Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi au hotuba nzuri. Pia nimpongeze Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ni juu ya ujenzi wa Vyuo vya Ufundi. Katika hotuba ukurasa wa 59 umezungumzia juu ya ujenzi wa Chuo cha Ufundi Stadi cha Mkoa wa Geita. Hili nalipongeza na ninashauri ujenzi uanze mara moja kutokana na mahitaji tuliyonayo katika Mkoa wetu. Mkoa una Wilaya tano na hatuna chuo hata kimoja katika Wilaya za pamoja na mpango wa ujenzi wa Chuo cha VETA Mkoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe msisitizo pia kwamba Serikali ione umuhimu wa kujenga vyuo hivi katika Wilaya zetu. Sera ya Taifa ni kuwa na VETA kila Wilaya. Kwenye bajeti nimeona ujenzi wa VETA Wilaya ya Chato, tunapongeza, lakini Serikali ione uwezekanao wa kujenga VETA Wilaya ya Geita kulingana na wingi wa watu katika Wilaya yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wanaomaliza Shule za Msingi na Shule za Sekondari ni wengi ambao hawaendelei na elimu ya juu na hao wanahitaji ujuzi na ufundi stadi ili kuwawezesha kumudu maisha yao kiuchumi na mwisho wa siku wachangie katika pato la Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya pili ni madeni ya Walimu. Hii ni changamoto sana maana Walimu bado wana madai yao makubwa sana. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita na Mkoa wa Geita madai ni makubwa na tayari madeni yamehakikiwa. Ili tuboreshe morale na ufanisi katika utendaji kazi kwa Walimu ni vema Serikali ikatilia mkazo katika kulipa madeni haya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya tatu ni juu ya malalamiko ya wanafunzi wa UDOM kitengo cha Diploma ya Ualimu. Ni wiki ya nne sasa hawafundishwi kutokana na mgomo wa Walimu wao. Malalamiko haya yamewasilishwa na viongozi wa wanafunzi katika Kitengo cha Ualimu UDOM jana, ambapo walikuja hapa Bungeni kutoa shinikizo kwa Waziri juu ya hatma ya suala hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri kwa Mheshimiwa Waziri wakati wa majumuisho hebu utoe kauli kuhusiana na jambo hili. Naomba ulifuatilie na ulitafutie ufumbuzi.