Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Sixtus Raphael Mapunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. SIXTUS R. MAPUNDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa na mimi nafasi ya kuchangia kwenye bajeti hii. Nchi yetu bado ni Taifa changa linalo-struggle sana kwa wananchi wake kuwa na uhakika wa kupata chakula, kuwa na uhakika wa kupata sehemu ya kulala na vilevile wanahangaikia sehemu ya kujihifadhi katika maana ya nguo na mambo mengine elimu na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hali ya namna hiyo, ni ngumu sana mtu unapoyahitaji yote kwa wakati mmoja kwa aina ya uchumi wetu ukayapata yote kwa wakati mmoja na kutokana na hali hiyo hiyo mahitaji yote unayataka kwa wakati mmoja, vilevile ni ngumu kukiacha kimoja ndiyo maana naungana sana na Serikali yetu ya Awamu ya Tano kwa jitihada zake za kwenda na miradi mikubwa wakati huo huo ikirekebisha mambo madogo. Haya mambo yote ndani ya nchi yetu siyo mapya yana mifano, wote mtakumbuka tuliposema tuwe na shule za sekondari kwa kila kata na wengine hapa mtakuwa mashahidi watu humu ndani waliwahi kusema ni vema tukaanza kutengeneza walimu, halafu baadaye tukajenga shule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kutokana na hali jinsi ilivyo hatuwezi tukasubiri watu kuzaliana watoto wakakua wasubiri kwanza mwalimu atakayepatikana kwa muda wa miaka saba, badala ya kujenga boma moja utakalolimaliza baada ya miezi mitatu. The same here, leo tunaongelea kuhusu viwanda mwingine anasema hapana tusijenge kiwanda twende kwanza tuka-produce, tukishazalisha kiwango cha hali ya juu sasa twende kwenye viwanda hili linakuwa ni kosa la pili linafanana vilevile leo unataka kujenga shule kipindi huna mwalimu, ukizalisha sana kabla hujaenda kwenye viwanda crisis yake itakuwa ni kubwa zaidi ni vema ukaanza kiwanda ukakikuza kiwanda kulingana na mahitaji yake kuliko ukaenda kwenye kuzalisha sana bila kiwanda yale malighafi utapeleka wapi? Ndiyo kwa maana nikasema nchi yetu ni nchi changa, inahitaji yote kwa wakati mmoja na yote lazima yaende hatuna njia ya mkato, kila utakalolichagua halitakuwa sahihi zaidi kuliko lingine. Ukisema leo uwekeze kwenye kilimo huwezi ukaacha afya, ukisema leo uwekeze kwenye afya hutaacha elimu. Kwa nchi yetu jinsi ilivyo hakuna namna, kweli kupanga ni kuchagua we don’t have choice, we must choose all of them. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili naomba niseme kidogo kwa mambo ambayo yameongelewa kwa muda wa miaka hii mitatu/minne kwa mfululizo miradi mikubwa sana mradi wa reli ya Mtwara, Liganga na Mchuchuma katika upande wa chuma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunapoenda kwenye maendeleo makubwa ya viwanda na Mheshimiwa Waziri wa Fedha nitakuomba sana ulitizame hili kama nilivyosema awali kupanga ni kuchagua mjadala wa Liganga na Mchuchuma umekuwa mrefu mno, tunaanza sasa hivi reli ya kati ya kisasa Liganga na Mchuchuma imejadiliwa miaka na miaka kwa nini tusimalize hilo? Lakini jambo la pili, siyo kila kitu lazima tukifanye wenyewe. Reli ya Mtwara itakwenda kuunganisha Liganga na Mchuchuma, itapita mpaka kwangu pale Mbinga, itakwenda mpaka Mbamba bay kwa nini tusianze kwa PPP kwa theory ile ile bila kuogopa miradi mikubwa kwenda nayo pamoja, kupanga ni kuchagua lakini hatuna choice lazima tuyachague yote kwa wakati mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine hili naomba niliseme kwa utulivu kidogo; Mungu alipotuumba wanadamu, kwanza zile siku zake tano za mwanzo akasema na liwe jua na uwe mwanga, ardhi na mimea vyote vikawepo. Ilipofika siku ya sita akasema na tufanye mtu kwa sura na mfano wetu. Baada tu ya kumuumba na kumwambia zaeni mkaongezeke akamwambia ukavitawale viumbe vyote vya ardhini na ndege wote wa angani; maana yake nini kila kitu kilicho juu ya sura ya ardhi ya Tanzania lazima kitawaliwe bila masharti yoyote kwa sababu tu kinatija kwa mwanadamu.

Mheshimiwa Spika, leo hii mnaongelea mambo ya umeme, reli ya kati mnasema mto Rufiji, Stiegler’s Gorge, nakupa hoja nyingi za kubeza mimi niseme kitu kimoja, moja ya biblia imesema tutawale, tuweke umeme kwa njia zozote zile lakini kwa hoja ya pili ni hoja ya kisayansi watu wamesema sijui maji, yataisha, sijui nini kitatokea, kuna kitu kimoja kwenye sayansi na wanasayansi wa anatomy watanisaidia. Ukisoma introduction to anatomy inakuambia sensitivity, irratibity na adaptation; kila kiumbe duniani ameumbwa kwa ajili ya kukabiliana na mazingira. Ukiona jambo linakusaidia leo kwa ajili ya kupiga hatua moja hata kama ina negative effect akili yako mwanadamu umeumbwa kukabiliana na mapungufu yanayotokana na maamuzi yako.

Mheshimiwa Spika, tukienda leo pale kuweka ule mradi kuna watu wanasema kuna baadhi sijui ya swala hawanywi maji wanakula ule mvuke unaotokana na maporomoko tutapoteza utalii, si kweli; kama binadamu anayekuwa kwenye baridi akitoka kule Mbeya anakuwa na vinyoleo akifika Dar es Salaam miezi miwili vinyoleo vinapuputika kwa ajili ya joto. Huyu swala atashindwa ku- adapt nature?

Jamani tusiogope kutoa maamuzi kwa ajili ya nature, Mwenyezi Mungu katuumba na hizi rasilimali tuzitumie, tukiziacha zitakuja kuwa laana kwetu, hatuwezi leo kwenda kulipa gharama kubwa sana ya umeme kwenye majenereta miaka nenda miaka rudi umeme wa maji uko pale hata kama utakuja kuchukua kinu cha kwanza kitatoa umeme mwaka 2029 is better ku-make decision leo. Ukiacha kutoa maamuzi leo, kesho aje atoe nani? Waliotengeneza reli ya kati walikuwa wanajua tutahitaji namna hii wali-make decision, we must make decision hata kama hata maamuzi yanatuumiza sana lazima tuyafanye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini moja la mwisho niseme kuhusu Watanzania. Watanzania inabidi si neno zuri sana kulisema lakini inabidi niliseme inabidi kidogo tuangalie akili zetu zikoje, kuna muda hatujui tunachokitaka, ukiambiwa reli isipokuwepo matatizo, ikiwepo mbona miradi yote mikubwa inaenda kwa wakati mmoja. Ndege isipokuwepo matatizo...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa...

MHE. SIXTUS R. MAPUNDA: Mheshimiwa Spika, ukiileta...

SPIKA: Mheshimiwa Sixtus malizia.

MHE. SIXTUS R. MAPUNDA: Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie kwa maneno mawili ya mwisho; Watanzania tujifunze kujua tunachokotaka lakini la pili ni afadhali tuwe na uwezo na udhubutu wa kutoa maamuzi yenye tija hata kama yatakuwa na hitilafu gari lililoanza safari ni rahisi kulirekebisha kuliko ambalo halijaanza kufanya safari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)