Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hoja iliyoko mbele yetu. Awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa uwasilishaji wa hotuba ya ofisi yake. Pia naomba nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli, na Serikali yake kwa ujumla jinsi wanavyofanya kazi tumeona katika miaka yote minne iliyopita Serikali yetu imefanyakazi nzuri tumepata mafanikio makubwa sana maendeleo yameonekana nampongeza sana Mheshimiwa Rais na Serikali yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikiendelea kuipongeza Serikali niipongeze sana Serikali kwa janga hili ambalo sasa linatukabili la corona Serikali ina jitahidi kutoa elimu inajitahidi kukabili tatizo hili na imeandaa kila aina ya misaada kwa wananchi nikuombe sana niombe sana sasa Serikali ikiwezekana iwaandae wananchi zaidi juu ya hali halisi ya corona ilivyo duniani na watanzania waambiwe bayana kabisa kwamba hali hii ikiendelea kuwa mbaya itabidi tukae ndani. Hivyo kila mtu akae akijua kwasababu hii ndiyo hali ya dunia ilivyosasa kwamba kule ambako corona imechachamaa watu wote sasa wanakaa ndani si vibaya kwa Serikali yetu kutamka hivyo kwamba watanzania tujue kwamba kama hali itaendelea kuwa mbaya tutakaa ndani ili kuhakikisha kwamba tunaepukana na tatizo hili la corona.

Mheshimiwa Spika, lakini wako wadau wanajitahidi sana kutusaidia kutoa elimu kwa wananchi ni mpenzi sana kusikiliza Radio One kwa kweli wanajitahidi kweli kweli Radio One kutangaza kutoa muda wao wa asubuhi zaidi ya masaa matatu wanazunguka mitaani wakielimisha wananchi. Jana nimeshuhudia mtangazaji anaongea na mtu wa daladala, mtu wa daladala anasema nina maji nilikuwa na sabuni lakini sabuni yangu imeibiwa mtangazaji anatoa fedha yake mfukoni anampa mtu wa daladala kwamba nunua sabuni nyingine ili kusudi abiria wako waendelee kupata huduma. Kwa kweli ni jambo ambalo linaonekana vyombo vya habari vimehamasika na wananchi wengi wamehamasika. Kwa kweli naipongeza sana Radio One kwa hilo waendelee kutoa elimu kwa wananchi na vyombo vyote vya habari viendelee kutoa elimu.

Mheshimiwa Spika, nikiacha hiyo habari ya ugonjwa wa corona, nije kwenye hoja ya Waziri Mkuu tuna tatizo kubwa sana la maji kama nchi lakini sasa ni takriban tunakwenda huu ni mwaka wa tano tumekuwa hapa Bungeni tukiambiwa miji 26 itapewa fedha ya kutengenezewa miradi ya maji na huu ulikuwa ni mkopo toka India miaka mitano inakwisha toka tunaanza Bunge hili tumekuwa tukiambiwa miji 26 itapewa fedha miji 26 mara muambiwe sijui kuna sijui kuna no objection sijui mara nini yaani tunaweza kusema ni hadithi tu zimekwenda mpaka tumefika leo tunafika mwaka wa tano hakuna maji kwenye miji 25 na wananchi wanaendelea kutudai maji na sisi tumekuwa tukiahidi na Serikali imekuwa ikituahidi.

Mheshimiwa Spika, naomba Waziri Mkuu atakapokuwa anahitimisha hoja yake atuambie kwamba hii miji 26 ambayo tuliambiwa itapewa maji, ikiwemo mji wa Njombe ni lini sasa itapewa maji na kama hiyo ya India imeshindikana kwa sababu kama jirani ameshindwa kumpa mwanao chakula mwenye mtoto si umpe chakula mwanao? Au utaacha mtoto afe tu eti kwasababu jirani aliahidi atampa chakula. Kwa hiyo, nafikiri tubadilishe utaratibu tuendelee na utaratibu kama nchi tuipe maji hii miji kwasababu maji ni uhai, maji ni afya na maji ni maendeleo.

Mheshimiwa Spika, nipongeze sana Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kazi nzuri kubwa anayoifanya ya kurithisha ujuzi. Kazi hii ya ujuzi ni kazi muhimu sana vijana wengi sasa wameanza kupata ujuzi ninachokiomba kwenye idara ile inayoshughulika na ujuzi ipanue nafasi iende mpaka kwenye nafasi za fani za kilimo, fani za ufugaji kwa sababu kilimo na mifugo ndiyo itaajiri watu wengi nimeona wanatoa kwenye ufundi wa magari, umeme, na nini hivi yaani katika vijana tulionao katika nchi hii hao mmewasaidia vijana wa mjini lakini vijana wa vijijini watasaidiwa kwa kupelekwa kwenye fani za kilimo na fani za mifugo tutakuwa tumewasaidia vijana wengi wa vijijini kupata ujuzi na tutumie vyuo vingi zaidi tusitumie vyuo hivi vitatu tu Don Bosco, DMI, DTI hapana tuende vyuo vingine.

Mheshimiwa Spika, iko private sector ina vyuo vingi tu ambayo inaweza ikasaidia kutoa ujuzi huu. Kwa hiyo, niombe sana hilo Mheshimiwa Waziri Mkuu mliangalie na msaidie vijana wengi zaidi ili kusudi wapate ujuzi kwa sababu ujuzi pekee ndiyo utawafanya vijana wa nchi hii kuweza kujiajiri na kuweza kufanya kazi katika ulimwengu huu unaokwenda sasa watanzania ya viwanda.

Mheshimiwa Spika, nimeona katika hotuba ya Waziri Mkuu akizungumza habari ya benki ya kilimo. Benki ya kilimo imefanya kazi nzuri miaka mingi tumekuwa tukilalamika sana juu ya benki ya kilimo lakini kwa sasa benki ya kilimo inaonekana imefanya jitihada kubwa sana binafsi nimemuona Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya Kilimo akipita kwa wadau mbalimbali na wananchi mbalimbali kuhamasisha na kuangalia miradi ambayo wanaweza wakakopeshwa na benki

Mheshimiwa Spika, niombe Serikali iendelee kuisimamia hii benki na benki yenyewe iendelee kujituma zaidi kushuka chini kwa wakulima wa kawaida kama vile anavyofanya Mkurugenzi wao basi watumishi wote ndani ya benki ile wafanye hivyo kwamba wawatembelee wananchi waone mahitaji ya wananchi wakulima ni nini. Lakini mara nyingi nimekuwa nikisimama hapa mbele yako nikilalamika sana juu ya matrekta, matrekta mengi wanayokopeshwa watanzania ni mabovu, matrekta mengi wanayokopeshwa watanzania hayakidhi haja ya kilimo tunaletewa katika nchi matreka ambayo hayana sifa. Taasisi zote zinazoleta matrekta zinaleta matrekta zinaleta matreka ambayo kwa kweli uimara wake na ubora wake ni chini sana. Kwa hiyo, niombe sana Serikali ilione hilo.

Mheshimiwa Spika, na mwisho kabisa ni suala la UKIMWI, tatizo la UKIMWI ni kubwa sana lakini ukubwa wa tatizo hili, sisi watanzania ni kama vile tumeufumbia macho. Kiwango chetu cha kutoa elimu kiende kwenye taasisi zilizochini kwa mfano halmashauri mimi ni mjumbe wa kamati ya Ukimwi lakini unakwenda pale halmashauri unakutana na watu ambao ni wajibu wao kutoa hiyo elimu lakini hawajui chochote hawatoi elimu na wala hawana data zozote niombe Serikali ilione hilo jambo liende lisimamiwe mpaka ngazi ya chini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini mwisho kabisa ni mfuko wa UKIMWI ATF hatuna mfuko, tunao mfuko wa UKIMWI lakini Serikali haichangii hatuna tozo mahala ambalo linasaidia kuingia kwa ajili ya mfuko wa UKIMWI, tunategemea kupata huduma ya dawa hizi za Ukimwi ARV kutoka kwa wafadhili. Leo hii wafadhili wanapambana na corona na inawezekana corona ikawabana sana wakaendelea kuhudumia watu wao tu sisi ambao tunategemea msaada kutoka kwao tutakwama na tusipokuwa na ARV maana yake sasa watanzania tutaanza kufa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naiomba Serikali iweze kuhakikisha kwamba inatafuta tozo yoyote ambayo watanzania tutachangia kwa ajili ya mfuko wa UKIMWI ili kusudi tuwe na mfuko wetu wa kujitegemea kuliko kutegemea wafadhili ambao leo hii mfadhili mkubwa ni Marekani, Marekani leo ana corona 200,000 na wanaendelea kupambana sasa atatukumbuka sisi kweli. Kwa hiyo, hii ni hatari sana kwetu na niombe sana Serikali iangalie hilo namna gani tutafanya tupate tozo ya aina yoyote ile iwe ni maalum kwa ajili ya masuala ya UKIMWI. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo ninakushukuru sana kwa fursa, ahsante sana. (Makofi)