Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Saed Ahmed Kubenea

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Ubungo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, nimshukuru pia Mheshimiwa Waziri, kwa kazi kubwa ambayo imefanyika kwenye Jimbo la Ubungo hasa kwenye eneo la urasimishaji wa maeneo ya watu ambao walikuwa wanakaa kwenye maeneo yasiyo rasmi. Mheshimiwa Wazri, hongera sana kwa kazi hiyo na tunaomba ile kazi ikamilike. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia namshukuru kwa master plan ya Dar es Salaam ambayo sisi kama wadau tumeshirikishwa kwa sehemu kubwa. Tunaomba ile master plan ikamilishwe ili Dar es Salaam mpya iweze kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la migogoro katika ardhi mingi inachangiwa na wafanyakazi wa Wizara ya Ardhi ambao sio waaminifu na sio waadilifu. Hapa naomba ni- declare interest kwa sababu jambo hili na mimi linanigusa kidogo kwamba kuna kiwanja katika maeneo ya viwanja 20,000 vilivyopimwa Dar es Salaam kuna mmoja wa wafanyakazi wa Wizara ya Ardhi alienda kumega lile eneo na akajimilikisha na Mheshimiwa Waziri, taarifa hizi zimefika Wizarani kwake lakini kwa mshangao mkubwa ameshindwa na kigugumizi kushindwa kuchukua hatua.

Mheshimiwa Spika, nashangaa kwa sababu Mheshimiwa Waziri amekuwa jasiri kwelikweli wa kutatua migogoro ya ardhi katika maeneo mengi lakini migogoro kama hii inayomgusa kwenye Wizara yake yeye mwenyewe anashindwa kuchukua hatua. Kwa hiyo, nimkumbushe Mheshimiwa Waziri kaka yangu Mheshimiwa Lukuvu ufanye hii kazi ambayo tumekuletea na kama unataka ukumbushwe zaidi umesahau tukuletee hizo nyaraka ili uweze kuzifanyia kazi haraka iwezekanavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni kuhusu National Housing ambalo limezungumzwa kidog na mzungumzaji aliyepita. National Housing imefanya miradi mikubwa Dar es Salaam na miradi mikubwa mitatu imesimama. Mradi wa Kawe na ule mradi wa Victoria. Mradi wa Kawe ulikadiriwa kutumia shilingi bilioni 114 wakati unaanza, karibu dola za Marekani milioni 63.9. lakini sasa hivi baada ya kusimama unakadiriwa kutumia shilingi bilioni 142. Mradi haujaenda mbele, National Housing imekopa kwenye taasisi za fedha. Mkopo ule unalipwa kutokana na mradi wenyewe, mradi umesimama. Matokeo yake National Housing wanalipa kutokana na mapato ya ndani ya kila siku ya kodi ambazo tunalipa sisi wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni muhimu sana Serikai ikachukua hatua za dharura kuruhusu National Housing waendelee kukopa ili kukamilisha miradi waliyoanzisha. Mradi kama ule wa Victoria, umekamilika kwa karibu asilimia 95 lakini National Housing wamezuiwa kuendelea kujenga kwa sababu wamezuiwa kukopa na baadhi ya benki zilishahamisha matawi yao kwa mfano Benki ya NBC ilikuwa na tawi Kinondoni pale eneo la Manyanya, wamefunga lile tawi wakitegemea watahamishia huduma zao kwenye tawi la Victoria na walishamaliza mkataba na yule mwenye jengo. Leo wamezuiwa kuendelea na Victoria NBC wamehamishia tawi lao pale Victoria. Kwa hiyo, wanapaswa kuhamishia hapo kwenye hilo jengo jipya, hawawezi kuhamishia kwa sababu jengo limesimama, jengo haliwezi kuendelea kwa sababu National Housing wamezuiwa kukopa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa jambo hili litaifanya National Housing isambaratike kabisa. Kwa hiyo, mikopo hii ni mikubwa kweli kweli sio mkopo wa bilioni moja au mbili, tunazungumzia mkopo wa bilioni 244, sio fedha ndogo kwa shirika kama hili! Na shirika limefika kikomo cha kukopa, limeomba ruhusa ya Serikali liruhusiwe kukopa kwa dharura. Serikali haitaki kutoa kibali. Mheshimiwa Waziri, jitahidi sana shirika hili lisije kufa mikononi mwako, utapata aibu. Limetoka mbali National Housing ilikuwa haijulikani kabisa, limejengwa vizuri, leo ina miradi mikubwa, ina miradi mpaka hapa Dodoma, isije ikafa mikononi mwako. Jitahidi sana.

Mheshimiwa Spika, nadhani kuna matatizo makubwa sana kwenye Bodi zetu za Wakurugenzi wa Mashirika ya Umma. Ni vizuri tunapoteua Bodi kwa sababu haiwezekani mkopo huu wote ukapita tu hivi hivi bila bodi kuangalia na kama Serikali inakuja kuona leo maana yake Bodi ilishindwa kuwajibika na ndiyo maana Serikali ilivunja Bodi ya National Housing. Kwa hiyo, nafikiri tunapounda Bodi zetu tuache kuingiza ushabiki wa urafiki, tuache kuingiza ushabiki wa siasa…

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. SAED A. KUBENEA: …tujenge Bodi imara. Nakushukuru sana. (Makofi)