Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze na mimi kuchangia hotuba ya Waziri wetu wa Fedha na Mipango siku hii ya leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwanza kwa kuunga mkono hoja asilimia mia moja kwa mia moja. Nayasema haya kwa sababu hotuba ya bajeti iliyosomwa kwetu hapa ikitanguliwa ikitanguliwa na hotuba ya hali ya uchumi wa nchi yetu imeonyesha dhahiri kwamba ni hotuba ya Serikali ya watu, iliyowekwa kwa watu, ili itimize malengo kwa ajili ya watu. Ninayo imani kwamba Serikali ya Chama cha Mapinduzi itatenda yote ambayo imeahidi kupitia bajeti hii, ninao uhakika kwa sababu bajeti zote ambazo zimepita zimetekelezwa kwa kiwango kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba Serikali yetu imekuwa ni Serikali sikivu inajali watu inatekeleza mipango inayoipanga kwa wakati. Niseme tu kwamba katika kuanza kuchangia kwangu nitajikita zaidi katika suala zima la kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, asilimia kubwa ya Watanzania ni wakulima wameajiriwa katika sekta hii na kwa ajili hiyo Serikali inatakiwa iweke msukumo zaidi katika sekta hii ambayo kimsingi inatakiwa iende sambamba na kaulimbiu ya Serikali yenyewe ya Tanzania ya viwanda. Maana mataifa yote ambayo yameendelea yalianda na mageuzi ya kijani, baadaye ya kaja mageuzi ya viwanda na mambo yote haya yakafanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ajili hiyo niseme kwamba Serikali iwekeze zaidi katika tafiti mbalimbali, ziwekewe pesa kwa ajili ya kuhakikisha kwamba utafiti unafanyika katika udongo. Udongo ukishajulikana tuna imani kwamba yale mapungufu ambayo yanakuwa yanajulikana kwamba haya ndio mapungufu basi hata mbolea ambayo itakuwa inatakiwa kwenye aina fulani ya udongo itajulikana. Tofauti na sasa hivi ambapo mbolea za aina moja zinakuwa zinapelekwa katika aina mbalimbali za udongo. Udongo mwingine upo ambao ni alkaline na mwingine ni acidic, kwa hiyo, matokeo yake unakuta kwamba saa nyingine wakulima wanaweza wakajikuta kwamba saa nyingine uzalishaji katika mashamba yao unakuwa ni hafifu kutokana na kwamba utumiaji wa mbolea unakuwa hauendani sambamba na mahitaji kwa wakati huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali yetu imejikitika kuhakikisha kwamba maeneo ya vipaumbele hasa katika miundombinu iwe ya barabara, ya reli, miundombinu ya umeme, maji na mambo yote haya ndio hasa kiini cha maendeleo ya Watanzania wenyewe. Ninashangaa pale watu wanaposema Serikali yetu inajali zaidi maendeleo ya vitu badala ya watu nashangaa kidogo, kwa sababu haiwezekani ukawa na maendeleo ya watu ukayatenga na maendeleo ya vitu. Kwa mfano, ujenzi wa hospitali, ujenzi wa barabara kwa sababu hospitali inaenda na afya ya mwananchi. Kwa hiyo, mwananchi ambaye atakuwa na afya goigoi hawezi kujenga uchumi, hawezi kushiriki katika uzalishaji mali na kwa maana hiyo mimi nina imani kabisa kwamba Serikali yetu iko kwenye njia sahihi na nikuombe Mheshimiwa Mpango na Naibu wako pamoja na wasaidizi wako muendelee kupiga kwenye bull kama ambavyo mmeendelea kufanya, watu wote hawa ambao tuko hapa tunajaribu kuzungumza, wakati mwingine tunajaribu kupiga makelele ya kujaribu kuwatoa kwenye target, ila naomba tu kwa kweli muendelee kushikilia kama hivi ambavyo mmepanga na mtekeleze kwa umakini mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali yetu imekuja na utaratibu wa ujenzi wa bwawa kubwa la uzalishaji umeme la Stiegler’s Gorge na ni juzi tu nimemuona Mheshimiwa Waziri mwenyewe amekwenda kuhakikisha kwamba ujenzi unaanza na mkandarasi amekabidhiwa site. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba utekelezaji wake ufanyike na kama ambavyo wameahidi wanasema kwamba baada ya miaka hiyo mitatu hizo megawatts 2,115 zitazalishwa, basi na yote yakafanyike ili sasa wale matomaso, wale wanaotaka mpaka waone, basi waje waone haya maajabu ya Serikali ya awamu ya tano yanafanyika wakati wao wenyewe wakiwa hai. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninayo imani na Serikali ya Chama cha Mapinduzi, kwa sababu ni Serikali sikivu na siku zote imekuwa ikisema na kutenda. Imesema inaanza ujenzi wa Standard Gauge Railway, ujenzi huo umeanzaDar es Salaam - Morogoro, wale ambao hawajawahi kutembelea wakaone, wataona ujenzi unaendelea. Morogoro – Dodoma ujenzi unaendelea na niombe tu kwamba hata ule mpango wa kujenga ile reli ya kutoka Isaka kuelekea Rusumo, ni- declare interest kwamba hiyo reli itapita pia katika Jimbo langu la Mbogwe.

Kwa hiyo, mimi ninaomba kwamba kwa kweli Serikali ya Tanzania na Serikali ya Rwanda mfanye hima kuhakikisha kwamba mnaijenga hiyo reli kwa sababu uwepo wa barabara ambayo sasa hivi inatoka Isaka kwenda Kigali, Rwanda, tumeona matokeo yake. Wakati ambapo barabara ya lami ilikuwa bado haijajengwa, maendeleo katika kanda yetu kwa kweli hayakuwa mazuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mpaka sasa baada ya kuwa ukamilifu wa barabara ya lami kutoka Isaka kwenda Kigali, Rwanda ilipokamilika na Kampuni ya Codify ikiwa imeshiriki katika ujenzi huo, tumeyaona maendeleo ya kasi ambayo yamejitokeza katika Miji ya Isaka, Kahama, Masumbwe, Ushirombo, Ruzewe, kote ambako barabara hii imepita, tumeyaona nageuzi na wengine hata wale ambao wanajua kwamba ambapo barabara ya lami kutoka Dar es Salaam kuja kukomea Dodoma hapa, kutoka hapa Dodoma kuelekea Mikoa ya Singida, Tabora, Shinyanga mpaka Mwanza, tulikuwa tunasafiri kwa siku zaidi ya tatu. Sasa lakini kwa wakati huu, hali kama inakuwa ni nzuri tu, unafika siku moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na unapotumia muda mfupi katika masuala mbalimbali, unahakikisha kwamba unashiriki katika ujenzi wa uchumi. Maana wanasema wazungu time is money. Kwa hiyo, unapokuwa unaweza ku-manage muda, ni hakika kabisa kwamba utakuwa mzuri sana katika ujenzi wa uchumi na kwa maana hiyo sisi tunapotengeneza miundombinu ya barabara...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Naibu Spika, ooh basi nakushukuru niombe kuunga mkono tena kwa mara nyingine, ahsante sana kwa kunisikiliza. (Makofi)