Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Spika, naomba kuchangia Wizara hii muhimu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusu umeme wa REA III Jimbo la Mikumi. Ninatambua kuwa mkandarasi wa REA III katika Jimbo la Mikumi ni State Grid lakini bado kazi ya kuleta umeme kwenye Jimbo la Mikumi inasuasua sana.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano Kijiji cha Udung’u kilichopo katika Kata ya Vidunda ambacho kipo kwenye mpango huu; na awamu hii mkandarasi ameshindwa hata kwenda kufanya survey na hakuna shughuli yoyote iliyofanyiwa kazi. Tunaomba kujua, ni lini wananchi hawa watapelekewa huduma hii muhimu?

Mheshimiwa Spika, Kijiji cha Vidunda bado hakijafanikiwa kwa namna yoyote ile, hata nguzo bado hazijapelekwa; wananchi wanataka kujua tatizo ni nini? Maana walinisikia nikiuliza swali Bungeni na walimsikia Naibu Waziri Mheshimiwa Subira Mgalu akiwahakikishia kuwa nguzo zipo.

Mheshimiwa Spika, Kata ya Ulaya. Mheshimiwa Waziri amekuwa akituahidi mara kwa mara kwamba Kata hii ya Ulaya itafikiwa, na alifanya ziara kwenye kata hii na akatembelea na Kituo muhimu cha Afya cha Ulaya ambacho hakina umeme na kinahudumia Tarafa nzima ya Ulaya yenye Kata za Ulaya, Mhenda na Zombo. Hata hivyo mpaka leo hii hakuna shughuli yoyote inayohusu umeme inayoendelea katika Kata hii muhimu ya Ulaya.

Mheshimiwa Spika, Kuhusu Kata ya Tindiga. Kwenye Kata ya Tindiga hakuna shughuli yoyote inayohusu umeme inayoendelea ingawa nayo ipo kwenye mpango wa REA III, kwenye awamu hii; Kata ya Tindiga ina Vijiji vya Tindiga A, Tindiga B, Malui, Kalukwambe na Malangali. Tunaomba kujua, ni lini kata hii na vijiji vyake vitapatiwa umeme?

Mheshimiwa Spika, Kata ya Zombo. Nguzo zimeanza kushushwa katika Kata ya Zombo lakini zoezi hili bado linasuasua na Serikali ilituambia itaunganisha umeme huu kutoka Kata ya Masanze kwenye Kijiji cha Changarawe. Kata ya Zombo ina vijiji vitano, ambavyo ni; Zombo Lumbo, Kigunga, Nyameni, Nyali na Madudumizi. Je, ni lini sasa Serikali itatuletea umeme kwenye vijiji hivi?

Mheshimiwa Spika, Kuhusu Kata ya Mhenda. Kata ya Mhenda ipo katikati ya Kata ya Mikumi maeneo ya Ihombwe na Kata ya Ulaya. Sasa tunaomba sana Serikali itusaidie kutuletea umeme kwenye Kata hii muhimu ya Mhenda yenye vijiji vya Mhenda, Ilakala, Nyaranda na Maili 60. Tunaomba sana Serikali itusaidie tupate umeme kwa wakati kama walivyotuahidi.

Mheshimiwa Spika, Kijiji cha Chonwe. Kijiji hiki kipo katika Kata ya Vidunda na kipo kwenye mpango huu wa REA III awamu ya kwanza, lakini mpaka leo hakuna jitihada zozote zilizooneshwa na Serikali na mkandarasi hajawahi hata kufika.

Mheshimiwa Spika, Kata ya Mikumi. Ikumbukwe kuwa Mikumi ni Jimbo la Kitaliii na kwenye Kata ya Mikumi kumekuwa na uwekezaji mkubwa sana wa hoteli za kitalii na camp sites. Pamoja na hayo, kwenye Kata ya Mikumi, katika hali ya kustaajabisha na kusikitisha maeneo ambayo yana uwekezaji wa hoteli za kitalii hayana umeme. Maeneo haya ni; Kikwalaza na maeneo ya Tambukareli ambako kuna Mji Mpya wa Kiserikali wa Mikumi. Kwenye maeneo ya Kikwalaza wenye hoteli wanalalamika sana kwamba wanapata gharama kubwa sana za kuendesha hoteli zao kwa kukosa umeme, kiasi kwamba inawalazimu kutumia majenereta makubwa sana, kitu ambacho kinawagharimu sana kwenye uendeshaji wa hoteli zao.

Mheshimiwa Spika, maeneo ya Tambukareli kuna maeneo ambayo leo watu wa TANESCO – Mikumi wamekuwa kimya na wamesababisha wananchi kushikwa na butwaa. Sasa wananchi wanataka kujua; Serikali ilipojibu swali langu Bungeni waliahidi kwamba kwa kuwa kuna shughuli za kitalii na zinaongeza Pato la Taifa letu basi wangetoa kipaumbele kwenye Kata hii ya Mikumi na maeneo yake haya ya Kikwalaza na Tambukareli. Je, ni lini tutapatiwa umeme kwenye maeneo sambamba na maeneo ya Barabara Kuu ya Tanzania kwenda Zambia, hasa maeneo ya Msimba na Ng’apa?

Mheshimiwa Spika, Kuhusu Umeme Jazilizi (Densifications). Maeneo ya Ruaha Mbuyuni, Malolo A, Malolo B. Mgogozi na Chabi yaliyoko kwenye Kata ya Malolo yamepitiwa na nguzo za umeme uliopo karibu. Nilishawahi kuuliza swali na Mheshimiwa Waziri alinijibu kuwa kuna pesa zimepatikana kutoka kwa wahisani na kwamba maeneo haya pamoja na maeneo ya PWD, Dodoma, Kipekenya, Dodoma Isanga, Munisagala na Chabima yaliyopo kwenye Kata ya Masanze na maeneo ya Gezaulole, Mbamba, Kiduhi vilivyopo kwenye Kata ya Kilangali; je, ni lini wataunganishwa na umeme?

Mheshimiwa Spika, Kata ya Uling’ombe. Hii ni kata ambayo ni muhimu sana kwa kilimo na madini na inapakana na Jimbo la Kibakwe ambalo lina umeme. Tunaiomba sana Serikali itupatie umeme kwenye Kata hii muhimu yenye vijiji vya Uleling’ombe, Mlunga, Ibanda na Lugawilo ili nishati hii ikatumike kukuza uchumi wa wananchi wa maeneo haya kwa kuchakata mazao na shughuli za madini.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.