Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. KATANI A. KATANI: MheshimiwaSpika, nikushukuru sana na nadhani unajua kwamba mimi nikizungumza bajeti ya Wizara ya Fedha mimi naangalia sana kwenye kilimo kwa sababu asilimia 95 ya watu wangu wa Tandahimba ni wakulima.

Mheshimiwa Spika, ukisoma Fungu 43 la Wizara ya Kilimo fedha iliyokuwa imetengwa ilikuwa kama shilingi bilioni 98.11 ya kugharamia miradi ya maendeleo, lakini hadi kufikia Machi, 2019 fedha iliyokwenda ni asilimia 42 tu. Sasa kwa sisi wakulima maana sisi wengine ni wakulima typical kama imekwenda asilimia 42 Waziri wa Fedha nadhani hapa si sawa, pana namna ambayo unapaswa uangalie uone sekta hii ya kilimo ambayo kwa Taifa la Tanzania asilimia 85 ni wakulima, fedha inayotengwa ya maendeleo inakwenda angalau asilimia 70 ili kilimo hicho tunachokisema tukione kimekuwa.

Mheshimiwa Spika, lakini mmezungumza suala la ukuwaji wa asilimia tano kwenye sekta ya kilimo ambayo mimi napata mashaka kidogo, kwa sisi wakulima wa korosho ambao tulizalisha tani zaidi ya 300,000 mwaka 2017/2018 na msimu uliopita tumezalisha tani laki mbili na kitu tukaona kwamba kuna ukuaji unaongezeka kidogo ninyi wataalamu wa hesabu mnaweza mkatupa tathmini hiyo mnaitoa kwa vigezo gani.

Mheshimiwa Spika, lakini limezungumzwa hapa kwenye suala la kilimo tulikuwa na mfumo ule wa fedha ile export levy ambayo iliondolewa na mzee wangu pale Kamala alikuwa ameomba kwamba Serikali sasa ione namna bora ya kuleta pembejeo za ruzuku kwa ajili ya kusaidia wakulima. Hili nadhani Mheshimiwa Waziri uangalie kwa namna ya pekee sana, itakuwa jambo muhimu na busara sana kwa wakulima suala la ruzuku. Kwetu sisi kwenye korosho mfano msimu huu tusipopata ruzuku kutoka tani 200,000 hizo zinazozungumzwa kuna uwezekano mkubwa msimu huu tunaokwenda tunakwenda kuzalisha tani 80,000.

Kwa hiyo, ni ombi langu kwa Wizara ya Fedha ambayo mwaka jana fedha zetu zimechukuliwa, tumesamehe, zimekwenda, tuone basi namna ya ku-recover hili jambo at least wakulima wapate ruzuku ya pembejeo ya korosho ili tuende kuanza msimu vizuri.

Mheshimiwa Spika, lakini nizungumze suala la miradi ya mikakati, Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri kuna siku nilikuandikia memo pale nikiwa nakwambia Tandahimba ambayo ndiyo wazalishaji wakubwa wa korosho mradi wa mkakati ambao walishaleta na mradi ule godown mmeshindwa kupeleka Tandahimba ambako wanazalisha tani zaidi ya 70,000 unakwenda kujenga ghala sehemu inayozalisha tani 10,000 hizo fedha mnazopeleka kwenye tani 10,000 return yake itakuwa kwa muda gani? Kwa sababu hizo fedha mngepeleka Tandahimba wanakozalisha tani 70,000 maana yake baada ya miaka miwili, mitatu kulikuwa na possibility kubwa ya fedha zenu kurudi, lakini unapopeleka fedha, mmepeleka fedha Mkuranga ambako wanazalisha tani 4,000 ukaacha kupeleka fedha Tandahimba wanakozalisha tani 74,000 ninyi wenyewe wataalamu wa uchumi sijajua, sijajua kitaalamu mnafanya utaalamu wa namna gani? Mnataka fedha zirudi ziweze kuwasaidia watanzania wengine au mnapeleka sehemu ambako fedha zitakaa miaka 15, 20 tukawa tunaendelea kulalamika matatizo ya fedha.

Ombi langu kwa Serikali, miradi hii ya mikakati pelekeni kwenye Halmashauri ambazo zinaweza kurudisha fedha, mfano Tandahimba ambayo inazalisha korosho zinauwezo wa kuzalisha tani 70,000 ina uwezo wa kuzalisha tani 80,000 ungepeleka mradi wa mkakati kama wa godown ambao Halmashauri ishawaletea mradi huo na bahati nzuri ulikuwa vizuri sana, return yake ilikuwa ya muda mfupi, leo inawezekana tungekuwa tumeshaanza kurejesha. Niwaombe sana muangalie mambo haya kwa namna ya kibiashara na kuona namna mnavyoweza kuzichukua fedha kupeleka sehemu nyingine.

Mheshimiwa Spika, niwaombe sana watu wa Wizara ya Fedha tumeona Benki ya Kilimo, Mwanza wakati tumeenda wakati wa Kamati ya Kilimo tumeona wenzetu mmewapelekea tawi kule, lakini nimesoma kitabu chako Mheshimiwa Waziri nimeona Dodoma pana tawi, lakini nimeona mna maandalizi ya Kanda ya Nyanda za Juu Kusini kule Mbeya, nione sasa kuna umuhimu wa makusudi kabisa kwa sehemu yenye uzalishaji mkubwa mfano wa korosho Mtwara nako kuwe kwenye mpango wa kupeleka Benki ya Kilimo ili at least watu wale wapate mikopo…

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Katani.