Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie kwenye mapendekezo haya ya bajeti. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri na timu yake nzima kwa kazi nzuri wanayofanya, najua wanapitia kwenye mawimbi wakati mwingine, lakini ndio kazi zenyewe zilivyo, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri hongera sana kwa kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia niipongeze Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti nadhani wamefanya kazi nzuri sana ukipitia report yao wameweka mambo mengi ya msingi ambayo wameyashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, upande wa Serikali nipongeze uamuzi wa kufuta tozo mbalimbali mlizozifuta, ninaamini nyingi zitasaidia kurahisisha ufanyaji wa biashara katika nchi yetu, nadhani hili jambo ni zuri na ni jambo la kutiwa moyo. Sasa tuende mbele zaidi tukaangalie zile tozo ambazo zina positive impact kwa wafanyabiashara na impact yake ni kubwa zaidi, hizi ziko nyingi ziko 54; lakini nyingi ni ndogondogo sana na pengine madhara yake yanaweza yasionekane sana kwa hiyo tuende zaidi ya hapo tulipoenda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niishukuru sana Serikali kwa kukubali pendekezo la kufuta tozo kwenye visima vile, visima vya watu binafsi nadhani uamuzi huu ulikuwa mzuri, ninaishukuru Serikali kwa niaba ya wananchi wangu wa Jimbo la Mtama, lakini na kwa niaba ya watumiaji wa visima kwa sababu nadhani hii ilikuwa ni kero kubwa, Serikali imekubali, imelifuta naomba nichukue nafasi hii kuishukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini sasa Mheshimiwa Waziri nadhani tuende mbali kidogo Kamati ya Bajeti imependekeza msamaha wa kodi kwenye ongezeko la thamani kwenye mitambo ya kuchimba visima vya maji. Kwa hiyo, pamoja na kufuta tozo lakini nadhani sasa fikirieni kwa sababu Mheshimiwa Waziri magonjwa mengi nchini hapa chanzo chake ni maji, lakini mitambo hii ikifutwa kodi, mitambo hii itatumika kuchimba visima, lakini pia itatusaidia kwenye kilimo kwenye kuchimba malambo. Kwa hiyo, ninaunga mkono pendekezo la Kamati ya Kudumu ya Bunge kwamba pamoja na kufuta tozo kwenye visima basi tuende mbali tufute pia VAT kwenye mitambo ya kuchimbia visima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaunga pia mkono pendekezo la Kamati ya Kudumu ya Bunge wamezungumzia kwa kina mgawanyo wa bajeti yetu. Bajeti yetu kwa sehemu kubwa na Kamati imeeleza, imepeleka fedha nyingi kwenye maeneo ya ujenzi na miradi mikubwa tuliyonayo, sio jambo baya kuwekeza kwenye hii miradi. Lakini sekta ambazo zinahusishwa watu wengi katika nchi yetu ni sekta ya kilimo ndio inahusisha watu wengi sana, karibu asilimia 70 ya Watanzania wanajihusisha na kilimo, lakini kinazalisha ajira kwa asilimia 65, asilimia 85 karibia ya bidhaa tunazouza nje zinatokana na kilimo, lakini inachangia Pato la Taifa kwa asilimia 29 na kwa asilimia zaidi ya 100 chakula cha nchi hii kinategemea kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hii ndiyo sekta ambayo ikiguswa inagusa maisha ya watu wengi na tungeweza kupambana na umaskini wa watu wetu kwa kiwango kikubwa. Ukiangalia mtiririko wa bajeti mwaka 2016/2017 kwa bajeti ya maendeleo tulitenga asilimia 1.38 ndio tukapeleka kilimo; asilimia 1.38, sekta ambayo ndio inabeba watu wengi.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2017/2018 tukatenga asilimia 1.25, mwaka 2018/2019 tukatenga asilimia 0.81 na huu ni utengaji sio upelekaji wa fedha, mwaka 2019/2020 tukatenga asilimia 1.17 ya fedha za maendeleo. Sasa hili ndilo eneo kubwa na kupanga ni kuchagua, kama tunataka kushughulika na umaskini wa watu wetu, tunataka kushughulika na watu walio wengi mimi nilidhani vipaumbele vyetu na mgao wetu eneo kubwa la fedha zingeenda huko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kama tumeshindwa kutenga fedha nyingi na upelekaji wa fedha kwenye sekta hiyo ambayo inagusa watu wengi unasuasua, mimi nilidhani ule utaratibu tulioanza nao mwaka 2016/2017 wa kufuta tozo nyingi kwenye eneo la kilimo ili itusaidie tungeendelea nao ingesaidia inge-replace hili ambalo tumeshindwa kulifanya la kutenga fedha nyingi kwenye sekta ya kilimo. Lakini safari hii tume-deal na tozo kwenye biashara, kwenye kilimo tumefumba macho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utakumbuka tulikuwa tunatenga fedha hapa kwa ajili ya pembejeo, kuna wakati tulifikia mpaka bilioni 200 tumeziondoa, pembejeo hakuna hazipatikani, viwanda vya kutengeneza havipo sasa na bado tozo bado ziko nyingi, pendekezo langu ni kwamba tuende tukazipunguze.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili; wigo wa wawalipa kodi kwa muda sasa imekuwa tukizungumza, kuna takwimu sina hakika kama bado ni hizo hizo kwamba inategemewa walipa kodi wako kama bilioni 14 wanaolipa ni milioni 2.5, kwa hiyo mzigo wa wawalipa kodi wengi ambao walitakiwa kulipa unabebwa na asilimia ndogo sana ya Watanzania. Sasa Mheshimiwa Waziri mimi nilidhani tungeanza hata kama ni kidogo kuupanua huu wigo wa wawalipa kodi tungekuwa tumepiga hatua fulani na wigo ungepanuka, nimemsikia mama yangu pale akizungumza hoja ya wafanyakazi, tunajua mshahara kidogo hatujapandisha maisha yao yanaendelea kuwa magumu.

Mheshimiwa Spika, mimi nilidhani tungekuwa tumepanua wigo wa walipa kodi tungeweza kushughulika kupunguza kodi hasa kwa wafanyakazi na hasa wafanyakazi wa chini. Ukichukua takwimu leo wafanyakazi wote nilisikia mama alizisema pale karibu shilingi bilioni 971 zinategemewa kutokea kwenye pay as you an ya wafanyakazi wa Serikali. Lakini wako wale wa chini kabisa walimu ambao ni wengi na ndio wanateseka tunategemea shilingi bilioni 194 tungezikata hata kwa asilimia 50 ambayo unapata shilingi bilioni 97, hizi tukazipeleka kwenye chanzo kingine ambacho tumekibuni huu mzigo ungepungua kutoka kwa wafanyakazi na hasa walimu.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi nadhani tungeianza hii hatua tulipo-introduce vitambulisho vile vya kitaifa lengo moja wapo ilikuwa ni ku-formalize sekta zetu lakini kwa kiasi gani tumeitumia imetusaidia kwa kiasi gani tusipotanua wigo wa wawalipa kodi tutaendelea kuwabebesha watu wachache mzigo mkubwa wa wawalipa kodi na kwa sababu mzigo unakuwa mkubwa wana-tendency ya kujitahidi kukwepa kwa sababu mzigo ni mkubwa sana. Kodi nzuri ni ile ambayo inalipika na inalipika kwa wakati, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nilikuwa napendekeza hebu tuanze basi tutoke hapa tulipo tuongeze wigo wa wawalipa kodi.

Mheshimiwa Spika, kwenye taarifa nilizozisoma hapa inaonesha kwamba sekta ya sanaa na burudani imekua kwa kiwango kikubwa, lakini ukweli sekta hii inakua kwa kudra. Sheria, kanuni na taratibu tulizonazo zinazosimamia sekta hii zimepitwa na wakati sana. Sasa lazima ifikie mahali Serikali twende tujikite tuzibadilishe sheria na taratibu zinazozisimamia sekta hii ambayo tunakubaliana kwamba inakua kwa kiwango kikubwa basi iendane na wakati, kwa sababu sheria tulizonazo zimepitwa na wakati na hazisaidii ukuaji wa hii sekta. Kwa hiyo mapendekezo yangu moja, tuangalie mgawanyo wa fedha tunaupeleka wapi kule ambako wapo watu wengi nadhani ndiko ambako tulipaswa kupeleka fedha nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini la pili ni vizuri tukaangalia namna ya kupanua wigo wa wawalipa kodi tusibaki na namba ile tunacheza nayo unarudisha, unajumlisha, unatoa mzigo unakuwa mkubwa sana. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana malizia.

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, ninaunga mkono hoja ahsante sana. (Makofi)