wa Ghana Serikali ipo serious, Ghana imesema wananchi kuanzia Jumapili hii wote wakae ndani Taifa zima linaenda kupimwa kwa sababu huwezi kujua ukubwa wa tatizo bila vipimo. Hii hapa mnasema eti tuko ishirini, ishirini tupime humu tu Bungeni hata mimi mwenyewe sioni kama niko guarantee na niko salama.

SPIKA: Tunaposema Mheshimiwa Sugu, hiyo unayosema Ghana wanasema watu wote wakae ndani ili Serikali ya Tanzania unayosema watu wote wakae ndani ili Oktoba uchaguzi kule Mbeya uhairishwe, hiyo sasa ndio tunasema haiwezekani.

MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Spika, kwenye uchaguzi nakuja, naomba tu utunze muda wangu.

SPIKA: Muda wake muutunze. (Makofi/Kicheko)

MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Muutuze muda wangu, kwenye uchaguzi nakuja, tuko vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naongea habari hizi serious sana, nyakati kama hizi zinaitwa defining moments. Nyakati kama hizi ndio leadership inapimwa, tutoke tuonyeshe leadership watanzania wanatuangalia. Kwa sababu hawa watu wanatushangaa kwamba aaah korona wanasema tunanii mbona wao wapo Bungeni eeeh! Kwa hiyo, lazima humu ndani tuwaonyeshe kwa nini tuko Bungeni, tujadili vitu vya kuokoa maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kauli yake kuwa uchaguzi utakuwa huru na wa haki, umezungumzia uchaguzi nakuja huko. Uchaguzi uwe huru na wa haki Mungu atupunguzie makali ya Corona ili tufike salama Oktoba, Mungu atusaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ili kutuhakikishia kwamba uchaguzi huu uwe huru na wa haki Rais achukue hatua chanya ku-support kauli zake. La msingi kabisa ili wadau wa uchaguzi, wa ndani, wa nje, wa kimataifa maana yake uchaguzi ni suala la wote, wadau wawe na imani nae wawe na imani na kauli yake kwa kuanza kabisa tunataka Tume huru. Tume ambayo watendaji wake watawajibika kwa tume na sio kwa mteuzi ambaye ni Rais. Tume ambayo yenye kinga na ulinzi wa kikatiba ya ajira za wale watendaji wa Tume kama ilivyo kwa majaji, kama ilivyo kwa CAG. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Isiwe rahisi kumchomoa Mtendaji Mkuu wa Tume hajatangaza tu hajamtangaza Sugu kesho hawi Mwenyekiti wa Tume, that isvery bad. Kuhusu Mbeya na Uchaguzi Mkuu kule tunasema hivi, Tume huru bila Tume huru lazima tutoboe mradi wananchi wametupa kura. (Makofi))

Mheshimiwa Spika, by the way Mbeya mimi hamjawahi kunipa kwenye silver plat. Uchaguzi wangu wa 2010 alikufa mtu mmoja kwa ajili ya kulinda kura, uchaguzi wa 2015 vilema watatu wengine mpaka leo nawahudumia. Uchaguzi huu na maisha yalivyokuwa magumu sijui mtatuzika wangapi Mbeya hata Corona inaweza ikawa na nafuu lakini sio kuchakachua uchaguzi huu kwa kigezo chochote kile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maana yake nawaona tu sasa hivi hawasemi tena kama kule Mbeya, hawasemi tena Sugu hashindi wanasema Sugu hatatangazwa, utafikiri nimewahi kutangazwa wakati nimelala nyumbani. (Makofi/Vicheko)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunataka Tume huru, yenye uwezo wa kuteua wasimamizi na watumishi wake yenyewe isiteuliwe, na haya maelezo yote haya tumeiweka kwenye hotuba ya KUB lakini pia yamo kwenye barua yetu tuliyomuandikia Mheshimiwa Rais kumpa mapendekezo ya tunaenda vipi Oktoba baada ya sisi kutoka Mwanza kwenda kuonesha kitambaa cheupe kwamba tupo tayari kwa maridhiano nilikuwepo kwenye ile…

SPIKA: Mheshimiwa Sugu, samahani kidogo kuna taarifa nadhani ni Naibu Spika au ni nani taarifa, malizia Mheshimiwa Sugu. (kicheko)

MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Spika, kama chama tumeandika barua kwa Mheshimiwa Rais mpaka leo haijajibiwa kutoa mapendekezo yetu, tunaenda vipi kwa amani kwenye uchaguzi wa Oktoba. Msisitizo wake na msingi ukiwa Tume huru. Kama Tume huru na haki basi turuhusiwe katika sehemu ya hizo haki turuhusiwe kupinga matokeo ya Rais Mahakamani. Mbona matokeo ya Mbunge tunapinga, ile mwaka 2010 yule alinipinga nikamtuliza na Mahakamani mwaka 2015, hakupinga kabisa kwa sababu kura zilikuwa ni nyingi mno. Mwaka 2020 hata njia ya Mahakamani hamtaiona nyinyi kwa Mbeya Mjini,hamtaiona hata njia ya Mahakamani. (Makofi/Kicheko)

MBUNGE FULANI: Taarifa Mheshimiwa Spika.

MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunataka tume huru tunataka sheria, Marekebisho ya Sheria za Uchaguzi, tunataka marekebisho ya Sheria za Uchaguzi…

SPIKA: Kengele imeshagonga tayari Mheshimiwa Sugu.

MHE. JOSEPH O. MBILINYI:…ili Rais nae akichakachua tumshitaki Mahakamani kwamba amechakachua uchaguzi. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)