Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru sana kupata nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii ya Nishati.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote niipongeze Serikali kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya ya kupeleka huduma ya Nishati hasa kwenye miradi ya REA ambayo kila eneo katika nchi yetu imeweza kufanyika. Nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri kwa jitihada kubwa na juhudi ambazo amezifanya kwenye maeneo mbalimbali ikiwemo Jimbo la kwangu amefika zaidi ya mara tatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri ameenda kijiji cha Kasekese, alipata mapokezi mazuri, makubwa lakini amefanya jitihada za makusudi kusukuma umeme kwenye vijiji vya Majalila, Kijiji cha Ifukutwa, Kijiji cha Kabungu na kwenye eneo la Gereza la Kilimo Kalilangurukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi letu sisi wananchi wa Mkoa wa Katavi, Kigoma na Rukwa hatuna umeme wa grid ya taifa, umeme huu ndiyo umeme ambao utakuwa suluhisho la kudumu kwenye maeneo mbalimbali ya mikoa hii mitatu na mr adi wa grid ya taifa ni wa muda mrefu toka mwaka 2010 ulianza kuzungumzwa kwenye vitabu mbalimbali vya Wizara. Niwaombe sasa kuwe na jitihada za maksudi ule umeme wa kilovolt 400 ambao tunategemea utoke Tunduma hadi Nyakanazi Mkoa wa Kigoma. Uwekwe kwenye mpango ambao na msukumo mkubwa ili uweze kutekelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, umeme huu utawasaidia wananchi wa Mikoa ya Rukwa, Katavi na Kigoma. Tuombe sana Serikali ipeleke fedha kwa ajili ya kuanza mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, umeme wa REA phase III. Tunapongeza jitihada za Serikali zilizofanyika lakini kasi ya wakandarasi waliopewa nafasi ya kuandaa miundombinu ya umeme wa REA III bado si ya kuridhisha. Pamoja na jitihada nzuri zinazofanywa na Wizara lakini bado uhitaji wa miradi hii kutekelezwa kwa wakati ni mkubwa sana. Nikuombe Mheshimiwa Waziri, umeenda pale Kijiji cha Mchakamchaka umezindua umeme, lakini baada ya kuondoka jitihada zile ambazo zilikuwa zinahitajika kusukuma ili miradi iweze kwenda kwa haraka bado hazijafanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimkumbushe Mheshimiwa Waziri alipofika eneo la Kasekese na alipofika Ifukutwa aliwaahidi wananchi wa Wilaya ya Tanganyika kwamba vijiji vyote vitapata umeme wa REA phase III. Niombe sana eneo la Mishamo na vijiji vyote vilivyoko kwenye eneo hilo naomba upeleke umeme na mkandarasi umuagize ahakikishe vile vijiji vinapata umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, liko eneo la ukanda wa ziwa...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa, kengele imeshagonga, ahsante sana.

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.