Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Takwimu zinaonesha kwamba nchi hii takriban asilimia 65 ya wakazi wake wanajihusisha na shughuli ya kilimo wengi wao wakiwa maeneo ya vijijini ukilinganisha na karibu asilimia 97 ambazo tulikuwa nazo miaka ile tunapata uhuru wetu. Sasa hii inatuambia nini, hii inatuambia kwamba kila mwaka asilimia ya watu wanaojihusisha na kilimo inazidi kupungua na matokeo yake tutafika mahali kama ambapo wenzetu USA wamefika asilimia mbili ya wakazi wake ndiyo wanaojihusisha na kilimo na masuala ya ufugaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii 65% ya Watanzania inazalisha chakula kwa ajili yake lakini pia inabidi izalishe chakula kwa ile 35% iliyobakia. Pia hii asilimia 65 inatakiwa izalishe mazao ambayo tunataka yaende viwandani. Vilevile hii asilimia 65 inatakiwa izalishe kwa ajili ya mazao ya kuuza nje ili tuweze kupata fedha za kigeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nafikiri ni muhimu sasa tujiulize swali, hii asilimia 65, je, itaweza kufanya haya yote ambayo tunakusudia iende ikayafanye? Takwimu za Serikali bado zinaonesha kuwa asilimia 53 ya Watanzania inalima kwa kutumia jembe la mkono, asilimia 20 ndiyo inayotumia matrekta, asilimia 27 ndiyo inayotumia wanyama kazi. Kwa hiyo utaona ni dhahiri kwamba kwa asilimia hizi jinsi zilivyo kwa sasa ni vigumu sana kufikia hicho ambacho tunakitaka. Ni wazi kwa kutumia jembe la mkono hatutatoka hapa tulipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nilikuwa nataka kuishauri Serikali hii, kwamba kama kweli inajali wananchi wake wananchi wake hawa ambao asilimia kubwa wameajiriwa na sekta ya kilimo ni lazima ifanye mapinduzi kwenye kilimo hiki ili basi wazalishe kile ambacho tunatarajia wazalishe. Leo katika nchi hii hakuna mkulima anafuraha; wakulima wa korosho wamenuna, wakulima wa alizeti wamenuna, wa kahawa walikwisha kununa wa mahindi ndiyo hivyo halikadhalika. Kwa hiyo ili mazingira haya ya kilimo yaweze kuvutia ni sharti wakulima wapate kile ambacho kitawasaidia ili waweze kwenda kuzalisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, bado bei ya mazao ya wakulima hali ni mbaya sana. Hebu Serikali tuishauri ikubali kuwaunganisha wakulima na masoko ili waweze kupata fedha ambazo zitawasaidia katika mambo yao lakini pia kuchangia kwenye uchumi wa taifa. Hapo nyuma tulikuwa na mikopo ya matreka kupitia Shirika la SUMA JKT, lakini mikopo ile sasa imefutwa, ukitaka trekta inabidi ulipe cash milioni 48, milioni 50. Hivi ni Watanzania wangapi wa vijijini wanauwezo wa wa kulipa shilingi milioni 48 ili waweze kumiliki trekta? Mheshimiwa Mpango wewe ni mkopaji mzuri sana, unakopa nje na unakopa ndani na ndiyo maana Deni la Taifa hadi sasa ni trilioni 51.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba na tunashauri wakulima wakopeshwe matrekta ili wakazalishe vizuri. Kwa majembe yetu ya mikono na kwa kutumia wanyama kazi hatuwezi kutoka hapa ambapo tumefika.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni suala zima la madeni ya Serikali, kama ambavyo nimesema hapa mbele. Walimu, kada ambayo inafanya kazi katika mazingira magumu sana wanaidai Serikali shilingi bilioni 61. Hizo hela za walimu wapewe. Tunafahamu mazingira ya kazi ni magumu miundombinu na kazi ya ni kidogo, tunaomba Serikali ilipe hela za walimu ili walimu wakafanye kazi na wazalishe elimu ya watoto wetu. Ahsante. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tatu ni…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)