Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Justin Joseph Monko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa na mimi nafasi ya kuchangia katika bajeti hii ya Wizara ya Fedha. Nianze kwa kuipongeza sana Wizara kwa bajeti nzuri ambayo wametuletea hapa na nina imani kubwa akiitekeleza hivi wanavyosema, wataweza kututoa hapa tulipo.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge waliotangulia wameanza kuzungumza mengi na mojawapo limekuwa ni Deni la Taifa na mimi niiombe tu Wizara kwa sasa Deni la Taifa kweli pamoja na kwamba limeongezeka, na Mheshimiwa Simbachawene amelielezea vizuri sana kwa sasa lakini tunaona kwamba deni hili linaendelea kuongezeka pamoja na kwamba inafanya miradi mikubwa ambayo kwa kweli tunaihitaji na ni miradi ya kimkakati ya nchi hii.

Mheshimiwa Spika, sasa wito wangu kwa Wizara ni kujaribu kuangalia kwamba deni hili liwe stahimilivu kama wanavyoendelea kusema kwa sababu ukiangalia sasa zaidi ya trilioni 50 wakati sisi uwezo wetu tunakusanya mapato ya ndani kwa trilioni 20, kidogo linakuwa na mashaka na hasa kwa sisi ambao siyo wachumi. Kwa hiyo, niiombe sana Wizara itupie macho kuhusiana na suala hili la Deni la Taifa na kuangalia tusijetukateleza.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni ukusanyaji wa mapato. Tunaipongeza sana Wizara wamefanya kazi nzuri ya kukusanya mapato na mimi nilitaka baadaye Mheshiwa Waziri atakapokuja, mwaka jana tulipitisha hapa, tulitoa msamaha wa kodi kwa mfano kwenye kulipia magari na nini. Nilitarajia sana kuweza kuona kwamba tuone msamaha huo uliotoka, mapato ambayo yalikuwa yamekusanywa yametusaidia kuongeza mapato kwa kiwango gani, lakini sijaliona hilo. Kwa hiyo, tunataka tuone namna ambavyo Wizara hii inaweza ikasimamia mapato hayo ambayo yanatusaidia katika utekelezaji wa miradi mbalimbali na hata ulipaji wa pensheni, nyongeza hata za mishahara pamoja na mambo mengine ambayo yanatokana na kuongezeka kwa mapato.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninataka nimuombe Waziri atakapokuja tuweze kujua, kitu ambacho Waheshimiwa Wabunge walipitisha mwaka jana hapa kimeleta manufaa gani.

Mheshimiwa Spika, na labda kazi kubwa ambayo Wizara inatakiwa kufanya sasa ni kujaribu kuendelea kuboresha mazingira ya ukusanyaji wa kodi, hasa kwenye maeneo mengi ili wananchi wengi waweze kulipa kodi. Bado wako wananchi ambao wanaendelea kukwepa kodi kwa sababu wakati mwingine mazingira ya ulipaji au kodi zenyewe siyo rafiki. Kwa hiyo, niombe sana Wizara iweze kuboresha kwenye maeneo haya ili wananchi waweze kulipa kodi inavyostahili.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la miradi na hasa miradi ya PPP; hotuba ya Mheshimiwa Waziri imeeleza vizuri sana, na kwamba sasa hivi wana mikakati ya kuweza kuzisaidia Halmashauri ili ziweze kuongeza uwezo wake wa ukusanyaji wa mapato. Kwa hiyo, niombe Wizara iweze kuwasaidia.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu tukiangalia, kwa mfano katika Halmashauri yangu ya Singida DC tuna miradi ambayo tumekwishakuiandika lakini imekwenda kwa muda mrefu na hatujapata fedha. Tumeomba kwa ajili ya ujenzi wa mradi wa soko pale Njiapanda ya Meriya na andiko hili limekuja muda mrefu, limepita katika hatua mbalimbali katika ngazi za mkoa na limekwishakwenda huko Wizarani, lakini katika bajeti hii sijaona kama limepata kibali cha kupata fedha.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ile bado ni duni sana, mwaka uliopita tulikusanya chini ya shilingi bilioni moja. Kwa hiyo, tunahitaji sana fedha hizi kwa ajili ya miradi hii mkakati ili tuweze kuongeza uwezo wetu na kuweza kuwasaidia wananchi. Kwa sababu mapato ya ndani ya halmashauri yanategemewa sana na vijiji vyetu, yanategemewa sana na akina mama, vijana na walemavu na yanategemewa sana na Waheshimiwa Madiwani katika kutekeleza miradi mbalimbali kule kwenye Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niombe sana Wizara ijaribu kuliangalia suala hili, ipitie na kama liko tatizo la maandiko ambayo tunaandika kutoka kwenye Halmashauri basi Wizara itusaidie ili maandiko haya na yenyewe yaweze kukidhi vigezo.

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Justin Monko.

MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, ahsante sana. (Makofi)