Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, naomba nianze mchango kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha leo kushika kalamu na kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii. Kwanza kabisa nianze kwa kuwapongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi wanayoifanya kwenye Wizara hii, wao pamoja na watumishi wote kwenye Wizara hii kwa juhudi kubwa wanazofanya za kuwaletea maendeleo katika Sekta hii ya Nishati hasa ya umeme. Wananchi wanaona juhudi yao katika kuwatumikia Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Mradi wa LNG Lindi; naiomba na kuishauri Serikali kuharakisha mazungumzo juu ya utekelezaji wa mradi huu muhimu kwa nchi yetu. Hata hivyo, katika kuharakisha huko hakuondoi umakini wa kuzingatia maslahi mapana kwa Taifa letu na rasilimali ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, REA awamu ya tatu kwa Mkoa wa Lindi haijafanya vizuri kwani hadi leo vijiji vingi vya Mkoa wa Lindi havijafanikiwa. Mfano Wilaya ya Liwale yenye vijiji 76, katika awamu ya tatu kulikuwa na vijiji 14, ni vijiji vitatu tu hadi leo vimewashwa umeme. Sasa awamu ya tatu, mzunguko wa pili imeanza kutekelezwa kwenye baadhi ya mikoa, Liwale bado tuko awamu ya tatu, mzunguko wa kwanza ambayo hakuna chochote kinachofanyika, japo REA awamu ya pili nayo haikufanya vizuri kwani hadi leo zipo taasisi hazijapata umeme kama vile shule, zahanati na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, naiomba Serikali kumbadilisha mkandarasi wa Mkoa wa Lindi ambaye ameshindwa kwenda na mkataba. Serikali kushindwa kumbadilisha mkandarasi huyu ni kukiri madai ya mkandarasi huyu kuwa Serikali haitoi fedha, ndiyo maana anashindwa kufanya kazi. Je, ni kweli kuwa Serikali haina fedha za kumlipa mkandarasi huyu?

Mheshimiwa Spika, sambamba na mradi wa LNG – Lindi, naomba kuishauri Wizara kushirikiana na Wizara ya Elimu kukiwezesha Chuo cha VETA Lindi kuanzisha masomo yanayohusiana na masuala ya gesi ili kuwawezesha wakazi au vijana wa Mikoa ya Lindi na Mtwara kushiriki vyema kwenye tasnia hii ya gesi.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hilo, naiomba Serikali kutoa kipaumbele kwa vijana wa Mikoa ya Lindi na Mtwara, pale inapotokea nafasi kuwawezesha Watanzania kushiriki katika tasnia ya gesi, yaani kimasomo ndani na nje ya nchi ili Wanalindi waweze kuona manufaa ya moja kwa moja kutokana na kugunduliwa kwa gesi katika mikoa hiyo.

Mheshimiwa Spika, mradi wa matumizi ya gesi majumbani ni muhimu sana kwani utasaidia kupunguza kwa kiasi kikubwa uharibifu wa mazingira. Pia wananchi wataona moja kwa moja manufaa ya kuwepo kwa gesi hiyo. Mradi wa matumizi ya gesi majumbani kwa Mkoa wa Lindi bado kabisa haujaanza. Kwa hiyo nashauri kufikiria kuanza kwa mradi huu kwa Mkoa wa Lindi.

Mheshimiwa Spika, ninaposema Mkoa wa Lindi naiomba Serikali itambue kuwa Liwale ni miongoni mwa Wilaya za Mkoa wa Lindi hivyo miradi hii inaporatibiwa wakumbuke na Liwale, hata wakandarasi nao wafahamishwe kuwa Liwale nayo iko Lindi. Mfano Kampuni za Shell na Equinor zimeanza kutoa huduma (incentives) kwa Mikoa ya Lindi na Mtwara, lakini Wilaya ya Liwale hawana habari nayo, kana kwamba Liwale haiko Lindi.

Mheshimiwa Spika, naendelea kuishauri Serikali kuendelea kuwekeza kupitia Kampuni ya TPDC kwani sasa kampuni hii haijawezeshwa vya kutosha kuweza kukidhi majukumu yake. Miradi mingi ya kampuni hii imeshindwa kufanya vizuri kutokana na ukosefu wa fedha. TPDC ni lazima ipewe fedha za kutosha.

Mheshimiwa Spika, Liwale nayo iko Mkoa wa Lindi, nayasema haya kwa kuwa Mawaziri wengi huishia Wilaya za Kilwa, Nachingwea, Ruangwa na Lindi na kusema kuwa wamemaliza ziara ya Mkoa wa Lindi. Jambo hili limewafanya hata wakandarasi kuacha kutekeleza miradi mbalimbali kwani wanajua kuwa haitakaguliwa na Waheshimiwa Mawaziri, hakuna Waziri anayekuja Liwale kukagua miradi ya maendeleo ikiwemo REA. Hivyo, namwomba Mheshimiwa Waziri wa Nishati aje Liwale aone haya ninayoyasema. Kati ya vijiji 76, vijiji vyenye umeme havifiki hata 15, hali ni mbaya sana.

Mheshimiwa Spika, mwisho, naiomba Wizara wawaruhusu wawekezaji wa umeme jua, Kampuni ya Power Conner, waweze kutuletea umeme sisi tulio pembezoni tusioweza kufikiwa na umeme wa REA.