Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, nachukua fursa hii kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Mheshimiwa Dkt. John Joseph Magufuli Rais kwa jinsi anavyoiongoza nchi yetu. Hata hivyo, Watanzania wanakiri kuwa Mheshimiwa Rais amechelewa kupokea uongozi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Dkt. Medard Matogolo Kalemani Waziri wa Nishati, Naibu Waziri na waandamizi wake kwa jinsi wanavyotumikia nafasi zao. Aidha, tunawaombea utume mwema katika kutimiza majukumu yao kwa Taifa la Tanzania.

Mheshimiwa Spika, nimesikitika kukosa nafasi ya kuchangia bajeti ya Wizara hii. Hoja yangu ni kutaka Mheshimiwa Waziri wakati wa kutupa hitimisho lake atuambie ni lini mradi wa REA III utafikisha umeme katika Makao Makuu ya Kata za Gunyoda, Muray, Silaloda, Gunyoda kwa kuwa mradi wa REA awamu ya kwanza ulifika Mbulu 2007 mpaka leo kuna vijiji 38 na kata tano ambazo bado line kubwa haijafika ukiacha vijiji vingi ambavyo umeme umepita bila kufika kwenye vitongoji.

Mheshimiwa Spika, naomba uchunguzi wa kina ufanyike katika mradi wa umeme wa REA 1 – II – III kuhusu idadi ya nguzo zilizopelekwa kwani wananchi wanalalamika kuwa ni nguzo nyingi zinazoletwa katika halmashauri ya mji wakati huo mradi hauendi wala kusambaa.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Kalemani alitoa ahadi ya kupeleka umeme katika Kata ya Muray toka mwaka 2016 akiwa Naibu Waziri mpaka leo umeme haujafika. Hivyo tunaelekea uchaguzi, kauli ya Mheshimiwa Waziri ni kauli ya Mheshimiwa Rais, hivyo basi, naomba kauli ya Serikali vinginevyo nitashika shilingi ni lini umeme wa line kubwa utafika kwenye Kata za Muray, Gunyoda, Silaloda na Soheda kupitia Mradi wa REA III katika Jimbo la Mbulu Mjini.

Mheshimiwa Spika, la pili, Serikali ina mkakati gani wa kusambaza chombo cha Umeme Tayari (UMETA) ili kupunguza gharama kubwa ya nguzo, waya na kazi zingine katika maeneo ya vijijini kwani mahitaji ya umeme katika kaya za vijijini ni taa, kuchaji simu hivyo chombo hiki ni muhimu sana

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa maeneo mengi ya REA awamu ya I – II – III yamerukwa katika Jimbo la Mbulu Mjini na kwa kuwa kuna shule nyingi za msingi, sekondari, Makanisa yaliyoachwa toka 2008. Nashauri ziara za viongozi wetu hususan Mawaziri inapotokea basi wawasiliane na Waheshimiwa Wabunge badala ya TANESCO kupanga ratiba ya ziara hizo ili Mbunge naye atoe ushauri wake kumsaidia Waziri.

Mheshimiwa Spika, kwa masikitiko makubwa Mheshimiwa Waziri wa Nishati Mheshimiwa Medard Kalemani alikuja kuzindua Mradi wa Umeme wa REA Jimbo la Mbulu Mjini katika Kata ya Ayomohe 2018 mwezi Mei lakini mpaka leo hakuna majengo yaliyosambaziwa hali hii imewapa mshangao wananchi wa Kata ya Ayamohe, naomba Waziri afanye tena ziara mapema mwaka huu ili kuleta msukumo.

Mheshimiwa Spika, mwisho, nachukua nafasi hii kuwaombea watumishi wetu wa TANESCO Mkoa na Wilaya ya Mbulu waliotangulia mbele za haki Mwenyezi Mungu awapokee katika ufalme wake usio na mwisho. Aidha, naomba Wizara iwateue watendaji wa nafasi hizo ili kuimarisha utendaji.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naomba kuwasilisha.