Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Shamsi Vuai Nahodha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. SHAMSI VUAI NAHODHA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme mambo manne la kwanza, nimewasikia baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wanasema bajeti ya mwaka huu imeweka mkazo mkubwa zaidi kwenye maendeleo ya vitu badala ya maendeleo ya watu. Mimi naomba nitofautiane na hoja hii na nitatoa sababu zifuatazo; kwanza historia inatuonesha kwamba nchi zote zilizofanikiwa kiuchumi zimewekeza kwenye miundombinu ya msingi hasa umeme na reli. Uingereza wamefanya hivyo, Marekani wamefanya hivyo na sasa Bara la Asia linafanya hivyo. Kwa hiyo Tanzania haijafanya kitu tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge waliokuwepo Bunge lililopita watakumbuka tulilalamika sana hapa kwamba Tanzania inashindwa kuitumia Bandari ya Dar es Salaam na kuifungamanisha na reli na ikaweza kuitumia soko kubwa la nchi zinazotuzunguka na tukafika mbali tukasema yuko kiongozi mmoja simtaji wa nchi moja ya Afrika Mashariki alinukuliwa akisema akipewa Bandari ya Dar es Salaam ataiendesha Bara zima la Afrika. Sasa maneno huumba, tulisema tunamhitaji kiongozi mwenye ujasiri, atakayefanya maamuzi magumu. Tumepata kiongozi tuliyemuomba, anafanya tuliyoyataka, halafu sasa tunafikiri tofauti. Inanikumbusha ule usemi wa watu wa Rufiji; zilongwa mbali zitengwa mbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tunatarajia na tunategemea Serikali iitumie Bandari ya Dar es Salaam kusafirisha mizigo mizito kuipeleka nchi zinazotuzunguka. Sasa tumeshafanya uamuzi huo kujenga reli tunawezaje kusafirisha mizigo mizito bila kutumia reli. Dunia nzima wataalam wanasema wazi kwamba usafiri ulio rahisi zaidi duniani kusafirisha mizigo mizito hakuna usafiri wowote kuliko reli. Sasa wanaodhani uamuzi wa kuwekeza kwenye reli na uamuzi wa kuwekeza kwenye umeme wa kutosha kutoka Bonde Rufiji si uamuzi wa busara mimi nawaomba tu wafikirie zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili mapinduzi ya kilimo duniani na Mapinduzi ya viwanda Ulaya, Marekani na katika siku za karibuni Asia yamewezekana kwa sababu ya uwekezaji mkubwa sana katika sekta ya umeme na reli. Iko hoja na hapa imesemwa kwamba wako ambao wanaona kwamba kwa nini hatuwekezi kwanza kwenye elimu, afya na maji. Mimi ninachosema kupanga ni kuchagua na hii hoja tunayoileta hapa ni sawa na wale wanaouliza ni lipi linaanza mwanzo kati ya kuku na yai, unaweza kusema ameanza kuku au ameanza yai, sasa ni lazima upate mwanzo sasa elimu ni muhimu, afya ni muhimu lakini nasema lazima tuwe na jambo la kuanza na kwa bahati mbaya hatuna uchumi uliokuwa mkubwa wa kutosheleza kufanya kila jambo kwa wakati mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa lazima tuamue sasa Serikali ya Awamu ya Tano imeamua kuanza na umeme, reli na kilimo nitaeleza baadae. Nadhani hapa hoja ya msingi ingekuwa kwa nini Serikali haiwekezi kiasi cha kutosha katika sekta ambayo ina uwezo wa kuwatoa watu wengi kwa wakati mmoja katika umaskini, na sekta hiyo basi ingekuwa ni kilimo. Wataalam wanasema wataalam wa uchumi sekta ambayo ina uwezo wa kuwatoa watu zaidi ya asilimia 50 katika umaskini ni sekta ya kilimo, kwa munasaba huo naishauri Serikali ifanye kila linalowezekana iwekeze kwenye sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mtakumbuka nchi yetu hivi karibuni tumesaini mkataba wa eneo huru la uchumi katika Bara la Afrika, sasa kama kuna sekta ambayo inaweza kutusaidia sisi kama Taifa kunufaika na mkataba huu sioni kama kuna sekta zaidi kuliko sekta ya kilimo. Umoja wa Mataifa unakadiria kwamba ifikapo mwaka 2021 Bara la Afrika litakuwa na watu wapatao bilioni 1.3 kwa maana hiyo kutakuwa na mahitaji makubwa sana ya kilimo. Kwa hiyo, Serikali yetu ikiwekeza kwenye kilimo tutaweza kunufaika tutatengeneza kwanza tutajitosheleza kwa chakula, pili tutapata malighafi kwa ajili ya viwanda na hatimaye nchi yetu itapata fedha nyingi zaidi na kuwekeza kwenye huduma mbalimbali za kijamii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la mwisho naomba nitoe ushauri kwa Serikali; hivi karibuni Israel imetoa nia ya kuisaidia nchi yetu kuipatia nafasi za masomo katika sekta ya kilimo zipatazo 100; lakini kwa bahati mbaya sana mpaka sasa tunapopzungumza bado nchi yetu haijatumia fursa hiyo vizuri.

Naiomba Serikali yetu tukufu ifanye kila linalowezekana tuwapeleke vijana wetu wakajifunze mbinu bora za kilimo na hasa kilimo cha umwagiliaji. Nchi ya Israel ni moja ya nchi ambazo zinafanya vizuri sana katika sekta ya kilimo. Lakini ushauri wa pili vijana hawa 100 tutakaowapeleka kila mwaka katika nchi ya Israel watakaporudi tuwape ardhi ipatayo hekari kama 10 hivi au 20 na tuwapatie mikopo ili waoneshe kwa vitendo kile walichojifunza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzetu Misri wanafanya hivyo, vijana wao ambao wanamaliza chuo kikuu hasa vyuo vikuu vya kilimo na mifugo wanapomaliza masomo wanapatiwa ardhi, wanapatiwa fedha katika kipindi cha miaka miwili au mitatu, wazalishe, wakishazalisha wanategemewa katika kipindi cha miaka miwili au mitatu warudishe mkopo na tukilifanya hicho jambo hilo katika kipindi cha miaka mitano mpaka 10 bila shaka sekta ya kilimo itapiga hatua kubwa sana za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. (Makofi)