Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. SHAABAN O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru na mimi kunipa nafasi niweze kuchangia Wizara hii ya Fedha. Kwanza kabisa nimshukuru mwenyezi mungu mwingi wa rehma kwa kunipa afya na nguvu na mimi niweze kuchangia katika hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimpongeze Rais wangu, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli, then nimpongeze Waziri Philipo Mpango na Naibu Waziri wake Mheshimiwa Ashatu Kijaji na timu yake ya wataalam kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli bajeti hii ni nzuri na imeenda kujibu matatizo ya Watanzania, ile kiu ya Watanzania naamini sasa imepata suluhu kwa bajeti hii. Wale ambao wanasema kwamba asiyepigia kura bajeti hii basi atamshangaa mimi nataka nisema atajishangaa yeye mwenyewe, kwa sababu bajeti hii haijawahi kutokea Mwenyezi Mungu anasema: :Man laa yashkur kalila laa yashkur kathira”; maana yake usiposhukuru kwa kidogo, basi hata kikubwa hutoshukuru. Ina maana mambo yote yaliyofanyika katika nchi hii hawa ndugu zangu wanataka waniambie hawajayaona? Nataka niseme basi tumwachie Mwenyezi Mungu kwa sababu yeye ndiyo mwenye majibu sahihi, lakini Mwenyezi Mungu anajua ameona na Watanzania wameona.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja katika kuchangia, nianze na barabara. Ni ukweli usiopingika kwamba barabara za vijijini ndiyo kila kitu ndizo zinazotoa mazao, ndizo ambazo wakulima wanazitegemea kuliko barabara nyingine. Sasa niiombe Serikali yangu Tukufu kwamba badala ya kutenga asilimia 30 kwa ajili ya TARURA basi watenge asilimia 40; niishauri Serikali yangu Tukufu; mimi naamini Mheshimiwa Mpango hili linawezekana. Wewe mwenyewe unajua kwamba barabara hizi za TARURA ni nyingi kuliko hata hizi za TANROADS. Nikuombe Mheshimiwa Mpango hili uliangalie kwa jicho la huruma ili sasa twende kukidhi haja za wananchi wetu, hususan wale waishio vijijini. Kwa kweli fungu hili la TARURA ni dogo sana ambalo kwa kweli haiwezi kabisa kukidhi barabara za vijijini.

Mheshimiwa pamoja na hayo kuna barabara ambazo zinaunga wilaya hadi wilaya; niishauri au niiombe Serikali yangu sasa ichukue barabara hizi ziingie kwenye TANROADS. Kwa mfano barabara zangu za kutoka Mlola, Makanya, Milingano hadi Mashewa, barabara hii ni barabara ya kiuchumi; nikuombe Mheshimiwa Mpango barabara hii ipandishwe hadhi. Bado kuna barabara ya Dochi, Ngulwi hadi Mombo kilometa 16; barabara hii siyo ya kiuchumi tu, barabara hii sasa itakuwa ni barabara ya mchepuo, hususan barabara yetu ya kuanzia Mombo, Soni hadi Lushoto. Kwa mfano mwaka juzi iliharibika mafuriko yaliingia kule maporomoko yakaziba barabara zaidi ya takriban wiki mbili na wananchi wale walipata tabu sana mpaka mazao yao yakaharibika. Kwa hiyo nikuombe barabara hii angalau ipandishwe hadhi ili ichukuliwe na TANROADS na iweze kutengenezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, niende kwenye kilimo. Kilimo ni uti wa mgongo wa taifa letu na asilimia 65 ya wananchi wa Tanzania ni wakulima. Kwa hiyo niombe sasa hawa Wakala wa Pembejeo wapeleke pembejeo kwa wakati. Wakati wa palizi anapeleka mbolea za kupandia wakati wa kuvuna anapeleka mbolea ya kukuzia; sasa hii jamani tutafika kweli ilhali tunataka kwenda kwenye uchumi wa viwanda?

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo tuangalie na masoko yetu, tuwatafutie wakulima wetu masoko. Mimi naamini kabisa kwamba Serikali hii ni sikivu na inaweza kabisa kutafuta masoko. Ni imani yangu kubwa kwamba kipindi hiki cha 2019/2020 wakulima wetu watapatiwa masoko ya kutosha ili waweze kujikimu katika hali hii, waondokane na hii hali ya kuhangaika huku na kule kutafuta masoko wao wenyewe

Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja kwenye elimu. Tunaenda kwenye uchumi wa viwanda, uchumi wa viwanda huu naamini kabisa unaendana sambamba sasa na kumalizia maabara zetu. Hizi maabara naamini kabisa zikimaliziwa tutaanza kupata watu ambao ni wataalamu kuliko ikifikia hatua tukaenda kutafuta wataalamu nje ilhali sisi wenyewe tuna watoto wetu ambao tukimaliza maabara hizi watasoma elimu kwa vitendo, moja kwa moja wataenda kuhakikisha kwamba wanasimamia viwanda hivi ambavyo vitafunguliwa; mimi naamini hii inawezekana. Kwa hiyo nikuombe Mheshimiwa Mpango sasa twende kumalizia maabara hizi, lakini sambamba na hayo lazima tuyamalizie pia haya maboma ya madarasa kwa shule zetu. Pamoja na hayo tujenge nyumba za walimu pamoja na hosteli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja kwenye pensheni kwa wazee. Wazee hawa wamesahaulika kwa muda mrefu sana, wazee hawa ndio ambao wametufanya mpaka leo hii tunasimama mbele yenu hapa tunaongea na nyinyi tunaongea na Bunge lako Tukufu, tunaongea na Watanzania. Niombe sasa kwamba wazee hawa kwenye ile asilimia 10 inayotoka halmashauri na wazee nao wawepo pale inaweza kuwa asilimia tatu kwa vijana, asilimia tatu kwa akinamama, asilimia mbili kwa walemavu, na asilimia mbili kwa wazee, hiyo inawezekana

Mheshimiwa Naibu Spika, moja kwa moja niende kwenye suala la faini za magari zinazotozwa na traffic. Nikuombe Mheshimiwa Mpango; faini hizi ukizilinganisha kati ya basi au pamoja na pikipiki ni vitu viwili tofauti sana.

Nikuombe sasa Mheshimiwa Mpango kwamba hizi faini 30,000 zinazotozwa kwenye bodaboda zipungue, angalau zifikie 10,000 kwa sababu hawa ndugu zangu kipato chao wanachokipata ni kidogo sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende tena kwenye suala la kitengo cha manunuzi. Hiki nilikielezea kipindi cha nyuma lakini ikawa nimeishia katikati. kitengo hiki kwa kweli kinakwamisha sana maendeleo. Ninaomba, ikiwezekana kitengo hiki kama si kufutwa basi kirekebishwe; kwa sababu mradi ambao unahitaji milioni 500 ukipeleka kwenye kitengo cha manunuzi utaambiwa labda bilioni 1.5.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitengo hiki kwa kweli mimi ni imani yangu kabisa kwamba kinazalisha rushwa moja kwa moja. Kwa mfano unaweza ukanunua hata koki au gate valve ya shilingi 50,000, lakini wao wakileta quotation yao wanakwambia hii inauzwa shilingi 500,000 sasa kweli utafika, kwa hiyo niombe tuangalie ikiwezekana tutumie force account katika suala hili; na hiki kitengo ikiwezekana kifutwe kabisa maana naamini kabisa kinakwamisha juhudi za Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niende moja kwa moja kwenye suala la viwanja vya ndege. Ni imani yangu kubwa sana kwamba Serikali hii imejitahidi kwenye ukarabati wa viwanja vya ndege. Niombe kwamba kile kiwanja cha ndege; kwa kuwa Tanga sasahivi imefunguka kibiashara basi ongeza fedha. Naamini umetenga fedha lakini fedha zile hazitoshi; ongeza fedha sasa ziende zikatengeneze uwanja ule kwani uwanja ule sasa hivi ndege haziwezi kutua usiku kwa sababu hauna taa. Kwa hiyo ni imani yangu kubwa; nikuombe uhakikishe kwamba unapeleka fedha za kutosha ili kwenda kujenga uwanja ule.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye suala la watumishi. Watumishi wetu wana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Muda wako umekwisha Mheshimiwa ahsante sana, Mheshimiwa Lucy Magereli atachangia kwa dakika saba, tutamalizia na Mheshimiwa Mashimba Mashauri Ndaki

MHE. SHAABAN O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.