Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja na naomba niendelee pale nilipokatishwa katika mchango wangu Bungeni. Kwa maoni yangu binafsi TMX iongoze soko na WRS iishie kumsimamia mtunza ghala/mwendesha ghala, na Sheria ya Ushirika ihusike na ukusanyaji wa mazao na kuyawasilisha kwa mwendesha ghala na kusimamia malipo kwa wakulima kupitia AMCOS.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hoja ya mifuko inayotengenezwa na viwanda vitatu nchini kwa sasa ya kuhifadhi mazao, hasa ya nafaka, ili yasiharibike. Mifuko hiyo inapunguza Post harvest loss ambayo kwa sasa ni zaidi ya asilimia 40 hadi chini ya asilimia 10. Mifuko hiyo inakosa soko kwa sababu mbili kubwa. Kwanza VAT ya asilimia 18 inayosababisha bei yake kufikia sh. 5,000/= kwa mfuko mmoja na hivyo wakulima kushindwa kuinunua. Pili wakulima bado hawajaelimishwa faida na umuhimu wa kutumia mifuko hiyo na hivyo kuona bei ya 5,000/= kwa kila mfuko mmoja unaoweza kuhifadhi kilogramu 100 kuwa kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali ifanye mambo mawili. Kwanza iondoe VAT kwenye vihifadhi nafaka ama vifungashio hivyo ili bei ishuke hadi 4,000/= na pili Serikali itoe elimu kwa wakulima juu ya umuhimu wa kutumia mifuko hii maalum ya kuhifadhi mazao ili yatumike kwa mwaka mzima bila ya kuharibika na wapate fursa ya kuyauza wakati bei ikiwa nzuri bdala ya kulazimika kuyauza wakati wa mavuno kipindi ambacho bei inakuwa ya chini sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niipongeze Serikali chini ya Uongozi mahiri wa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa miradi mikubwa ya kielelezo inayotekelezwa; ya SGR, Umeme, upanuzi wa magati ya Bandari za Dar es Salaam Mtwara na Tanga; vile vile ujenzi wa mitambo ya kuzalisha umeme ya Kinyerezi, bwawa la kuzalisha umeme katika Mto Rufiji pamoja na bwawa la kuzalisha umeme kwenye Mto Rusumo. Hakika miradi hii ni ya kihistoria na itatuaondoa kwenye umaskini wa kipato na usio wa kipato.

Mheshimiwa Naibu Spika, historia nyingine ni pamoja na kuhamishia Makao Makuu ya Serikali ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania kutoka Dareslaam na kuja hapa Dodoma. Dodoma ni katikati ya nchi yetu na hivyo kupunguza gharama za uendeshaji wa Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo ni historia ya kitaifa inayoandikwa na Serikali ya CCM ya Awamu ya Tano (5). Kuna historia nyingi zimeandikwa na Serikali hii ya CCM ya awamu ya Tano katika Wilaya zetu zote nchini. Kwa mfano Namtumbo kwa mara ya kwanza Serikali hii iliyoundwa na Mheshimiwa Rais na Makamu wa Rais na Waziri Mkuu Wilaya yetu tumejengewa kituo cha afya kimoja cha Kisasa kabisa, hospitali ya Wilaya, VETA; miradi mikubwa ya maji minne; umeme vijiji 43 kwa mpigo; minara ya mawasiliano katika kata 18 kati ya 21 tulizonazo; zahanati 11 kwa mpigo na kadhalika. Aidha, imetuleletea soko la mazao ya ufuta, tumbaku, soya na korosho pamoja na historia nyingine nyingi. Serikali hii idumu milele na milele, na tusiruhusu awamu nyingine ya utawala iingie.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba vituo vya afya, barabara, minara ya mawasiliano, miradi ya maji, zahanati na masoko ya mazao zaidi ili wata wa Namtumbo tuneemeke.