Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Kama kijana wa Kitanzania kiongozi nasimama kwa uchungu sana kwa yanayoendelea ndani ya Bunge letu. Tunapofanya siasa na kuchafua sura ya Taifa letu badala ya kulitetea na kuliweka vizuri Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, muda ni mchache, nizungumze mambo machache. Jambo la kwanza nizungumze nafasi ya haki za binadamu kwenye mahusiano ya Kimataifa. Nakubaliana kabisa kwamba haki za binadamu zina nafasi kubwa kutuweka kama Taifa kwenye sura nzuri kwenye ulimwengu huu, kwenye mahusiano yetu na nchi nyingine na Mataifa mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu ambacho tunasahau, Tanzania ni miongoni mwa nchi chache sana ambazo zinatii na kufuata haki za binadamu. Ni miongoni mwa nchi chache sana ambazo haki za binadamu hazitajwi tu, tumeziweka kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Sura ya Kwanza, sehemu ya tatu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika…

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Taarifa.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, zaidi ya hayo…

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Taarifa.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Kwenye nchi yetu tunazo sheria zilizotuwekea utaratibu, tunayo institutional and legal framework ya namna… (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, muda hautoshi.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

NAIBU SPIKA: Hakuna mtu ametoa taarifa, Mheshimiwa Salome naomba unyamaze. Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa naomba ukae nimeshasimama, naomba ukae. Waheshimiwa Wabunge tujifunze kuheshimu mamlaka…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

NAIBU SPIKA: Nasema hivyo kwa sababu, nisikilizeni. Mheshimiwa Susan Lyimo amechangia dakika zake tano hakuna mtu nimemruhusu kusimama, Mheshimiwa Lulida amechangia hakuna mtu amesimama na huyu mchangiaji wa CCM atachangia bila mtu kusimama. Mheshimiwa Timotheo Mzava. (Makofi)

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa hoja yangu ni hii, kwamba kwenye nchi yetu tunayo Katiba na tunazo Sheria za Haki za Binadamu na namna ambavyo mtu atakuwa anahisi haki za binadamu zimevunjwa, aende kwenye vyombo vya sheria kwenda kufuata haki hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kushauri vitu viwili; cha kwanza niishauri Serikali. Niiombe Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje semeni juu ya haya mambo, tusiache watu wakachafua nchi yetu. Mheshimiwa Kabudi ameenda Geneva, ametoa taarifa nzuri na amesifiwa lakini huku ndani watu hawajui.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili nataka kushauri, kwa kuwa tunayo legal na institutional framework ya namna ya ku-deal na mambo ya haki za binadamu, niwashauri wenzangu, Watanzania wote twende kwa namna hiyo, tuache kuzunguka kwenye maofisi huko mara kwenye Mabalozi, tunao utaratibu wa kisheria na kikatiba wa namna ya ku-deal na vitu vya namna hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumze jambo la pili kwenye diplomasia ya uchumi. Diplomasia ya uchumi ni dhana pana na inawezekana tunapata shida sana kuielewa, niwapongeze sana Mabalozi wa nchi yetu ambao wanatuwakilisha kule nchi. Balozi wetu wa China, Balozi wa Urusi wanafanya kazi kubwa, matokeo tunayoyaona kwenye utalii sasa hivi ni matokeo ya kazi kubwa wanayoifanya kwenye diplomasia ya uchumi. Hata kitendo cha Zimbabwe kukubali tupeleke mahindi tani zaidi ya 700,000 kwenye ziara ya Mheshimiwa Rais ni matokeo ya diplomasia ya kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wasichoelewa ni kitu kimoja, Sera yetu ya Mambo ya Nje, Toleo la Mwaka 2001 imejisimika kwenye diplomasia ya uchumi, lakini haina maana kwamba kwa sababu ya diplomasia ya kiuchumi tumeacha vitu vingine na hata sera ile imesisitiza kwamba tunaendelea kuimarisha misingi na kanuni za sera yetu ya asili ile ya mwanzo ambayo ilitokana na Serikali ya Awamu ya Kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, miongoni mwa kanuni za kwenye Sera yetu ya asili ya Mambo ya Nchi za Nje pamoja na kwamba ilikuwa ni kwa ajili ya kuangalia ukombozi wa nchi nyingine, ilikuwa ni kulinda uhuru wa Taifa hili. Kuja kwa sheria za kwenye Sekta ya Madini, mabadiliko tuliyoyafanya ni ishara ya kulinda uhuru wa Taifa kwenda kutafsiri diplomasia ya uchumi ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niishauri tu Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje iendelee kutoa ushirikiano mkubwa kwenye mikataba na Mataifa mengine, kwenye mikataba ya wawekezaji ili katika kufanyia kazi mambo hayo, tujitahidi kuhakikisha kwamba na zile dhana zote zinazohusiana na mambo ya diplomasia na uhusiano wa mambo ya nje zinazingatiwa vizuri kwa kuondoa mikwaruzano na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze sana Serikali, tangu 2015 mpaka sasa tumeanzisha Balozi zaidi ya saba, mpaka juzi tumeanzisha Balozi nyingine ya Cuba. Kukubaliwa kuanzisha balozi kwenye nchi nyingine, yenyewe ni ishara kwamba tuna mahusiano mazuri na nchi nyingine. Hii dhana inayojengwa kwamba tuna mahusiano mabaya, watu wanatupotosha. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe sana Serikali, waendelee kusimamia mahusiano na nchi nyingine, waendelee kusimamia diplomasia ya Tanzania kwenye Mataifa mengine. Sisi tunamwamini Mheshimiwa Profesa Kabudi, Mheshimiwa Dkt. Ndumbaro na tunamwamini Mheshimiwa Rais, wafanye kazi kwa niaba ya Watanzania, nchi yetu ipate sura nzuri mbele ya ulimwengu na dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)