Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie hoja hii muhimu iliyo mbele yetu kuhusu bajeti ya Serikali na hali ya uchumi. Nichukue nafasi kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyenipa afya na uzima nimepata nafasi hii ya kuchangia.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuunga mkono hoja asilimia 100 kwa sababu ya mambo mazuri yaliyokuwepo ndani ya suala hili. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na wataalamu wote wa Wizara ya Fedha na taasisi zake.

Mheshimiwa Spika, nianze kujibu hoja mbalimbali zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge. Kwanza nichukue nafasi hii kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge waliochangia kwenye hoja zile zinazohusu sekta ya kilimo na nitatoa ufafanuzi wa hoja chache lakini tuwaahidi kwamba michango yao yote ina umuhimu mkubwa kwa mustakabali wa kilimo chetu nchini lakini kwa maendeleo ya Taifa letu. Michango yote tutaifanyia kazi na wale ambao hoja zao nitakuwa zijazigusa kutokana na muda basi Wabunge wote mtazipata kwa maandishi ndani ya muda mfupi.

Mheshimiwa Spika, nianze kwanza kwa hoja ya pamba uliyosema maana muda wenyewe ni mchache nisije nikamaliza kabla sijagusa suala hilo. Kwanza, ni kweli soko la pamba haliendi mwendo mzuri na tumefungua msimu tangu tarehe 2 Mei lakini mpaka sasa mwenendo wake sio mzuri. Tulishatoa bei elekezi ya Sh.1200 lakini kwa bahati mbaya wakati bei ile inatoka soko la dunia bei zilianza kushuka hasa kutokana na vita vya kibiashara kati ya nchi ya China na Marekani, kwa sababu nchi ya China ndiyo watumiaji na wanunuzi wakubwa wa pamba na nchi ya Marekani pamoja na kuwa ni wazalishaji wakubwa wa pamba nao wanawauzia China lakini pia ndiyo wanunuzi wakubwa wa nguo kutoka China.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kutokana na msuguano wao na kuwekeana vikwazo, huyu amekataa kununua nguo za kutoka China mwingine amekataa kununua pamba kutoka nchi ya Marekani. Kwa hiyo, wanapogombana mafahari wawili nyasi zinaumia na sisi huku nchi za Afrika ndiyo tunaumia ikiwemo Tanzania na bei imeendelea kushuka mpaka leo.

Mheshimiwa Spika, wakati tunapanga bei pamoja na wadau na wanunuzi bei katika soko la dunia ilikuwa ni zaidi ya dola senti 0.75, leo hii tunapozungumza ni dola senti 0.66 zaidi ya dola senti 0.9 imepungua. Kwa hiyo, wanunuzi kama tunavyofahamu ni wafanyabiashara wameshindwa kuingia sokoni na wameshindwa kupata mikopo kwenye taasisi za fedha hasa mabenki kwa sababu mabenki wamekataa kuwapa mikopo kwa sababu wanasema huwezi kuwapa mikopo wakati kwenye biashara hii anaenda kutengeneza hasara.

Mheshimiwa Spika, kama Serikali tumefanya vikao mbalimbali na kikao cha mwisho kimefanyika siku tatu zilizopita Dar es Salaam na wanunuzi wote tumekubaliana kwamba wataingia sokoni kununua kwa bei ileile Sh. 1200 na Serikali tumeweza kudhamini mikopo yao kutoka kwenye benki na tumewaelekeza kwamba wasiuze pamba hiyo mpaka mwezi Agosti, kama watauza pamba hiyo kwa hasara Serikali tutafidia hilo gap la hasara lakini bei iendelee kuwa Sh.1200. Kwa hiyo, sasa hivi wako kwenye harakati mbalimbali za ku-finalize na benki ili wapate hela wataingia sokoni muda siyo mrefu.

Mheshimiw Spika, hoja ya pili ambayo imezungumzwa na watu wengi ni kuhusu bajeti ndogo ya sekta ya kilimo. Kwanza, tunavyofahamu bajeti yetu ni cash budget tunakwenda kutumia kutokana na tulichokipata lakini kama Serikali kila mwaka tumeendelea kuiongeza bajeti hii. Mwaka uliopita 2018/2019 katika Wizara ya Kilimo bajeti ilikuwa ni shilingi bilioni 204 lakini mwaka huu tumewekewa zaidi ya bilioni shilingi 254, kuna ongezeko la shilingi bilioni 50 kwa mwaka mmoja.

Mheshimiwa Spika, pia sekta ya kilimo ni mtambuka, usiangalie tu kwamba Wizara ya Kilimo. Tumesema mapinduzi ya kilimo yataongozwa zaidi na ASDP II ambaayo inatekelezwa na Wizara zaidi ya nane. Kwa hiyo, ni vema kuangalia na bajeti hizo za Wizara zingine ambazo zote zinakwenda kusherehesha suala la kilimo.

Mheshimiwa Spika, kuna suala la bajeti ya Wizara ya Viwanda, Wizara ya Ardhi, kwa sababu kilimo huwezi kulima kwenye angani, unatakiwa kulima ardhini. Kwa hiyo wanapoenda kupima mashamba na maeneo ya kilimo wanatekeleza SDP II. Kuna Wizara ya Uvuvi na Mifugo, Wizara ya TAMISEMI, Ofisi ya Waziri Mkuu, Uwekezaji, zote hizi bajeti zao pamoja na Wizara ya Maliasili na Utalii upande wa misitu ambao ndiyo kilimo chenyewe, zote zinatekeleza SDP II mapinduzi makubwa ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, katika sisi Wizara ya Kilimo tuna taasisi zaidi ya 22, bajeti zake haziko hapa kwenye bilioni 254, hizi bajeti zake ziko kwenye Mfuko wa Hazina kwa sababu hizi taasisi zetu nyingine zinaripoti kwenye Mfuko wa Hazina. Tuna bajeti zaidi ya bilioni 69 kuanzia Bodi za Mazao pamoja na taasisi nyingine. Pia tuna makusanyo mbalimbali, mapato mbalimbali kwenye Bodi zetu, kama wanavyofahamu kule kwenye pamba tuna Sh.100 kwa kilo kwa ajili ya Mfuko wa Pembejeo na Bodi nyingine ziko kama hivyo. Zote hizi zinakwenda kutekeleza bajeti ya kilimo, kwa hiyo kwa bajeti ya kilimo ni pana sana huwezi kuiona tu kwenye Wizara moja hii Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Spika, la tatu, wamechangia Wabunge wengi kwenye suala la uwekezaji kwenye kilimo cha umwagiliaji kwamba ni kweli na wengine wamefika mbali, wanasema kwamba Serikali haijafanya jambo lolote kabisa, si kweli Waheshimiwa Wabunge. Kama wanakumbuka huko nyuma Serikali katika baadhi ya mikoa tulikuwa tunapeleka chakula cha msaada, upungufu wa chakula.

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Naibu Waziri.

NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)