Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema, aliyetujaalia uzima. Pia nitumie nafasi hii kwa dhati kabisa kuipongeza Serikali, kumpongeza Mheshimiwa Rais na Serikali yake kwa kazi kubwa wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni mara yangu ya kwanza kuchangia bajeti ya Serikali. Tangu nimekuwa Mbunge hii ni mara yangu ya kwanza kuchangia bajeti. Nafarijika sana kuona kwamba nakwenda kuchangia bajeti ambayo ukiisoma unaiona bajeti inayogusa maisha ya watu wa Tanzania. Yanaweza yakasemwa maneno mengi, kunaweza kuwa na hadithi nyingi, lakini ukweli ni kwamba bajeti iliyowasilishwa inakwenda kugusa maisha ya wananchi wetu kwenye maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza sana Serikali. Hii miradi mikubwa tunayofanya, inawezekana matokeo yake yasionekane kwa haraka leo, lakini ni miradi ambayo inakwenda kutuvusha kama Taifa kutoka hapa tulipo tuweze kwenda kwenye hatua nyingine. Unapoona mtu analalamika anasema hali ya uchumi ya watu wetu siyo nzuri, mtu analalamika anasema tume-import sana kuliko ku-export, lakini wakati huo huo miundombinu ya kusaidia tuwe na viwanda vya kutosha kwenye nchi yetu watu wanaipiga vita. Ni vitu vya ajabu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unapotaka kuwa na umeme wa uhakika ni kwa ajili ya kusaidia viwanda, unapotaka kuwa na miundombinu ya barabara ya uhakika, kuwa na bandari ya uhakika ni kwa ajili ya kusaidia viwanda, ukipata viwanda vingi ukazalisha vizuri, tutafika huko tunakotaka kufika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, nimeona tangu mjadala huu umeanza tumekuwa tukipigana kelele, mtu anasema, Serikali hii hakuna kitu ilichokifanya. Pia tumefika mahali tunahukumiana kwa kutumia Ilani za Vyama tulizotumia kwenye uchaguzi wetu wa mwaka 2015. Sisi wote tunajua, Vyama vinapokwenda kwenye uchaguzi, Ilani tunazozinadi tunazinadi kwa ajili ya kuwatumikia Watanzania kwa miaka mitano, ndiyo muda tuliojiwekea kwa uongozi kama Taifa kwa mujibu wa Katiba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, muda wa kutekeleza Ilani ni miaka mitano. Miaka mitano haijaisha, pressure hizi zinatoka wapi?mtu anaongea kana kwamba leo ndiyo tunamaliza, Serikali inakwisha, muda wa uongozi umekwisha, tunakwenda kwenye uchaguzi. Hii siyo sawa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wamezungumza kuhusu shilingi milioni 50, mtu anapiga kelele anasema mliwaahidi Watanzania shilingi milioni 50, ziko wapi? Kwanza nikubaliane kabisa na dada yangu Mheshimiwa Gekul. Tunapoahidi vitu, Serikali iliyopo madarakani iliahidi vitu vingi, kila kitu kinafanyika kulingana na nafasi na wakati ambao tunao. Hizo shilingi milioni 50 za kwenye vijiji, yako mambo yamefanyika makubwa kwenye maeneo ya watu wetu na yanayogusa maisha ya Watanzania, tofauti hata na hiyo shilingi milioni 50 ingekwenda moja kwa moja kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Serikali, tumefanya vizuri kwenye maboma ya shule za sekondari na za msingi, tupeleke na huo moyo kwenye zahanati kwenye vijiji ambavyo watu wetu wapo. Wananchi wetu wanajitoa sana kwenye ujenzi wa zahanati, tumefanya vizuri kwenye maboma shule za sekondari na za msingi, hebu twende tukasaidie na kwenye zahanati. Huyo anayesema kwamba bajeti haigusi maisha ya watu, akaangalie maji, zahanati na barabara, atasema kama bajeti inagusa maisha ya watu au haigusi maisha ya watu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nishauri mambo machache kwa ajili ya kusaidia kuongeza mapato kwenye nchi yetu. Mheshimiwa Waziri wa Fedha unafahamu, inawezekana kabisa wakati mwingine kuongeza kodi kukakupunguzia idadi ya watu wanaoweza kuwa walipa kodi. Inawezekana kabisa kuongeza kodi kukakupunguzia idadi ya watumiaji wa huduma ambayo ingesaidia kupata kodi. Sasa naomba sana Mheshimiwa Waziri hili jambo tuliangalie vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, mimi nilikuwa naangalia tu barabarani mle, miaka michache iliyopita watu waliokuwa wanatumia magari ambayo yamesajiliwa kwa majina yao, ninavyoona kama idadi ile inapungua. Ukiangalia vizuri, inawezekana imesababishwa na kuongezeka kwa kodi ile, lakini kodi ile ingekuwa angalau kwenye kiwango kizuri, ni rahisi kupata watu wengi zaidi na kupata kodi nyingi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili lipo pia kwenye Sports betting. Tunachukua kodi kule, wale waendeshaji wanalipa asilimia 25 ya mapato ghafi wanayopata, lakini na yule mtu ambaye anashinda kwenye ile zawadi anayopata analipa asilimia 20. Wako watu ambao kwa kuona kwamba wanalipa kodi, wengine wameamua kuacha hizo, wameamua kufanya za online, inasababisha kwenda kukosa kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshauri Mheshimiwa Waziri, tuangalie namna ya kupunguza kodi hasa kwa wale ambao wanashinda ili ku-encourage watu wengi zaidi waweze kushiriki ili kutengeneza kodi zaidi kwa wale wanaoendesha lakini pia wanalipa kodi kwenye huduma nyingine kama wakifanya matangazo wanatoa ajira kwa watu wetu na vitu vingine vya namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye upande wa utalii. Juzi hapa tumefanya mnada wa vitalu. Katika vitalu 26 naambiwa tumefanikiwa kuuza vitatu saba. Hii imechangiwa sana na ongezeko la gharama za kununua vile vitalu. Naiomba Serikali, vitalu hivi vikikaa kwa muda mrefu bila kuwa na watu waliovichukua tunapata hasara sisi kama Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni Mjumbe wa Kamati yako ya Bunge, Ardhi Maliasili na Utalii. Tuliishauri sana Serikali, tunaweza tukaweka makadirio yetu lakini tusiyatangaze, lakini pia tusiwe rigid kwenye hayo makadirio ambayo tumeyaweka, lakini pia tusiongeze sana ili kuweza kusaidia watu wengi waweze kujitokeza na kuja kuomba kununua vitalu ili tufanye biashara na Serikali iweze kupata fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine kwenye upande wa utalii ni kwenye hoteli. Miaka ya nyuma Serikali yetu iliamua kubinafsisha baadhi ya hoteli. Ziko baadhi ya hoteli nyingine ambazo ziko chini ya Serikali pia ziliuzwa. Watu waliobinafsishiwa hoteli hizi, ukienda vizuri, hoteli nyingi zilizobinafsishwa hazifanyi kazi vizuri na kwa kutokufanya kazi vizuri hazitengenezi vizuri ajira, hazitengenezi vizuri mapato kwa maana ya kulipa kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunahangaika sana kukuza utalii na utalii ni eneo ambalo tunaweza kutusaidia kama Taifa kupata fedha nyingi, lakini tunakuza utalii, lakini ili tuwaalike watalii wengi zaidi waweze kuja kwenye nchi yetu, wakati huo huo miundombinu tuliyokuwa nayo haiendani na hii kasi ya uingizaji wa watalii kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye nchi yetu ukilinganisha vitanda ambavyo tunavyo vinavyoweza kulipiwa kodi, ukilinganisha na nchi jirani za wenzetu, sisi bado tuko nyuma sana. Tungeweza kutatua tatizo hili kwa kwenda kuziboresha hoteli ambazo ziko ndani ya nchi yetu. Cha kusikitisha zaidi, ziko hoteli ambazo tulizibinafsisha, watu wakachukua zile hoteli, wakachukua mikopo, wakafungua biashara nyingine za namna ile kama hoteli na wakafanya kazi na wanafanya kazi vizuri. Zao zinakwenda vizuri, walizobinafsishiwa na Serikali haziendi vizuri. Naishauri sana Serikali, tuna jambo la kuangalia hapa. Tuangalie namna ya kuboresha hizi huduma za hoteli ili tuweze kuwasaidia watu wetu, tuweze kusaidia nchi yetu kuweza kupata mapato zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunakubaliana kwamba kilimo ni miongoni mwa maeneo muhimu katika kutafuta malighali kwa ajili ya viwanda vyetu. Naiomba sana Serikali, tuendelee kuweka mkazo kwenye kilimo, hasa kilimo cha umwagiliaji ili kuhakikisha kwamba watu wetu wanazalisha zaidi na wapate soko la kuweza kulisha viwanda vyetu na waweze kupata fedha, lakini pia viwanda viweze kwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kule Korogwe tunalo bonde ambalo likitengenezwa mradi wa umwagiliaji, tunaweza kulima hekta 5,000. Kwa karne tuliyonayo hekta 5,000 ni eneo kubwa sana. Ukiwa na wananchi 5,000 wamejiingiza kwenye kilimo cha uhakika wanaweza kulima kwa zaidi ya mara mbili kwa mwaka mmoja. Ni kuwa na misimu ya kilimo zaidi ya miwili kwa mwaka mmoja. Ni jambo kubwa sana. Tunatengeneza uchumi mzuri kwa ajili ya maisha ya watu wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilisema nichangie hayo machache kuishauri Serikali namna ya kuongeza mpato, kubwa nasema bajeti hii ni nzuri, bajeti hii inafaa, bajeti hii inagusa maisha ya wananchi wetu moja kwa moja, watu wamepiga kelele tulikuwa tunaomba sana tozo zipunguzwe tusiwe na mtiririko wa kodi na ndiyo spirit ya Mheshimiwa Rais, bajeti hii iliyowasilishwa inajibu hoja hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono bajeti hii. Ahsante sana. (Makofi)