Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Madini

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Madini

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba hii mbele yetu. Nampongeza sana Mheshimiwa Waziri Biteko, Naibu Waziri, Mheshimiwa Haroon Nyongo (Mb), Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri na kubwa wanayofanya.

Mheshimiwa Spika, nchi yetu ina madini, vito na rasilimali nyingi za madini ya thamani na yasiyo na thamani lakini kwa umasikini uliopo hata maeneo yanayotoka madini au rasilimali hizi haziakisi utajiri huo. Hii inatokana zaidi na utekelezaji wa sheria na kanuni zetu katika kuwezesha mali hii kulisaidia taifa. Hatuna rafiki wa wazalishaji wa sekta hii kwa jinsi tunavyowanyanyasa kwa lugha, vitisho, kodi na tozo.

Mheshimiwa Spika, Mradi wa Makaa ya Mawe Kiwira na Kabulo. Mgodi wa Makaa ya Mawe wa Kiwira umesima kwa zaidi ya miaka tisa sasa. Mwaka 2018 uchimbaji ulianza kidogo katika mgodi wa Makaa ya Mawe wa Kabulo; tangu wakati huo hatujapata taarifa yoyote mpya ya mendeleo ya migodi hii miwili. Hotuba ya Waziri wa Madini ukurasa wa 53 una-report kuwa STAMICO wamechimba tani 22,119 za makaa ya mawe na kuuza tani 7,664.8 tu.

Mheshimiwa Spika, lakini taarifa hii ni ileile tuliyopewa kwenye hotuba mwaka jana. Ina maana hatuna maendeleo yoyote yaliyofanyika tangu Aprili, 2018? Serikali itufahamishe ina mpango gani wa kufufua mgodi wa Kiwira na kuendeleza mgodi wa Kabulo. Tangu mgodi wa Kiwira usitishe chini ya Tanpower Resources Company Limited kumekuwa na sintofahamu ya nani muhusika mkuu wa mgodi huu baada ya kuondolewa kwa muwekezaji huyu aliyekabidhiwa mgodi tangu mwaka 2005; waliopewa silimia 70 ya hisa na Serikali kubaki na silimia 30.

Mheshimiwa Spika, tangu mgodi kurudishwa Serikalini mwaka 2009, NSSF walilipa madeni ya mgodi shilingi bilioni 28.72, Benki ya CRDB nayo ina deni, PPF, NSSF wanaudai mgodi Dola milioni saba. NSSF ilitaka kuchukua mgodi huo na kuuendesha na kulipa madeni yote. Hii ingewezekana kwa sababu mgodi una mali nyingi zaidi ya madeni.

Mheshimiwa Spika, mgodi wa Kiwira ulilenga kutumia Makaa ya Mawe kuzalisha umeme na kuuza TANESCO. Mgodi huu ulikuwa unatoa ajira 7000 kwa wananchi wa Ileje kwa uchache lakini kwa kiasi kikuba na Kyela na Rungwe. Mgodi ulikuwa unawezesha Halmashauri kupata mapato na vilevile kuchangamsha uchumi kupitia biashara na ajira zinazounganisha watoa huduma kwenye mgodi. Vilevile kwa familia za watumishi wa mgodi wanaonufaika na mgodi. Sasa hivi kusimama kwa mgodi huu kumezorotesha uchumi wa Ileje na wilaya za jirani kwa zaidi ya miaka tisa sasa na hivyo ni athari hasi sana kwa wilaya yenye rasilimali muhimu na kubwa kama mgodi huu wa makaa ya mawe.

Mheshimiwa Spika, aidha, huu mgodi huzalisha umeme; hii pia imeleta athari kwasababu maeneo haya yamekosa hii connection. Katika bajeti ya Wizara ya TAMISEMI ilitengwa bajeti ya kujenga daraja kwenye Mto Mwalisi linalounganisha mgodi wa Kiwira na Ileje. Je, hiyo fedha itatolewa lini ili kurahisisha usafirishaji wa makaa ya mawe?

Mheshimiwa Spika, Wana Ileje tunaomba sana Mgodi wa Kiwira na wenyewe uanze kazi; na vilevile na ule wa Kabulo uendelee kwa kasi zaidi kwa kutafuta masoko zaidi kwa mwe yanayochimbwa.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.