Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kutoa mchango wangu katika bajeti yetu ambayo tunaendelea kuijadili hapa Bungeni. Awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa mapaji yake kutuwezesha wote kuwa salama na tunaendelea na kazi yetu vizuri kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anayoifanya pamoja na watendaji wake wote, lakini nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ndugu John Pombe Magufuli kwa jinsi alivyoweza kuangalia kipindi cha Hadubini cha TBC na kuwachukua wale wajasiriamali wawili, Ndugu Ngailo na Ndugu Mwafute kutoka katika Jimbo langu ambao wanafua umeme na wanasaidia wananchi wengine. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa lile alilolifanya na ninampongeza sana kwa hilo, lakini niseme tu kwamba bado wapo wengine, yupo Bwana Mhando yupo Kijiji cha Uliwa, lakini yuko Bwana Mwanyika yuko Uwemba pale anaunda mashine za maji basi kama Mheshimiwa Rais alivyosema, Mawaziri wanaohusika wajaribu kuangalia wataalam hawa ili waweze kusaidia maendeleo. Huyu anayeunda mashine za maji anaunda mashine za maji ambazo zinaendeshwa bila kutumia nguvu ya umeme, wala nguvu ya jua, wala nguvu ya mafuta. Zinatumia maji kwa maji, zinaitwa Hydraulic ram au kwa kifupi Hydram. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimepitia sana kitabu cha Mheshimiwa Waziri cha bajeti, lakini moja ya jambo ambalo ninaliona katika Wizara ya Fedha na bajeti nzima kwa ujumla ni kama vile suala la kodi imeachiwa Wizara ya Fedha na TRA, Wizara zingine zote ziko likizo kabisa hazina habari ya kodi wakati kumbe tungeweza kuhakikisha kwamba na Wizara zote zinasaidia kwa nguvu zote upatikanaji wa kodi. (Makofi)

Mimi ningelikwenda kwenye kodi moja tu ya Pay As You Earn, hii ni kodi ambayo wanatozwa wafanyakazi, lakini ziko Wizara ambazo zingeweza kusimamia ajira kwenye Wizara zao kupitia sekta binafsi, taasisi za sekta binafsi zikapata kuajiri watu wengi ili kusudi waweze kulipa Pay As You Earn. Kwa mfano, nikichukua Wizara ya Elimu, kwanza na-declare mimi ni mdau wa elimu, nikichukua Wizara ya Elimu kupitia NACTE. NACTE ndiyo inayosimamia vyuo vya kati. Viko vyuo vinakufa na chuo kinapokufa maana yake kinakosa wanafunzi na wafanyakazi wanakosa ajira, lakini watu wa elimu wao hawahangaiki, wacha tu kife wala siyo jukumu lao, lakini wajue kabisa kwamba pale kunakosekana ajira na Serikali inakosa kodi. Mwalimu mmoja mwenye mshahara wa shilingi 600,000 akikosa ajira katika chuo maana yake anashindwa kulipa Pay As You Earn ya shilingi 800,000 badala yake anakwenda kupewa kitambulisho cha machinga analipa shilingi 20,000.

Kwa hiyo, mimi nafikiri Wizara ya Fedha na Serikali kwa ujumla sasa itoe jukumu rasmi kabisa kwa Wizara zote na kuwe na database kila Wizara ihakikishe kwamba inakuza ajira ya sekta binafsi kwenye Wizara yake na ipewe na malengo kwamba tunataka katika Wizara yako bwana uhakikishe kwamba unasukuma ajira inayoweza kuleta Pay As You Earn kiwango hiki. Wakiwa na malengo hayo watahakikisha kwamba wanasimamia taasisi zao zisiyumbe na nafasoi hiyo wanayo. Kwa mfano, NACTE tumeiondolea jukumu la kugawa wanafunzi kwenye vyuo, tumeomba wanafunzi waombe kwenye vyuo matokeo yake ni kwamba wanafunzi wanaoomba kwenye vyuo kwa mfano, Chuo kama cha Mpwapwa cha Mifugo wanaomba wanafunzi 800, wanaochukuliwa na chuo ni wanafunzi 400, ada inayolipwa na mwanafunzi yule kwneye Chuo cha Mpwapwa ni kubwa kuliko chuo cha private kwamba NACTE wangepewa hiyo nafasi maana yake wale wanafunzi wengine waliobaki wangewagawanya kwenye vyuo vya binafsi na wangeweza kulipa. Hilo lilikuwa ni suala la kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini suala la ufungaji wa biashara, Mheshimiwa Waziri umezungumza vizuri sana, lakini ziko biashara huwezi kufunga. Kwa mfano, taasisi kama ya elimu hufungi, Maafisa wa TRA wamekuwa wakifunga account. Fikiria shule ya bweni, watoto wako shuleni wanahitaji kula, wanaweza wakaumwa, wanahitaji kupelekwa hospitali na nini, TRA wamefunga account za shule mpaka walipwe fedha yao, jambo hili linaumiza sana wamiliki wa mashule na linawafanya wamiliki wa shule wanashindwa kuhudumia watoto kwa sababu TRA wamefunga account. Mimi naomba utakapokuwa unajumuisha utuambie vitendo hivi vya kufunga account za taasisi kwa sababu taasisi kama shule huwezi kufunga, unafunga account za shule. Suala kama hili tunaliwekaje, naomba uliwekee ufafanuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeangalia bajeti haijasema vizuri sana juu ya wakulima, lakini tunasema kwamba wakulima ndiyo wanaotusaidia katika nchi kuhakikisha kwamba mfumuko wa bei upo hapo ulipo ni kwa sababu wakulima wetu wamelima chakula cha kutosha, chakula ndani ya nchi kipo cha kutosha. Niombe sana wakulima hawa wasaidiwe. Pembejeo ziko ghali sana, wakulima hawa hawana mbegu bora, wakulima hawa hawana nyenzo za kilimo lakini wakulima hawa hawana wataalam wa kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe la kwanza kabisa ambalo serikali mnaweza mkafanya jitahidini sana kuhakikisha kwamba wakulima udongo unapimwa ili kusudi ajue kabisa anapotia mbolea kwenye shamba lake anatia mbolea anatibu nini kwenye ule udongo. Sasa hivi imekuwa ni mazoea tu wanatumia mbolea udongo haujapimwa, lakini tupate Maafisa Ugani na Maafisa Ugani hawa wapate vyombo vya usafiri ili kusudi waweze kuwafikia wakulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mimi nadhani na sisi sasa tuombe wakulima tukutane na Mheshimiwa Rais tupeleke malalamiko yetu kwasabbau imeonekana kwamba sasa suluhisho la matatizo ni mpaka wadau wanaohusika na sekta hiyo wakutane na Mheshimiwa Rais. Sisi wananchi wa Jimbo la Njombe ni wakulima, tunalima sana viazi mviringo, tumelalamika sana juu ya lumbesa sana, lakini hakuna hata mmoja anayeshituka juu ya hiyo lumbesa. Lumbesa ina madhara. Madhara ya lumbesa kwanza kabisa inamnyonya mkulima, lumbesa inamuumiza yule mpakiaji wa ule mzigo. (Makofi)

Mimi ningedhani kwamba Wizara ya Afya ingetoa sasa vipimo kwamba binadamu anatakiwa kupakia au kubeba mzigo wenye uzito gani. Wale vijana wanaopakia ile mizigo wanabeba magunia yenye kilo 150 ni maumivu makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine ni kwamba mapambano haya ya lumbesa hivi leo neongea hapa kama watu wa vipimo wananisikia wataanza operation kesho Njombe na kuwaambia wananchi kwamba ninyi wananchi wa Njombe Mbunge wenu amelalamika juu ya lumbesa, sasa tunazuia lumbesa. Tunawaomba lumbesa ikazuiwe sokoni kwenye masoko makubwa kama ya Dar es Salaam, Morogoro, Dodoma na masoko mengine ndiko huko Lumbesa ianze kuzuiwa, lakini wasizuie wafanyabiashara njiani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiacha suala la kilimo, suala la miundombinu. Njombe tumelalamika sana, Jimbo la Njombe tumelalamika sana juu ya barabara ya Itoni - Manda. Barabara hii ndiyo barabara kuu ya kilimo. Kama kweli tunathamini wakulima, tunathamini shughuli za kusaidia nchi kupata chakula, hebu tuwezeshe hii barabara ya Itoni - Manda iweze kuwa bora, iweze kuwa ya lami. Fedha mnayotumia kama Serikali kukarabati ile barabara mara kwa mara ni nyingi ambayo mngeweza kutia lami kilometa moja moja leo hii ile barabara ingeshatiwa lami yote. Niombe sana barabara ya Itoni - Manda iweze kuangaliwa. (Makofi)

Jambo lingine ambalo sisi kama Njombe, kama Mkoa sasa ni suala la Mchuchuma na Liganga. Hili jambo limesemwa sana lakini nataka niwaambie hivi Serikali, hivi kuna ulazima gani wa kuhakikisha kwamba tunachimba chuma na tunachimba makaa ya mawe? Mimi ushauri wangu tuchimbe makaa ya mawe tuachane na chuma kwasababu makaa ya mawe yaliyopo pale tukichimba tani 300,000 kwa mwaka tutachimba miaka 150 wakati kile chuma tutachimba miaka 50 kitakuwa kimekwisha na makaa ya mawe ili uweze kuyachimba nyenzo ni chache, unahitaji bulldozer, unahitaji excavator, vitu viwili tu na malori ya kupakia makaa kupeleka sokoni. Hebu mtusaidie watu wa Njombe basi haya makaa yaweze kuchimbwa vinginevyo mkumbuke kama kuna kitu mkaitia Serikali kinaitwa rainfall alliance. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, rainfall alliance ni mkataba ambao Serikali iliingia leo hii chai inayolimwa na Magereza haiwezi kuuzwa kiwanda chochote kwa sababu wanasema ile ni forced labour, wafungwa hawaruhusiwi kuchuma chai. Sisi tukiwa shule za msingi tulichuma chai ya shule, leo hii haturuhusiwi kuchuma chai ya shule na kupeleka kiwandani. Kiwanda kinachonunua hiyo chai, chai yake haitanunuliwa kokote kule.

Sasa iko hoja inakuja huko duniani wanataka kupiga marufuku matumizi ya makaa ya mawe, sasa tutafika mahali haya makaa ya mawe ya Mchuchuma yatachacha na kwa sabbau tu tumeufungamanisha na mradi wa chuma. Hebu tuitenganishe hii miradi na tuhakikishe kwamba tunaanza kuchimba huu mkaa mara moja, kwa sababu hebu angalia kama ule mradi wa makaa ya mawe wa Ruvuma ule wa Ngaka, makaa yake tunapata shilingi ngapi na tukiongeza na huo wa Mchuchuma tungepata shilingi ngapi kama Serikali? Nafikiri tunajizuia wenyewe na tunaona kwamba maendeleo yetu yanakwama.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, sisi kama wananchi wa Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini tunaomba sana Serikali itusaidie na juzi nimeona Rais wa Congo alivyokuja na Rais wetu wanazungumzia juu ya biashara ya Congo na Tanzania na sisi tunaomba utusaidie ili kusudi tuweze kufanya hiyo biashara ya Congo na Tanzania.

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Muda wako umekwisha Mheshimiwa, kengele ya pili imeshagonga, ahsante sana.

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, ninaunga mkono hoja. (Makofi)