Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

Hon. Jerome Dismas Bwanausi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kupata nafasi ya kuchangia, kwenye bajeti hii ya Wizara ya Nishati, nianze pia kwa kumpongeza Waziri wa Nishati na Naibu wake kwa kazi kubwa wanayoifanya katika Wizara hii. Waziri na Naibu wake wamekuwa wakizunguka nchi nzima na ziara zao zimekuwa na tija kwa kiasi kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende moja kwa moja kwenye Jimbo langu kwanza, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri hivi karibuni amefanya ziara katika Jimbo langu la Lulindi kule Wilayani Masasi ziara ambayo imeleta matumaini mapya kwa wakazi wa Jimbo la Lulindi. Lakini nimuombe tu Mheshimiwa Waziri kuweka msisitizo kwa yale aliyoyasema alipokuwa Jimboni Lulindi na hasa pale alipotoa maelekezo kwamba vijiji vile takriban tisa ambavyo viko katika Jimbo langu ambavyo vimepitiwa na umeme kwa miaka mingi lakini havijashushwa TANESCO uliwaagiza wafanye hiyo kazi katika vijiji hivyo vya Dagaga, Mkangaula, Mpita, Guluni, Maugura na vijiji vile vingine vyote ambavyo uliviainisha vikiwemo na cha Chanika ili kuhakikisha kwamba vijiji hivyo vipatiwe umeme haraka iwezekanavyo. (Makofi)

Lakini pia nikumekupongeza sana Mheshimiwa Waziri, kwa jinsi ulivyotoa maelekezo kwamba maeneo ambayo tayari yana umeme, yasisubiri tena mpango mwingine wa REA hakikisheni wananchi lipeni walipie ili nguzo Serikali iwapelekee kwa kweli huu ni mpango mzuri na tunaupongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naushauri Mheshimiwa Waziri, kuhusiana na usambazaji wa umeme vijijini tunalo tatizo kubwa sana kwamba tunatakuwa kuwa na vijiji vingi sana tunavigusa lakini matokeo yake wakandarasi wanakwenda kuweka umeme katika kijiji robo tu ya kijiji na eneo lingine linabaki. Hili jambo linatuletea mgogoro mkubwa sana tunategemea kwenye REA awamu ya tatu mzunguko wa pili hili jambo liangaliwe sana kama tunakwenda kwenye kijiji tuhakikishe kijiji chote kinapewa umeme badala ya kuwekewa katika eneo dogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia suala la kuruka vijiji, kijiji kimoja kinapata kingine kinarukwa kingine hakipati hili jambo Mheshimiwa Waziri umelisisitiza sana lakini wakandarasi wamekuwa hawatekelezi kama vile unavyowaagiza.

Mheshimiwa Spika, lakini mwisho nimemsikia dada angu Mheshimiwa Peneza kuhusiana na mradi wa Rufiji mimi nilikuwa nadhani ingekuwa busara kwa sasa kwa upande wa wenzangu kule ndugu zangu kutouzungumzia sana juu ya kana kwamba huu mradi usitekelezwe Serikali imekwishaamua na katika ukurasa wa 23 wa hotuba ya Rais…

SPIKA: Mheshimiwa Upendo unaelimishwa huku!

MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Upendo nilikuwa nasema kwamba hivi sasa si vizuri sana kupoteza nguvu kubwa sana kujadili jinsi gani huu mradi utatekelezwa Serikali imekwisha dhamiria, imeshasema haiyumbishi na utatekeleza kwa wakati na historia jinsi mnavyoona sasa Serikali ya Awamu ya Tano ya Dkt John Pombe Magufuli inatekeleza kwa wakati miradi yake yote. Kwa hiyo, huu mradi hauyumbishwi na mtu wa ndani wala wa nje kutokana na hotuba ya Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)