Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, nakupongeza sana kwa hotuba nzuri sana yenye ufafanuzi mzuri sana wa Sekta ya Elimu. Pili, naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja. Pamoja na kuunga mkono hoja hii, naomba kuchangia maeneo yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani Wizara ya Elimu na Wizara ya TAMISEMI washirikiane kuhakikisha kwamba suala la madawati linakwisha na wanafunzi wote kuanzia Shule za Msingi na Sekondari wanakaa kwenye madawati siyo kukaa chini. Hii inaathiri sana taaluma na ni suala la aibu, karne ya 21 bado wanafunzi wanakaa chini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Shule ya Mpwapwa Sekondari (Mpwapwa High School) ilianzishwa mwaka 1926. Hivi sasa shule hiyo imechakaa sana na haifanani kabisa na hadhi ya Shule ya Mpwapwa Sekondari ya zamani. Je, Serikali ina mpango gani wa kuzikarabati Shule za Sekondari Kongwe kama vile Mpwapwa Shule ya Sekondari, Msalato Sekondari na Kilakala Sekondari? Nashauri suala hili wasiachiwe Wizara ya TAMISEMI peke yao, lazima na Wizara ya Elimu ishiriki kikamilifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha zinazotengwa kwa ajili ya chakula cha wanafunzi wa sekondari za bweni ni kidogo sana na kusababisha kila mwanafunzi kupata shilingi 1,500/= kwa siku, yaani chai/uji, chakula cha mchana na jioni. Hela hiyo haitoshi kabisa, dola moja kwa siku. Nashauri Serikali iongeze angalau ifike shilingi 2,500/= kwa kila mwanafunzi wa bweni. Wanafunzi lazima wapate chakula ambacho ni balanced diet (carbohydrates, vitamins na proteins) siyo ugali na maharage kila siku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kufutwa kwa ada, wananchi wamelipokea suala hilo kwa furaha sana na uandikishaji wa wanafunzi Darasa la Kwanza umeongezeka sana kuliko ilivyokuwa mwanzo. Waliogopa ada na michango mbalimbali. Shule ya Sekondari ya Mpwapwa ni Kongwe lakini mpaka sasa haina gari na ni muda mrefu sana. Je, ni lini shule hii itapatiwa usafiri wa gari? (wapo Wanafunzi 600)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Chuo cha Ualimu cha Mpwapwa kilianzishwa mwaka 1926. Chuo hicho kinahitaji ukarabati mkubwa zikiwemo nyumba za Walimu. Kuna baadhi ya nyumba hazijafanyiwa ukarabati, sasa ni zaidi ya miaka 20, zimechoka sana. Ni lini Chuo na nyumba za Walimu zitafanyiwa ukarabati mkubwa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu upungufu wa Walimu katika shule zote za Sekondari za kutwa, naishauri Serikali ihakikishe kila shule iwe na Walimu wa kutosha na wa masomo yote ili kuboresha taaluma katika shule hizo. Maslahi ya Walimu yalipwe mapema ili kupunguza malalamiko ya Walimu. Naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.