Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uzima na afya njema kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu kuchangia hoja iliyo mbele yetu ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchukua nafasi ya kipekee, kama wenzangu walionitangulia, kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa uongozi wake madhubuti na makini unaoendelea kugusa, siyo tu wananchi wa Tanzania, bali wa kuigwa katika nchi za Bara la Afrika na dunia kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa uongozi wake ndani ya Bunge hili. Aidha, napenda kuwapongeza sana Mheshimiwa Spika na Naibu Spika kwa namna ambavyo mnaliongoza Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kumpongeza kwa kipekee, Mheshimiwa Prof. Palamagamba Aidan Mwaluko Kabudi, Mbunge, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, kwa uongozi makini na kuhakikisha tunapata ufanisi mkubwa katika utekelezaji wa majukumu ya Wizara anayoiongoza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nampongeza Mheshimiwa Andrew Chenge, Mheshimiwa Mussa Azzan Zungu na Mheshimiwa Najma Martaza Giga kwa namna wanavyoonesha uwezo mkubwa wa kuongoza Bunge katika kipindi hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mwenyekiti na Wajumbe wote wa Kamati ya NUU kwa ushauri na maoni yao katika utekelezaji wa majukumu ya Wizara. Pia nawashukuru sana Wabunge wenzangu wote kwa ushirikiano wao wanaoendelea kunipa. Nawaombea kila la heri katika utekelezaji wa majukumu yao hapa Bungeni na kwenye majimbo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya kipekee, napenda kuwashukuru wananchi wenzangu wa Jimbo la Songea Mjini kwa imani kubwa wanayonipa na wanayoendelea kuionesha. Nitaendelea kuwa nao karibu na kushirikiana nao katika kuleta maendeleo makubwa na naahidi kuwa sitawaangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuishukuru sana familia yangu, ikiongozwa na mke wangu mpendwa, Flora Ndumbaro, kwa uvumilivu kwangu na kwa namna wanavyonisaidia na kuniunga mkono katika majukumu yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, shukrani za dhati ziende kwa Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu, Mabalozi, Wakurugenzi, Watumishi na wasaidizi wangu katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa ushauri na msaada wao katika utekelezaji wa majukumu yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huo, nianze sasa kujibu hoja mbalimbali zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge. Kwanza, nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia hoja hii ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Ni dhahiri kwamba michango yao itatusaidia sana katika kufanikisha shughuli za Wizara na kuimarisha ufanisi wa utendaji wa Wizara.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ya kwanza ambayo napenda kuiongelea ni suala la kuondoka kwa Balozi wa Jumuiya ya Ulaya hapa nchini. Mtoa hoja alisema Serikali ieleze ni kwa nini iliweka shinikizo la kumwondoa Balozi huyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama Wizara na kama Serikali tulipokea tamko kutoka ka wenzetu wa Jumuiya ya Ulaya mnamo tarehe 5 Novemba, 2018 likisema kwamba limemuita Balozi huyo nyumbani kwa majadiliano. Suala la kuja Balozi yeyote hapa nchini, kuishi kwake na kuondoka kwake kunaratibiwa na Mkataba wa Vienna unaohusu mahusiano ya kidiplomasia wa mwaka 1961. Katika mkataba huu, nchi ambayo imemleta Balozi huyo ina mamlaka ya kumwondoa pasipo kutoa sababu kwa nchi nyingine yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tulipata taarifa ya kuondoka kwa Balozi huyu hatukupewa sababu yoyote ile. Hivyo, kututaka leo tutoe sababu wakati sisi siyo tuliomwondoa na sisi hatukuambiwa ni kwa nini ameondoka, siyo sahihi. Waliomwondoa ndiyo wako kwenye nafasi ya kutoa sababu ni kwa nini walimuondoa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna hoja ya Brexit. Mtoa hoja amesema Serikali itoe msimamo wake kuhusiana na hoja ya Brexit. Brexit ni hatua ya Uingereza kujitoa katika Jumuiya ya Ulaya. Sisi tuna mahusiano mazuri na Jumuiya ya Ulaya na Uingereza lakini pamoja na mahusiano hayo mazuri hatuingilii mambo yao ya ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sababu za Uingereza kujitoa zinamhusu yeye, kwa sababu sera yetu sisi hatuingilii mambo ya ndani, tunasubiri maamuzi ya mwisho ya Brexit. Endapo watajitoa ndipo tutaanza mchakato wa kuanzisha mahusiano binafsi na Uingereza au wataalam wanasema bilateral relations. Kwa hivi sasa kwa kuwa mahusiano yetu na Jumuiya ya Ulaya ni mazuri tusingependa kuingia katika suala hili la Ulaya na Brexit. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia suala la EPA liliongelewa na kusema kwamba nchi nyingine zimeshasaini EPA ispokuwa sisi. Naomba nitoe taarifa kwamba zaidi ya asilimia 50 ya nchi za Afrika hazijasaini EPA. Katika Afrika Mashariki, kati ya nchi sita ni nchi mbili tu zimesaini EPA, nchi nne, ambazo ni nyingi, hazijasaini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hawajasaini siyo kwamba hawaipendi, nchi nyingi ikiwemo Tanzania tume-raise concern. Sisi Tanzania tumehoji vifungu nane vya mkataba wa EPA. Katika vifungu nane hivyo tume-raise issues 12 ambazo tunasema zikiwa-addressed tutasaini mkataba wa EPA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, moja kati ya issues, niwasaidie tu, ni kwamba mkataba huo unakwenda kupoka mamlaka ya Bunge hili hasa kwenye kutunga sheria zinazohusiana na fedha au kodi. Sasa hatuwezi kusaini mkatana ambao unapoka mamlaka ya Bunge pasipo Bunge lenyewe kuridhia. Kwa hiyo, suala hilo siyo la kwetu sisi tu, ni la Bunge hili na ni la Watanzania wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, imeongelewa pia hoja kuhusiana na haki za binadamu. Naomba niseme, haki za binadamu ni suala mtambuka na zinaangaliwa sana kwa mujibu wa Kikanda. Sisi Afrika tuna Mkataba wa Afrika wa Watu na Haki za Binadamu, wenzetu wa Ulaya wana Mkataba wa Haki za Binadamu, neno watu halipo, hiyo ni tofauti kubwa sana ya mtazamo wa haki za binadamu kati ya Afrika na Ulaya. Ndiyo maana sisi kwa muktadha wetu tumeanzisha Mahakama yetu iliyoko pale Arusha ili masuala ya haki za binadamu kwa muktadha wa Kiafrika tuyashughulikie kwenye Mahakama zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapokuja sasa kuanza kucheza ngoma ambazo siyo za kwetu tunakuwa tunapotoka. Kwenye hili, naomba nirejee ushauri mzuri aliyoutoa Mheshimiwa Mnzava kwamba katika kutatua changamoto za haki za binadamu Tanzania tuna mihimili ya kutosha; tuna Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Mahakama Kuu ambayo ina mamlaka kwenye haki za binadamu, Mahakama ya Afrika Mashariki ambayo pia inashughulikia haki za binadamu na Mahakama ya Afrika inayoshughulikia haki za binadamu ambayo iko Arusha. Kwa kuonesha umuhimu Mahakama hizi mbili, ya Afrika Mashariki na ile ya Afrika, ziko Tanzania, ziko Arusha, tumeziweka hapa kwa sababu tunapenda na tunalinda haki za binadamu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba tu niseme katika haki za binadamu tuko vizuri pengine kuliko nchi ambazo watu wengi wanaziongelea. Niwape mfano tu, kuna nchi ambazo tunazisema sana humu ndani, hazijasaini Mkataba wa Haki za Mtoto Duniani lakini mnadhani kwamba hizo ndiyo zinatimiza haki za binadamu. Nchi hizo hazijasaini Mkataba wa Rome Statutes ambao unashughulikia masuala ya ICC.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote kwenye kipengele cha haki za binadamu tuko vizuri. Tufuate vyombo hivi ambavyo vipo, tuache kupeleka masuala ya haki za binadamu sehemu ambako hakuhusiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchukua fursa hii, kwa namna ya kipekee, kumpongeza sana Waziri, Mheshimiwa Prof. Palamagamba Kabudi. Najua wengi wangetamani Mheshimiwa Prof. Kabudi aweze kujibu mambo ambayo siyo mazuri. Mheshimiwa Prof. Kabudi anafanya kazi vizuri, tuna wazalendo wachache sana nchi hii kama yeye. (Makofi/Vigelegele)

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, watu huwa tunasubiri mpaka mtu afe ndipo tumsifie.

Naomba mimi nimsifie Mheshimiwa Profesa Kabudi wakati bado anaishi na angalau na yeye mwenyewe apate pongezi hizi. (Makofi)

MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu utaratibu.

NAIBU SPIKA: Kanuni inayovunjwa Mheshimiwa Mbilinyi?

MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu utaratibu, nikishaeleza ndiyo nitasema, naomba nafasi kwanza.

NAIBU SPIKA: Unasimama kwa mujibu wa Kanuni gani? Usiwe mbishi bila sababu na wewe ni Mbunge wa siku nyingi, kanuni inayovunjwa ni ipi. (Makofi)

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, endelea.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mbilinyi, naomba ukae, Mheshimiwa Naibu Waziri endelea.

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, wazalendo kama Mheshimiwa Prof. Kabudi ni wachache. Hii ni tunu ambayo Mwenyezi Mungu ametujalia, tunapaswa kuienzi na kuilinda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Prof. Kabudi ameifanyia mema nchi hii, mambo ya kihistoria, ametuletea sheria mbalimbali nzuri na anaongoza Wizara hii kwa ufanisi wa hali ya juu. Naomba Waheshimiwa Wabunge wote tuchukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Prof. Kabudi, tumtakie maisha marefu ili aendelee kutumikia Tanzania kizazi na kizazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)

WABUNGE FULANI: Unga mkono hoja.

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)