Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Naibu Spika, shukrani kwa kunipa nafasi. Nianze na hali ya uchumi hotuba ya Mheshimiwa Waziri inaonyesha kwamba pato letu la Taifa linapanda lakini uhalisia wa mambo hali mtaani ni ngumu, vyuma vimekaza mambo hayaendi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, viashiria vinaonyesha kwamba hali ni ngumu kwa sababu kwanza kwa sasa hata bidhaa tunazosafirisha kwenda nje zimepungua, mazao kama korosho, kahawa kiasi tunachosafirisha kwenda nje kimepungua. Kutokana na hiyo pia kuna hoja ya mikopo katika sekta binafsi imeshuka. Sambamba na hilo mfumuko wa bei umepungua upo chini ya asilimia tano. Sasa wachumi wanatuelekeza kwamba kama hali ndiyo hiyo ya mfumko wa bei, unaweza ukaathiri kwanza ukasabaisha kutovutia wawekezaji, pili mikopo kutolipika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama hivyo ndivyo ilivyo, mimi siyo mchumi lakini nilikuwa na wazo katika suala moja. Kama mfumko wa bei umeshuka, Wabunge wengi waliposimama wakati wa Bajeti ya Maji walipendekeza Serikali iongeze tozo ya shilingi hamsini katika lita ya mfuta ili basi kupata fedha nyingi pesa nyingi za kutosha kwa ajili ya kuondokana na tatizo la maji. Sasa Mheshimwa Waziri wa Fedha kama mfumuko wa bei umeshuka kwa nini usikubaliane na pendekezo hilo la Waheshimiwa wa Bunge ili basi tukaondokana na tatizo la maji.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika jambo ambalo Serikali ya CCM bado haijashughulikia vizuri ni tatizo la maji, kuna tatizo kubwa sana la maji. Kama tumefanikiwa kwenye umeme kupitia REA kwa utaratibu wa kuweka tozo katika mafuta why not tusifanya katika maji kuna tatizo kubwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamshauri Mheshimiwa Waziri wa Fedha aliangalie suala hili kuna tatizo kubwa miradi ya maji haiendi kwa sababu pesa hakuna. Kwangu kule Kilwa tumefanya contract na watu wa DDCA sasa tuna mwaka wa nne kila siku tunagomba hapa visima havichimbwi kwa sababu DDCA hawana pesa, sasa kama tutakuwa tuna pesa ambazo tumezi- ring fence, nafikiri tunaweza tukafanikiwa kutatua tatizo la maji kama ambavyo tumefanikiwa kwenye umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jingine ni suala zima la mikopo ambayo Benki Kuu imepunza riba kwa benki lakini benki bado hazipunguza riba kwa wateja. Mheshimiwa Waziri wa Fedha ukapokuja hebu tuambie kama Benki Kuu imepunguza riba tena imepunguza sana, kwa nini wateja nao wasipunguziwe riba? Kwa sababu sasa uwezo wa watu kukopa, watu wengi wanaogopa kukopa lakini pia watu wengi wanashindwa kulipa mikopo ambayo wamekwisha kopa. Nalo hilo naomba ulingalie ili basi Watanzania waweze kunufaika.

Mheshimiwa Naibu Spika, jingine niende kwenye suala zima la mifugo na uvuvi. Mheshimiwa Waziri wa Fedha katoa mapendekezo ya kuondoa karibu tozo 15 kwenye sekta ya uvuvi na sekta hii inasimamiwa na Wizara ya Uvuvi na Mifungo, lakini hajaondoa tozo hata moja kwenye sekta ya uvuvi. Mifugo tozo 15 zimeondoka, kwenye uvuvi hata moja hujaondoa tozo. Napata shida kwamba pengine Mheshimiwa Mpina yale mapendekezo yetu ya shida wanazopata wavuvi haukupelekewa labla, nataka niamini hivyo.

T A A R I F A

NAIBU SPIKA: Nani aliyesema taarifa?

MHE. JULIUS K. LAIZER: Mheshimiwa Naibu Spika, nipo hapa.

NAIBU SPIKA: Aaaah! Mheshimiwa Julius Kalanga.

MHE. JULIUS K. LAIZER: Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka kumpa tu taarifa mzungumzaji kwamba siyo busara sana kuendelea kutoa reference ya mapunguzo ya tozo katika mifugo kwa sababu kulikuwa kuna umuhimu wake wa kupunguza. Kama kuna hoja ya kudai punguzo kwenye samaki tudai bila kuona kwamba kupunguza kwenye mifugo maana yake imeathiri haki ya wavuvi, nimeona mijadala hii ikiendelea hivi kanakwamba wafugaji wao hawastahili kupunguziwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo nafikiri tujenge hoja kulingana na mazingira tuliyonayo kuliko ku-justify kwamba tusipunguze kwenye mifugo tupunguze kwenye samaki.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kalanga sidhani hiyo ndiyo hoja ya kwamba mifugo iliyopunguziwa tozo 15 zipungue ili zipelekwe kwenye uvuvi, ni kwamba mifugo tozo zimepungua 15, kwenye uvuvi hakuna nadhani ndiyo hoja ambayo Mheshimiwa Mbunge anajaribu kuiweka hapo.(Makofi)

MHE. VEDASTO E.NGOMBALE: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru kwa ufafanuzi.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Vedasto. (Makofi)

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Naibu Spika, sikusudii kutaka kubagua hizi sekta hapana, hizi sekta zote zinasimamiwa na Waziri mmoja. Waziri na Waheshimiwa Wabunge mnaweza mkawa mashahidi kwa kadhia ambayo imewapata wavuvi kwenye suala zima la kuchomewa nyavu zao, kwenye suala zima la tofauti ya tozo kati ya dagaa wanaovunwa baharini na dagaa wanavunwa ziwani. Kwa mfano, baharini tozo ya kilo moja ya dagaa ni Dola ya Kimarekani 1.5. Ukienda Ziwa Tanganyika tozo ni Dola za Kimarekani ni 1.5, ukienda Ziwa Victoria Dola za Kimarekani 0.16. sasa ni matarajio yetu sasa hii tofauti Mheshimiwa Waziri wa Fedha wewe ndiyo Baba ungekuja kurekebisha kwa sababu kama nchi moja halafu kunakuwa na tofauti ya tozo inatusumbua sana. Sasa tukiona kwamba sekta hii imeshughulikiwa na nyingine haijashugulikiwa ndiyo maana tunataka Mheshimiwa Waziri wa Fedha utusaidie katika hilo.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo ningependa nilizungumzie ni suala zima la korosho, ni dhahili shahili kutokana na maamuzi yaliyofanyika kwenye korosho uchumi umetetereka na hasa wa Mikoa ile ambayo inazalisha korosho. Kwanza mpaka sasa kuna baadhi ya wakulima wengi hawajalipwa na hasa wale wakulima wa chini, hata katika zile pesa ambazo zimelipwa sasa kuna tofauti ya malipo kati ya Wilaya moja na nyingine, kuna Wilaya ambazo zimelipwa mpaka asilimia 90 lakini kuna Wilaya nyingine hata asilimia 50 haijafika.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pendekezo langu na ushauri, korosho zile zipo maghalani na zinazidi kuoza, wapo wafanyabiashara ambao wanataka kununua ninaishauri Serikali na hasa Waziri wa Wiwanda na Biashara Mheshimiwa Rais amekuchangua ili uweze kufanya maamuzi, fanya maamuzi ya kuuza korosho zile hata kwa bei ya chini kwa sababu kadri zinavyozidi kukaa korosho, zinaaharibika ziuzwe sasa angalau tupate nusu hasara.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukweli ni kwamba zile korosho huwezi kuziuza katika bei ile kwa sababu sasa zimeshaanza kuharibia. Sasa nishauri Serikali uzeni angalau tupate chochote kitu ili mambo yaweze kwenda sawa pia wale ambao hawajilipwa walipwe kwa sababu msimu mwingine una karibia.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala zima la bandari. Katika ukurasa namba 28 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha katika kipengele cha tatu anasema ana kusudio la kuwekeza kwenye maeneo ambayo Serikali inaweza kupata mapato zaidi hususan katika uvuvi wa Bahari Kuu kwa kujenga bandari ya uvuvi na ununuzi wa meli za uvuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa Serikali ni kama ina kigugumizi kwamba ni bandari gani sasa iwe bandari ya uvuvi. Katika nchi hii kuna bandari nne, kuna Bandari ya Tanga, Bandari ya Dar es Salaam, Bandari ya Kilwa na kuna Bandari ya Mtwara. Bandari hizi tatu tayari Serikali imeshafanya mkakati wa kuziendeleza, lakini Bandari ya Kilwa hakuna chochote ambacho kimefanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapendekeza Serikali sasa iifikirie bandari ya Kilwa kuwa kama bandari ya uvuvi. Bandari ya Kilwa ina historia kubwa, ukisoma historia ya toka enzi ya Ibn Battuta wanaitaja Bandari ya Kilwa, Mvumbuzi Ibn Battuta alipotembea alipofika katika Bandari ya Kilwa alikutana na Mji mkubwa unaovutia. Sasa kama tuna bandari ya kale toka enzi ya Dola ya Kilwa, lakini mpaka sasa Serikali haijakumbuka kuindelezea. Nafikiri sasa Serikali ione umuhimu wa kuingalia Bandari ya Kilwa na iipe kipaumbele ndiyo iwe bandari ya uvuvi hiyo itakuwa hata mizimu itatuona maana hiyo ndiyo bandari ya kale, kwa kufanya hivi tunaweza kupata mapato ya kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana.(Makofi)