Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nashukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia bajeti hii muhimu iliyo mbele yetu, ni bajeti muhimu sana kwa sababu ndio roho ya uchumi wa nchi, inasimamia roho ya uchumi wa nchi.

Kwanza nianze kwa kusema kwamba naunga mkono hoja, lakini ninayo mambo machache ambayo ningependa nishauri, ili Wizara iweze kuyazingatia na Serikali iweze kuyazingatia.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia ukurasa wa 10 Mheshimiwa Waziri ameeleza vizuri kwamba uchumi wa Taifa au pato la Taifa limekua kwa asilimia saba, ni jambo jema na ninampongeza kwa kazi hiyo, lakini alipoanza kubainisha sekta ambazo zimekua kwa kasi; sekta ya kwanza ambayo ameonesha kwenye kitabu, nitatumia yaliyoandikwa tu kwenye kitabu, ya kwanza amesema ni sanaa na burudani imechangia kwa asilimia 13.7. Nikasema hilo ni jambo jema, sanaa na burudani. Sekta iliyofuata ni ujenzi asilimia 12.9, sekta iliyofuata ni uchukuzi na uhifadhi wa mizigo asilimia 11.8 na sekta nyingine aliyoitaja ni habari na mawasiliano asilimia 9.1.

Mheshimiwa Spika, sasa nilipofika hapo nikastuka kidogo nikasema sasa kilimo vipi, mbona wala hakitajwi hapa? Maana ukiona uchumi sasa sanaa na burudani ndio inachangia kwa kasi, ndio imekua kwa kasi, ni jambo jema, lakini lazima ujiulize kilimo vipi?

Mheshimiwa Spika, sasa kilimo baada ya kuangalia kwenye nyaraka nyingine ni kwamba chenyewe kimekua kwa asilimia 5.3. Sasa kwa nchi yetu hii ambayo wananchi wengi ni wakulima na sehemu kubwa kwa kweli ya Watanzania ni wakulima, ukiona kilimo hakikui vizuri basi ujue hata ukienda kwa wananchi kuwaelezea kwamba uchumi unakua wao watashangaa kwa sababu sio sehemu ya kukua huko. Ndio maana namuomba Mheshimiwa Waziri akija wakati wa kufafanua atualeze kidogo walao na wakulima wasikie na wao wamekua kwa kiasi gani, walau wawe na matumaini kwamba sasa Serikali kuna mambo inayafanya yatakayosaidia na kilimo na chenyewe kukua. Wasanii na burudani barabara, lakini huenda ni kwa sababu tu si kwamba wasanii wamefanya mambo mengi ila kwa sababu sekta zilizo muhimu hazijakua kwa hiyo na zilizokua palepale zinaweza kuonekana kwamba sasa zenyewe ndio zinakua kwa kasi, hilo jambo la kwanza.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo ningependa kuchangia ni mfumuko wa bei. Ukisoma kitabu cha Mheshimiwa Waziri kinatueleza vizuri kwamba mfumuko wa bei ni asilimia 3.2. Ni jambo jema, nampongeza kwa hatua hiyo, lakini mimi nikajiuliza, nikaangalia huu mfumuko wa bei unachangiwa na nini hasa kutokua, kwa nini tunafanya vizuri?

Mheshimiwa Spika, nikagundua tunafanya vizuri sasa tuwapongeze wakulima kwa sababu mfumuko wa wakulima wa chakula wenyewe umekua tu kwa asilimia 3.2 na ni kwa sababu wakulima wetu hawa wanaweza kuzalisha chakula kwa wingi na cha uhakika na ndio maana wanalinda mfumuko wetu wa bei. Kwa hiyo, lazima tuwapongeze wakulima wetu hawa, lakini nikajaribu kujiuliza sasa ni wapi ambapo sasa huyu Mheshimiwa Waziri ambaye mfumuko wake wa bei unaendelea kuwa mdogo kwa sababu tu wakulima wana mazao, bei hazipandi za mazao ya wakulima kwa sababu tuna sera ambazo zinahakikisha wakulima hawa wanalipwa kidogo.

Sasa kama tuna sera zinazohakikisha wakulima hawa wanalipwa kidogo ili mfumuko wa bei usipande ukaharibu vitu vingine, je, wakulima hawa tunawapelekea ruzuku maalum kiasi gani ya kuwawezesha kunufaika na mfumuko wa wa bei unaoendelea kwa kidogo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maana mtu akikutendea jamo jema basi na yeye lazima umpe fadhila na fadhila ya kwanza kabisa ka mkulima ni ruzuku ya mbolea, lakini sioni. Nimejaribu kupitia sana labda kwenye sekta, labda tutaona badae, sijaona ruzuku ya mbolea tunayopeleka kwenye kilimo, sijaona mkakati maalum. Nchi nyingine duniani zinakuwa na mfumuko kidogo wa mazao ya kilimo, lakini kwa mfano kule Ubelgiji wakulima wanaambiwa kwamba bwana tunakuomba wewe usizalishe eneo lako na kwa kuwa hautazalisha sisi tunajua ungezalisha ungeweza kuzalisha maziwa mengi, kwa hiyo, kwa mwaka huu tunakulipa pesa hii ya maziwa ambayo ungezalisha, lakini wewe pumzika usizalishe, ili kulinda bei ya mazao, lakini sasa sioni mikakati ya makusudi ya namna hiyo, ndio maana nashauri Waziri wa Fedha aanze kuangalia ni kwa namna gani huu mfumuko wa bei ambao unakuwa wa chini na anayechangia sana ni mkulima na kwa sababu anazalisha kwa wingi, kwa nini tusimfikirie huyu mkulima kumwezesha, kumsaidia?

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ni uhimilivu wa Deni la Taifa; ukisoma kitabu cha Mheshimiwa Waziri ametuambia deni la Taifa limepanda kutoka trilioni 49.86 mpaka trilioni 51.03 na akatueleza vizuri tu akasema hiyo ni sawasawa na kupanda kwa asilimia 2.35. Sasa na mimi nikasema ngoja na mimi nijifanye nisiyejua hesabu, nijifanye sijui hesabu na sijui hesabu ngumu ngumu; nikasema kama kwa mwaka mmoja Deni la Taifa limeongezeka kwa asilimia 3.5 je, kwa miaka mitano deni hili litaongezeka kwa asilimia ngapi? Hesabu zikaniambia litaongezeka kwa asilimia 17.2. Nikapata mstuko kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini namuomba sasa Mheshimiwa Waziri akija baadae anihakikishie kwamba Mheshimiwa Kamala usiwe na wasiwasi, deni hili halitakuwa hivyo kama unavyofikiri, bali litakuwa kidogo. Akishaniambia hivyo, ajiandae kwa sababu nitamuuliza litakuwaje kidogo kwa sababu bado tunaendelea, Stiegler’s Gorge ndio tumeanza na fedha nyingi lazima ziende huko, lakini nitamueleza pia SGR ndio tumeanza na fedha nyingi lazima ziende huko na ametueleza yeye kwamba, fedha katika masoko ya nje, misaada ya wahisani imekua migumu migumu sana kwa hiyo, lazima tuendelee kutafuta fedha ndani na nje, nitamuuliza maswali hayo kwa hiyo, kukopa lazima kuendelee na kukopa si dhambi, cha msingi mnajipanga vipi kulipa na mkopo huo unautumia namna gani?

Mheshimiwa Spika, lakini mambo haya lazima tuyazungumze kwa sababu ndio kazi ya Mbunge. Kazi ya Mbunge ni kuzungumza, ni kutumia microphone na kushauri. Na lazima tushauri kwa msisitizo.

Kwa hiyo, lakini uhimilivu wa deni mwingine wanasema mauzo ya nje sasa tumeweza kufikia asilimia 157.3 hii tuko chini ya ukomo ambayo ni asilimia 240, lakini kwa hesabu ya haraka haraka ni kwamba asilimia 82 tu ndio zimebaki, hiyo maana yake hiyo. Nikaangalia na kutumia mapato ya ndani kulipa deni nikaona sasa ni asilimia 15 na ukomo ni asilimia 22 nikajua sasa kumbe tumebakiza asilimia sita. Kwa hiyo, hivi viashiria vya ukomo wa deni pamoja kwamba ni vizuri hapa, lazima tukubaliane kuna taa ya njano imeanza kuwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na ukiwa unaendesha gari ukakutana na taa ya njano lazima kwanza ushike brake kidogo na kama gari lako ulikuwa hujakagua brake usiendeshe tu, uanze kukagua brake ziko namna gani, na kama mafuta yameanza kwisha ile taa ya mafuta ikiwaka basi simama kwenye kituo cha karibu ujaze mafuta ili uendelee na safari. Ukiyadharau haya ukasema gari halijasimama ukaendesha tu, utapata tatizo na uendeshaji wa gari wa style hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho naomba niseme niko kwenye Kamati ya Bajeti na ninakushukuru Mheshimiwa Spika ulinipeleka kwenye hiyo Kamati, nakushukuru sana, nimejifunza mambo mengi. Moja nililojifunza ni kwamba tunakusanya saa nyingine fedha ambazo tunajua hizi fedha hatukutakiwa kuzikusanya, tunasema tuta-refund, lakini hatu- refund.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano kwenye madini peke yake wanadai bilioni 600, ukienda kula TBL wanadai-refund bilioni nyingi tu, ukienda viwanda vya soda wanadai fedha. Sasa shida ya fedha ambazo humrudishii mtu na ulitakiwa umrudishie fedha yake unapokaanazo ni kwamba unakuwa umeshikilia mtaji. Unaposhikilia mtaji ni kwamba unakuwa umeshikilia ajira; unaposhikilia mtaji, unaposhikilia fedha za kampuni maana yake umeshikilia ajira za Watanzania. Huyu badala angeweza kuwa na mipango ya kuajiri zaidi inabidi asitishe ajira ili aweze kuendelea kiwanda chake kwenye …, kwa hiyo, nasema eneo hili ambako ni mabilioni ya fedha nyingi tu yapo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini hakuna kinachoshindikana katika Bunge. Kama Serikali inaona zile fedha lazima aendelee kuzitumia basi ituletee hapa turekebishe sheria kwamba wasisubiri chochote fedha hizi sasa zinakuwa rasmi za Serikali na wajipange vizuri kwa siku zijazo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)