Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Nitumie nafasi hii kwanza kabisa kumshukuru Mungu lakini pia kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri. Mheshimiwa Naibu Waziri na Watendaji wao Wizarani wanafanya kazi kubwa, wanafanya kazi nzuri sana hongera sana kwa kazi nzuri wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja kwa mujibu wa tafiti mbalimbali duniani moja ya njia bora kabisa ya kuondoa kama sio kupunguza migogoro ya ardhi ni kupima na kupanga matumizi bora ya ardhi. Hii ndio moja ya njia bora kabisa pamoja na kwamba tunakubaliana kwamba kwa mujibu wa sheria zetu Planning Authority ni kule kwenye Serikali za Mitaa, lakini Wizara ndio yenye jukumu la kusimamia kutekeleza sera kwenye Sekta ya Ardhi. Naomba sana pamoja na changamoto za kifedha na za kibajeti watutafutie mkakati maalum wa kupima na kupanga maeneo yetu. Tume ya Mipango ya Ardhi inafanya kazi nzuri, lakini bado uwezo wake ni mdogo na imebaki kuwa kama waratibu tu.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni kwenye mashamba yasiyoendelezwa. Nitumie nafasi hii kwa dhati kabisa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, tangu ameingia amefanya kazi ya kufuta hati za mashamba ya baadhi ya wawekezaji ambao hawayaendelezi vizuri na hata kule kwetu Korogwe, hili pia limefanyika pamoja na maboresho yaliyofanyika kwenye mashamba yale sita ambayo yalifutwa, bado alichokifanya Mheshimiwa Rais kinawasaidia sana watu wetu na sisi watu wa Korogwe tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, ninayo mashamba mengine kule na nimeshamwambia Mheshimiwa Waziri zaidi ya mara moja na namwamini sana baba yangu na naikubali sana kazi yake, kama pale Wizarani kuna watu wanakwamisha yasifike kwa Mheshimiwa Waziri hebu aingie ndani aangalie kuna nini huko, kuna shamba la pale Mwakinyumbi, Hale. Nimekuja juzi kwenye Bunge lakini hii nazungumza ni mara ya tatu kama sikosei.

Mheshimiwa Spika, kuna shamba linaitwa Kwashemshi, kuna mwekezaji anasema yeye ni mwekezaji wa Mkonge, anakodisha kwa watu wengine, miaka miwili iliyopita alikuwa anakodisha kwa wananchi walime mahindi kule ndani kwa sababu eneo kubwa halijalimwa mkonge. Mwaka huu ameamua mpaka na kuwafukuza wananchi amechukua mtu binafsi amekuja analima mahindi kwenye shamba hilo, wananchi hawana maeneo.

Mheshimiwa Spika, mimi ni muumini ambaye naamini kabisa sio sawasawa kila ardhi ya mwekezaji tukaichukua tukagawa kwa wananchi, hatuwezi kuwa nchi ya namna hiyo, lakini lazima tukubaliane kama mtu amepewa ardhi haitumii kwa mujibu wa masharti aliyokabidhiwa masharti yake ya umiliki, wahukue hatua. Hili suala nimelisema muda mrefu, namwomba sana Mheshimiwa Waziri aingie, najua kwake mara naambiwa halijafika, mara limefika likarudi, sielewi kinachoendelea hapo, hebu aangalie Mheshimiwa Waziri hapo kwenye Wizara, kuna mtu atakuwa anacheza na hivi vitu, kuna shamba linaitwa shamba la Mwakinyumbi.

Mheshimiwa Spika, huu ni mwaka sijui wa ngapi tunalalamika na hili jambo. Marehemu Profesa Majimarefu amepiga kelele sana humu ndani mpaka Mwenyezi Mungu amemchukua, hatujui kinachoendelea kwenye mashamba haya. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri kwa unyenyekevu mkubwa na kwa kazi yake anayoiamini awasaidie watu wa Korogwe waweze kupata maeneo, lakini pia kazi zifanyike vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri jambo lingine hasa kwa niaba ya vijana wote lakini na Watanzania kwa ujumla, sasa ni wakati muafaka wa kuwa na sera ya nyumba. Ni wakati muafaka kama Taifa kuwa na sera ya nyumba, hebu Wizara walifanyie kazi hili jambo tuweze kufikia mahali pazuri.

Mheshimiwa Spika, yamesemwa hapa na nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kazi anayoifanya, ile kazi tuliyoikuta inafanyika Kilombero, Ulanga na Malinyi ilikuwa ni kazi nzuri sana nimpongeze yeye lakini niipongeze na ile timu iliyokuwa inasimamia ule mradi. Mheshimiwa Waziri kwenda kugawa hati ni sehemu ya namna ya kusadia kutatua changamoto za migogoro ya ardhi kwa watu wetu, hakuna kosa. Korogwe pia tukipima tutamwita Wziri aje atugawie hati na sisi tutapokea.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri anafanya kazi nzuri, sina maneno mengi, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)