Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. GEORGE B. SIMBACHAWENE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa dhati kabisa kwa kunipa nafasi ya mwisho kwa leo hii na bila shaka ndiye mchangiaji wa mwisho kwa maana ya wachangiaji wa kawaida katika bajeti ya Serikali. Nianze kwanza kabisa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Manaibu Makatibu Wakuu na Viongozi wa Taasisi zote na Idara zote zilizoko chini ya Wizara hii kwa kazi kubwa na nzuri wanayofanya ya kuhakikisha kwamba, tunakuza uchumi wa nchi yetu, ili tuweze kupata matunza tunayoyataka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza nianze kupongeza kwa Serikali kutekeleza kwa vitendo ahadi ya kuhamishia Serikali Dodoma kama Makao Makuu ya nchi. Ni jambo kubwa ambalo liliahidiwa kwa muda mrefu, lakini limetekelezwa na tunaona kasi yake ambavyo Dodoma inabadilika na mimi kama Mwanadodoma kwa niaba ya Wananchi wa Dodoma niseme jambo hili limetufurahisha. Tunaona namna ambavyo tumepata faida ya moja kwa moja na isiyo ya moja kwa moja na imebadilisha maisha ya watu wetu. Serikali imelifanya jambo hili bila kutumia gharama kubwa, lakini lina tija kubwa sana kwa Wananchi wa Dodoma na sisi tunaoishi Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na niseme tu na nilitaka niwataarifu Wananchi wa Mkoa wa Dodoma kwamba, kwa bajeti ya mwaka huu jumla ya pesa itakayoingia Dodoma kwa ajili ya kutengeneza miundombinu ya barabara tu ni bilioni 175. Bilioni 175 zitapitia TANROADS, zitapitia Halmashauri ya Jiji ya Dodoma na zitapitia kwenye Fungu lile la miradi ya Miji ya Kimkakati, ukijumlisha zote ni kwamba, bilioni 170 na ushee zinaingia Dodoma kwa ajili ya kutengeneza barabara ikiwepo barabara ya mzunguko. Hili si jambo dogo, ni jambo kubwa na tunaipongeza sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, limezungumzwa jambo hapa lililokuwa linahusianisha maendeleo ya watu dhidi ya maendeleo ya vitu na jambo hili limetafsiriwa vizivyo likinukuu Kauli ya Mwalimu Nyerere na ni upotoshaji mkubwa. Na kama kungekuwa kuna Profesa anasahihisha mtihani kwa watu waliokuwa wanachangia wakienda na mtizamo wa hoja hiyo wote wangepata sifuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, alichokisema Mwalimu ni kwamba, maendeleo ni lazima yawe yale yanayotambua pia hali ya usawa, haki na utu kwa maana ya dhana ya usawa, haki na utu kwa sababu ya element za kikoloni zilizokuwepo wakati huo wakati wakoloni wanatuambia tutawafanyia hiki, tutawafanyia hiki, hamna haja ya kudai uhuru kwa sababu, tutawafanyia kila kitu. Akasema hapana, lazima utu wetu, haki, viwepo ndipo tuone uzuri wa maendeleo. Leo kilichotafsiriwa hapa ni kama vile usijenge barabara, lakini uvae nguo nzuri, usijenge nyumba, lakini upulizie perfume, ndicho wanachozungumzia, hiyo sio hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Profesa Shivji alipokuwa anaongea katika mdahalo wa Kigoda cha Mwalimu Nyerere tarehe 25 Machi, 2017 aliondoa utata wa jambo hili. Na katika maeneo aliyosema, alisema namnukuu, “Hakuna kitu kinachoitwa maendeleo ya vitu kutokana na ukweli kwamba, vitu havijiendelezi.” (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia alipokuwa anahitimisha akasema, uhuru bila maendeleo ni ulaghai uliosukwa na walionacho. Uhuru bila maendeleo ni ulaghai uliosukwa na walionacho kwa hiyo, ili uweze kuitafsiri vizuri kati ya maendeleo ya watu na maendeleo ya vitu katika falsafa za kisasa za mendeleo kwa maana ya maendeleo huwezi ukatenganisha hivi vitu viwili. Na ukitenganisha utapata tatizo maana tunajenga miradi mikubwa kwa ajili ya kujenga msingi wa uchumi wa nchi yetu. Tunajenga Airport ili tupate kuingiza fedha zaidi kila kinachofanyika, tunajenga barabara, tunajenga madaraja, tunajenga mradi wa kuzalisha umeme, ili hivi vijenge msingi wa uchumi wetu, uchumi wetu bado ni mdogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunataka Serikali iende kwenye kuzalisha chuma la Liganga, ili tuweze ku-export chuma tupate fedha nyingi. Hii yote ni katika kujenga msingi wa uchumi maana uchumi wetu ni mdogo, lakini hapa mtu anasema eti kwa nini hamuongezi mishahara? Uchumi huu mdogo unaongezaje mshahara?

Mheshimiwa Naibu Spika, ni lazima uanze kujenga uchumi wa nchi kwanza, msingi wake wa uchumi ndio uongeze mshahara, utaongeza hewa tu. Hapa sasa hivi ninyi Waheshimiwa Wabunge na wengi wetu tumeajiri wafanyakazi wa ndani, tumwambie Mheshimiwa Dkt. Mpango hapa aweke kima cha chini shilingi milioni moja kama tutaweza kulipa kwa uchumi tulionao, uchumi wetu hauwezi kubeba. Kwa hiyo, Rais anaposema nipewe muda tuweke mambo sawasawa halafu tutaongeza mshahara kwa kiwango kizuri, lazima tuelewe msingi wake ni nini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa dhati ya moyo wangu ninaamini Serikali inafanya vizuri. Mheshimiwa Dkt. Mpango endeleeni tukamilishe miradi hii mikubwa, ili tuweze kutatua tatizo la msingi na baadaye uchumi wetu uweze kukua, tulionao uchumi wa sasa ni mdogo mno.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)