Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa fursa hii, na nianze kwanza kwa kukushukuru wewe mwenyewe Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimshukuru sana Mheshimiwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wenyeviti wote, na mahsusi Mwenyekiti Mheshimiwa Mussa Azzan Zungu ambaye, ninyi nyote kwa pamoja mmeshiriki katika kutuongoza vizuri katika mjadala huu wa Bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii. Pia kipekee niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote kwa kujadili hotuba ya Wizara yetu ya Maliasili na Utalii kwa mwaka wa fedha 2019/2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, ninamshukuru sana Mheshimiwa Kemilembe Julius Lwota, Mbunge ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa kuchambua na kujadili utekelezaji wa bajeti ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2019/2020; lakini pia, kwa kutoa maoni kuhusu makadirio na mapato ya matumizi kwa mwaka wa fedha wa 2018/2019. Vilevile ninamshukuru Mheshimiwa Mchungaji Peter Simon Msigwa Mbunge, na Naibu wake Mheshimiwa Catherine Ruge, ambao ni wasemaji kwa upande wa Wizara ya Maliasili na Utalii kutoka Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninawashukuru pia, Waheshimiwa Wabunge wote kwa namna ya kipekee kwa kutoa michango mbalimbali ya kuongea hapa Bungeni lakini pia michango ya maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara imepokea na kuchambua michango kutoka Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni na Waheshimiwa Wabunge. Jumla ya Waheshimiwa Wabunge 68 kwa ujumla wao, wamechangia ambapo 36 wamechangia kwa kuongea hapa Bungeni na 32 wamechangia kwa maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuwahakikishia kuwa maoni na ushauri wote uliotolewa na Wabunge utazingatiwa kwa dhati kabisa katika utekelezaji wa majukumu ya Wizara yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, zimetolewa hoja nyingi mbalimbali na kwa faida ya muda naomba nisizirudie, lakini ninaomba nitoe ufafanuzi kwenye maeneo machache, na ninaomba Waheshimiwa Wabunge waniruhusu nifanye hivyo kwa faida ya muda.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hoja zote zilizotolewa hapa, hoja ambayo tunaona tuipe uzito sana katika kuitolea ufafanuzi kwa sababu inagusa maeneo mengi ya Waheshimiwa Wabunge, lakini pia wananchi kwa ujumla wake ni hoja ya nigogoro ya mipaka baina ya mamlaka za maeneo mbalimbali yaliyohifadhiwa na wananchi wanaozunguka maeneo hayo. Ushauri umetolewa, maombi yametolewa na Waheshimiwa Wabunge kwamba pengine ile Kamati ambayo Mheshimiwa Rais aliyoiunda Januari 15 mwaka 2019, baada ya kukamilisha kazi yake inge-share ripoti ya kazi hiyo na Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, ufafanuzi pamoja na kwamba Mheshimiwa Waziri Mkuu aliutoa hapa juzi, na naona pia jana imejitokeza na leo imejitokeza, naomba tu niwape comfort Waheshimiwa Wabunge kwamba mchakato huu kwanza, kama alivyosema Mheshimiwa Waziri Mkuu, uliagizwa na Mamlaka ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na hivyo kazi tuliyotumwa mimi pamoja na Mawaziri wenzangu wengine saba ilikamilika na tumeshawasilisha ripoti kwa aliyetutuma, na ndio utaratibu wa kiutendaji. Sasa Mheshimiwa Rais atashauriwa na Baraza lake la Mawaziri na hatua zitakapo anza kuelekezwa kwamba zichukuliwe ni wazi Waheshimiwa Wabunge watapata mrejesho. Hata hivyo niwatoe hofu kwamba tumefanya sample ndogo ya maeneo wamezungumza Waheshimiwa Wabunge wengi, kwa sababu nafahamu wengi wangetamani tufike kila eneo ndipo waone kwamba tunashughulikia migogoro ya maeneo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Naomba niwape comfort Waheshimiwa Wabunge kwamba kazi iliyofanyika imefanyika kwa kikamilifu na ni kazi ambayo ilipewa uzito mkubwa sana na Serikali na si kazi ambayo ilianza Januari 15, kuna kazi nyingine zilishafanyika huko nyuma. Kuna Tume mbalimbali zilishaundwa, tumechambua taarifa zote hizo lakini tukaona haitoshi tukaona pia tuchukue maoni kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge na tukapata maoni yenu, mapendekezo yenu na maombi sehemu nyingine na yote haya, tumeyafanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia tukaona haitoshi tukawaita Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya, Makatibu Tawala wa Mikoa, wa Wilaya, Wakurugenzi wote wa halmashauri zote hapa nchini wakaja pia wakazungumza na Kamati yetu, nao wakatuelezea migogoro mingine ambayo ipo katika maeneo yao na yote hiyo tumeifanyia kazi na kimsingi kuna migogoro ambayo mahsusi tumeipatia mapendekezo kadhaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo kwenye maeneo mengi zaidi, tumeweka tu principle ambayo itatumika kufanya maamuzi tunavyoelekea mbele. Kwa hivyo hata kama mgogoro haukuwepo katika migogoro ambayo tumeipitia, na hiyo itakuwa ni bahati mbaya sana, basi itaguswa na hiyo principle ambayo tutaitumia katika kufanya utekelezaji; na hii sasa, ni mpaka pale ambapo Mheshimiwa Rais atakubaliana na mapendekezo ambayo tumeyapeleka.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini walau linaloleta faraja kubwa kwa Waheshimiwa Wabunge na kwa wananchi ni jambo moja, na hili ni spirit ya Mheshimiwa Rais. Azma ya Mheshimiwa Rais ilikuwa ni kupunguza manung’uniko, kero na migogoro kwa upande wa wananchi kuliko hata kwa upande wa hifadhi; japokuwa aliweka angalizo kwamba tuhakikishe tunalinda hifadhi hizi, tuhakikishe pia tunalinda ikolojia hizi ambazo tunazo kwa namna yoyote ile. Kwamba tutatue migogoro lakini tuhakikishe pia uhifadhi unaendelea na shughuli za utalii zinaongezewa tija. Kwa hivyo mambo yote yamezingatiwa katika uchambuzi wetu na mapendekezo yako vizuri. Kwa hivyo comfort iliyopo ni kwamba kwenye maeneo yale yenye kero, kwa kweli spirit na muongozo wa Mheshimiwa Rais ulikuwa ni kwamba wananchi wapate ahueni; na hilo ndilo tulilolizingatia katika mapendekezo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa kuwa bado kazi ni mbichi naomba niishie hapo nisije nikajikuta naanza kuelezea baadhi ya migogoro ilhali hatujapewa muongozo na aliyetutuma; lakini walau muwe mna-comfort hiyo kwamba migogoro baada ya mapendekezo haya kupitishwa na Mheshimiwa Rais pengine tutaipunguza kwa kiasi kikubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Maelekezo mengine yote ya ushirikishwaji wa wananchi tunayapokea kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge na ndivyo ambavyo tumekuwa tukifanya; labda tutaweka msisitizo zaidi kwamba wananchi washirikishwe kwa kiasi kikubwa katika kupitia mipaka na katika zoezi zima la kuweka vigingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna maelezo pia ambayo yalitolewa kwenye ripoti ya Kamati, lakini pia Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, pia Mheshimiwa Sakaya, Mheshimiwa Catherine Magige, Mheshimiwa Yussuph Hussein pia alizungumzia leo na Waheshimiwa wengine wamezungumzia eneo la Ngorongoro. Naomba hapa nielezee tu kwamba, eneo hili ni katika maeneo ya urithi wa dunia ambao unatambulika na UNESCO. Pia ni eneo nyeti kidogo kiuhifadhi ma unyeti wake kwa kiasi kikubwa unajengwa na msingi kwamba ni eneo pekee ambalo matumizi mseto ya ardhi yanaruhusiwa kwamba kuna matumizi ya uhifadhi wa wanyamapori katika eneo hilo lakini pia shughuli za mwananchi zinaruhusiwa, wananchi wanaishi sambamba na wanyamapori.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na changamoto nyingi ambazo zimejitokeza kutokana na model hii na ukweli unazidi kujibainisha pale ambapo tunaona dhahiri kwamba idadi ya watu toka mwaka 1959 inapotangazwa ambapo walikuwepo 8,000 imeongezeka sana leo hii tuna watu takribani 93,000 katika eneo lile lile. Pia idadi ya mifugo imeongezeka, shughuli za utalii pia zimeongezeka kulikuwa kuna lodge chini ya sita leo hii tunazo lodges zaidi ya 10 katika eneo hilo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo shughuli za utalii zimeongezeka, shughuli za watu zimeongezeka pia wananchi wanaopita katika eneo la Ngorongoro kwenda Serengeti na kwenda Mkoa wa Mara upande wa pili pia wameongezeka. Kwa hivyo kulikuwa kuna haja ya Serikali kwa kweli kukaa chini kutathmini na hatimaye kuja na mapendekezo kwamba nini kifanyike katika eneo hili nyeti sana la kiuhifadhi la Ngorongoro. pia kwa kuzingatia ukweli kwamba per square meter eneo la Ngorongoro ndio hifadhi pekee ambayo inaingiza pesa nyingi zaidi kuliko hifadhi zote Afrika Mashariki na Kati, per square meter. Kwa hivyo, ni eneo fulani ambalo kiuchumi ni muhimu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tumefanya kazi hiyo, niliunda Kamati mimi kama Waziri mwaka jana mwezi Machi, Kamati imetuletea ripoti wiki iliyopita na ina mapendekezo kadhaa. Mapendekezo tunaona yakikubaliwa na wananchi na wadau wote yatakuwa mazuri yatasaidia ku-balance mahitaji ya makundi yote ambayo yanatumia ardhi ya Ngorongoro wakiwemo wananchi pia sisi wahifadhi na shughuli za utalii kwa ujumla wake kwa sababu tunapendekeza na kama Serikali itakubali kwa maana ya kupitia Baraza la Mawaziri, basi sisi tunapendekeza kwamba eneo la Ngorongoro kwa kuwa linazidi kupata athari kubwa ya mazingira ni lazima tuchukue hatua mahususi kama zifuatazo; kwamba katika eneo lile kuna shughuli ambazo zinahusiana na uhifadhi 100%. Eneo kwa mfano la crater, kuna craters tatu pale almost, ya Embakai pamoja na hiyo Ngorongoro Crater ni lazima maeneo haya yalindwe. Pia kuna msitu wa Kaskazini ni lazima eneo hili lilindwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunavyoona sisi pengine matumizi katika maeneo haya nyeti na maeneo mengine ambayo yana wanyamapori wengi kama Ndutu pengine yawe limited kwa ajili ya wanyamapori.

Vilevile tunaona kwamba mle ndani kuna makazi ya wananchi, wananchi wale hawaruhusiwi kulima, hawaruhusiwi kujenga nyumba za kudumu, kwa hivyo maisha yao yanakuwa magumu sana. Ukitaka kujenga shule alizungumza Mheshimiwa Catherine Magige ni mpaka wapate kibali, wakitaka kujenga zahanati ni mpaka wapate kibali, kwa hiyo wanakuwa wanapata adha kubwa sana kuleta maendeleo katika maisha yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi pia tunaona hii si sawa, jamii ya wananchi wa Ngorongoro ina haki kama jamii ya wananchi wa Iringa, jamii ya wananchi wa Moshi, ya kujiendeleza. Hatuwezi kusema jamii hii itabaki kuwa duni toka enzi na enzi mpaka leo tunaona kwamba lazima tuipe fursa pia ya kujiendeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, jamii hii hairuhusiwi kulima katika eneo lile tunalazimika kuwapa chakula kidogo ili kuwasaidia, lakini jamii pia nayo imebadilika sana, leo hii jamii ya Ngorongoro sio wafugaji 100%, kwa kiasi kikubwa pia kuna watu wanahitaji kulima kuna watu wengine mle zaidi ya asilimia 25, hawana ngombe hata mmoja kwa hivyo siyo wafugaji, hawana mfugo hata mmoja, kwa hivyo siyo wafugaji. Je, hawa watu wanaishije, huwezi kusema wanaishi kwa kutegemea maziwa na nyama peke yake, kwa hivyo tumeona tugawe sehemu kadhaa tutengeneze vijiji proper vijiji ambavyo wananchi wataruhusiwa kufanya shughuli zozote zile za uendelezaji, wataruhusiwa kumiliki ardhi, wataruhusiwa kufanya shughuli za kiuchumi nyingine kama sehemu nyingine yoyote ile ya nchi, kwa sababu kwa sasa hivi wanahesabika wako ndani ya hifadhi. Kwa hivyo wamekuwa limited kufanya shughuli kadhaa ambazo zinatambulika na lazima zifanyike kwa kibali maalum. Kwa hivyo, tunaona tutaanzisha sasa vijiji mahususi katika eneo hili ambavyo vitakuwa haviingiliani sana na uhifadhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, tutabakisha maeneo ambayo yatatumika kwa ajili ya shughuli za uhifadhi mseto ambapo wanyapori watapita humo na wananchi wataishi katika maisha yale ya kizamani ya kimila ya kiasili ya kimasai kama ambavyo iko sasa. Kwa hivyo tutaweka maeneo hayo matatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo tunaona kwamba eneo lile bado ni finyu sana ni lazima tu-annex maeneo ya jirani ambayo yana uhifadhi pia yana mila zinazofanana na watu wa pale ili eneo liwe kubwa zaidi ili wananchi tutakapokuwa tunawahamisha kwenye maeneo yale nyeti tuwasogeze pembeni hapo waweze kukaa. Sasa tutaweka mfumo ambao utatoa motisha kwa watu ambao watakubali kuhama wao wenyewe katika eneo moja kwenda eneo linguine, lakini pia tutaweka masharti magumu kwa watu ambao watataka kuendelea kubaki katika eneo hilo. Lengo letu ni kutotumia nguvu katika kuendelea kuhakikisha hifadhi ya eneo la Ngorongoro inabaki kuwa endelevu kwa vizazi na vizazi vinavyokuja.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo napenda kulitolea ufafanuzi ni suala la hifadhi mpya ambazo tumeziongeza kwa Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) na hizi ni yale yaliyokuwa mapori ya akiba matano na ninayo furaha kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba mchakato ambao tuliupitisha hapa Bungeni kwenye Bunge lililopita kupitia azimio la kupandisha hadhi mapori ya akiba haya matano kuwa hifadhi za Taifa umekamilika, Mheshimiwa Rais ameshaandika tangazo kwenye gazeti na muda si mrefu litakuwa liko public.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa mkononi ninayo hati ambayo inatoka kwa Mheshimiwa Rais ambapo akitangaza hifadhi tatu mpya za Taifa ambazo kama Mheshimiwa Bernadetha Kasabago Mushashu alivyopenda tumwambie majina ya hifadhi hizo maana yake anasikiasikia tu. Naomba nimpe taarifa rasmi sasa Mheshimiwa Bernadetha Kasabago Mushashu kwamba Mheshimiwa Rais ameamua kutangaza Hifadhi ya Taifa ya Burigi - Chato National Park, Hifadhi ya Rumanyika - Karagwe National Park na hifadhi ya Taifa ya Ibanda - Kyerwa National Park. Kwa hivyo hizo ndio hifadhi mpya tatu ambazo zinaingia katika orodha ya hifadhi za Taifa na zitakuwa chini ya usimamizi wa Mamlaka ya Hifadhi za Taifa ya Ngorongoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nitamke kwamba Wizara ya Maliasili na Utalii ilianza mchakato wa kuunda mfumo wa kukusanya takwimu na taarifa mbalimbali kutoka kwa watalii wa kielektroniki, pia mfumo wote wa shughuli zilizo chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia wizara yenyewe kama makao makuu lakini pia na taasisi zote zitafanyika kwa njia ya mtandao na tumejenga mfumo mpya kabisa ambao utakuwa mmoja tu na utakuwa chini ya Wizara na taasisi zote watapewa windows kwa ajili ya kufanya shughuli zao ujulikanao kama MNRT Portal.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo huu umeshaanza kutumika kwenye baadhi ya taasisi na taratibu tunaendelea kusambaza kwenye taasisi nyingine na utakapokamilika changamoto ya takwimu itapungua sana na mfumo huu mwisho wa siku utafika mpaka kwa wadau, watu wanaofanya biashara ya tour, wale tour operators, watu wa mahoteli, wote watakuwa na huu mfumo na watafanya kazi zao kwa kutumia mfumo huu wa kielektroniki ambapo utakuwa unaoana na mifumo mingine kwenye taasisi zingine zote ambazo zinahusika na kuwachaji tozo wadau mbalimbali wa utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano, tutakuwa tuna link ya OSHA tutakuwa tuna link ya BRELA, tutakuwa tuna link ya TRA, utaunganishwa na kufungamanishwa na mifumo yote ya Serikali na hivyo itakuwa ni rahisi kulipa tozo, ni rahisi kuletewa invoice na itakuwa ni rahisi kufanya booking na package za wageni wanaokuja katika kampuni yako. Kwa hivyo tunaamini mfumo huu utapunguza kwa kiasi kikubwa sana business process ambazo zinafanywa na taasisi mbalimbali zilizopo chini ya Wizara yetu pamoja na wadau wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Waheshimiwa Wabunge wa kutoka Kusini ambao wanasema hii ndio kusini proper wamezungumzia sana kuhusu mradi wa Regrow kutokuwa na impact kubwa sana katika Mikoa ya Ruvuma, Lindi na Mtwara. Wameongea kwa uchungu sana kuhusu Mji Mkongwe wa Mikindani, Mji Mkongwe wa Kilwa Kisiwani, hifadhi ya Selou kwa upande wa Mkoa wa Lindi nami nawaelewa. Naomba niseme nimechukua concern yao na nitaifanyia kazi kwa ukaribu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuanzia napenda pia niwape taarifa tu kwamba Mji Mkongwe wa Mikindani pia tumeshausajili kwenye urithi wa dunia na kila mwaka tunafanya Tamasha la Mji Mkongwe wa Mikindani, pia Mji Mkongwe wa Kilwa nao tuko katika mchakato wa kuusajili ili nao uwe katika orodha ya miji ambayo ni urithi wa dunia. Pia tuko katika mpango wa kuendeleza utalii wa fukwe na kwa sasa tutaanza na fukwe za Kigamboni na Bagamoyo. Kwa kuanzia tumeshaandika andiko, liko tayari na katika hatua ya pili sasa tutazungumzia fukwe za ukanda huu wa kusini hii ya Lindi na Mtwara.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu fukwe ya Mnazibay tunafahamu fukwe ya Kisiwa cha Mafia ni katika fukwe bora kabisa duniani na zinapendeza kwa kweli madhari yake na hilo halina mjadala, halibishaniwi, ni ukweli usiopingika, lakini tunakwenda kwa awamu. Katika awamu ya kwanza tunaona kwanza tufanye kazi kubwa ya kuwekeza kwenye utalii wa fukwe katika Jiji la Dar es Salaam na hapa tumeangalia sana uwepo wa miundombinu. Ili uwe na product ya utalii ambayo inafanya kazi kimkakati ni lazima uwe karibu na uwanja wa ndege wa Kimataifa. Ili kuwe kuna uwezekano wa zile long-haul flight kufika na kushusha wateja na wateja kufika kwenye kivutio kwa haraka zaidi kuliko kuwa na stop nyingine tena kwamba achukue local flight kwenda kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo, tumeona katika kukuza fursa ambayo inakuja na utalii wa fukwe, utalii wa mikutano na utalii wa meli, tuwekeze kwanza katika Jiji la Dar es Salaam. Huu ni mradi mkubwa sana ukianza huu mradi, dunia nzima itatikisika kwa sababu idadi ya watalii itaongezeka kwa kiasi kikubwa sana. Pia ni concern ya Waheshimiwa Wabunge kwamba tuongeze idadi ya watalii hapa nchini. Utalii wa Tanzania kwa kiasi kikubwa kwa sasa ni utalii unaoendana na mazingira asilia, utalii wa nature, utalii wa wanyamapori kwa kiasi kikubwa zaidi ya asilimia 80 na utalii huu pia umejikita katika circuit moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iliona katika Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano wa mwaka 2016 – 2021, tufanye diversification, tutanue wigo wa vivutio vya utalii ili tutengeneze mazao mengine ya utalii, mojawapo ni hili zao la utalii wa utamaduni ndio maana nazungumzia Mji Mkongwe wa Mikindani, Mji Mkongwe wa Kilwa, Mji wa Bagamoyo na vivutio vingine vya malikale kama vile Isimila, Kalenga na historia ya nchi yetu kupitia Machifu na vitu vingine. Sasa hiyo ni aina moja ya zao la utalii ambalo ni lazima sisi kama Serikali tuwekeze.

Mheshimiwa Naibu Spika, zao lingine kubwa na muhimu la utalii ambalo ni lazima tuwekeze kama tunavyoelekezwa na Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano ambao tuliupitisha hapa Bungeni ni utalii wa fukwe na lingine ni utalii wa mikutano na lingine ni utalii wa maze yaani cruise ship.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa sisi tumeona tuanze kwa Dar es Salaam tuunganishe haya mazao yote kiurahisi zaidi na pale tayari tuna advantage ya uwanja wa ndege wa kimataifa ambao upo pale na sasa hivi unafanyiwa uendelezaji mkubwa na Serikali, ujenzi umevuka asilimia 99. Kwa hivyo muda si mrefu tutakuwa tuna uwanja wa ndege mzuri zaidi, tuna shirika la ndege ambalo linafanya kazi vizuri. Sasa tukiunganisha na vivutio vya fukwe vilivyopo pale Dar es Salaam na vivutio vya utamaduni itakuwa rahisi sana kupata faida na tija ambayo itakuja na hizi product. Kwa hivyo sasa hivi wenzetu wa TPA ambao tuko nao katika uendelezaji wa mradi wa utalii wa cruise ship, utalii wa meli tunajenga gati maalum kwa ajili ya cruise ship tourism na hii itatusaidia sana kuongeza watalii. Kwa tathmini niliyofanya na wataalamu tunaweza tukapata zaidi ya trilioni tatu kwa utalii wa cruise ships.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo utalii wa meli tu peke yake unaweza ukaleta trilioni tatu. Huu utalii tulionao leo unatuletea trilioni sita. Kwa hivyo kwa haraka haraka tu unaona kwamba kama ni matunda yanayoning’inia chini zaidi, lower hanging fruits maana yake cruise ship tourism ni lazima tuwekeze kwa haraka sana. Kwa hivyo, tunawekeza katika eneo hili na tayari tunarudisha uanachama wa nchi yetu katika yale mashirika ya kimataifa yanayohusika na cruise ship tourism ili tuwe katika mikakati ya kupanga, kufanya marketing mapema ili tutakapokamilisha ujenzi wa gati hili maalum kwa ajili ya cruise ships watalii waanze kuingia nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni utalii wa mikutano; utalii huu tukiwekeza vizuri kama ambavyo majirani zetu wamefanya tuna uwezo wa kupata zaidi ya trilioni mbili kutokana na mikutano ambayo itavutiwa hapa nchini. Eneo lingine ni huo utalii wa fukwe ambao kwa ujumla wake tunakusudia kuanzisha eneo maalum la utalii pale Kigamboni na eneo la Bagamoyo ambapo tutajenga kumbi kubwa za mikutano na hapa nazungumzia mikutano ambayo watu zaidi ya 5,000 wanaweza wakaingia na wakafanya mikutano kwa wakati mmoja. Sizungumzii ukumbi kama ule tulionao sasa wa AICC, nazungumzia project kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuko katika hatua za kufanya andiko la mradi huu, hatua ya awali ya utafiti imekamilika, sasa tuna proposal ambayo itakwenda kwa Makatibu Wakuu, baadaye Baraza la Mawaziri na mradi huu ukipitishwa tutaanza kuutekeleza. Uzuri tuna uwezekano mkubwa sana wa kupata fedha kwa ajili ya kutekeleza mradi huu. Huu ni awamu ya kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, awamu ya pili tutakwenda kwenye fukwe za Maziwa pia tutakwenda kwenye fukwe zilizopo Mafia, Kilwa, Mtwara na maeneo ya Tanga mpaka Pangani kuunganisha na hiyo Bagamoyo niliyoisema. Kwa hivyo eneo hili kwa kweli tunalipa kipaumbele cha hali ya juu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine ni hoja ya hoteli zilizokuwa chini ya Shirika la Utalii Tanzania (Tanzania Tourist Corporation) ambalo lilivunjwa na baadaye mahoteli 17 yakauzwa kwenye sekta binafsi. Katika hoteli hizi kuna hoteli, nilipoteuliwa kwa kweli nilipewa maelekezo ya namna ya kuzifanyia tathmini hoteli hizi zote ili tuweze kuona ni zipi bado ziko viable na zipi ambazo haziko viable ili tuweze kuvunja mikataba, tuzirudishe ndani ya umiliki wa Serikali na hatimaye tuweze kuzikodisha kwa waendeshaji wengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika tathmini iliyofanyika takribani hoteli 10 zilionekana zina changamoto mbalimbali za kimkataba na katika hizi 10 ilionekana hoteli nne tayari zimekiuka moja kwa moja masharti ya mikataba ya mauziano baina yake na Serikali. Hizi ziko chini ya kampuni moja inaitwa Hotels and Lodges Limited na hizi nazungumzia hoteli kama Seronera Wildlife Lodge, Ngorongoro Wildlife Lodge na Kilimanjaro Wildlife Lodge na ile ya Mafia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa tuko katika hatua mbalimbali ndani ya Serikali ili kufanya uchambuzi wa nyaraka ambazo zipo, tukishirikiana na Wizara ya Katiba na Sheria, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Wizara ya Fedha na wiki ijayo tutakaa kikao cha mwisho ili kufikia maamuzi ya nini itakuwa hatma ya hoteli hizi nne ambazo moja kwa moja zimeshakiuka masharti ya mkataba ili tuweze kuchukua hatua ya kuzirejesha Serikalini.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo lilizungumziwa hapa na limezungumziwa na wachangiaji wengi, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Mheshimiwa Peter Msigwa, Mheshimiwa Grace Kiwelu na wachangiaji wengine lilihusu biashara ya wanyamapori hai nje ya nchi. Biashara hii kwa ndani ya nchi bado inaruhusiwa na actually tunahamasisha iweze kufanyika pia tunawahamasisha wadau mbalimbali waanzishe ranch kwa ajili ya kufuga wanyamapori kwa sababu kuna uhitaji mkubwa wa wanyamapori. Pia nyara ambazo zinaweza zikatumika kwa ajili ya shughuli mbalimbali hapa ndani ya nchi pia kuvutia wawekezaji kutoka nje waje hapa ndani ya nchi wawekeze kwenye viwanda vya Nyara pia ufugaji wa wanyamapori na hatimaye tuweze kuindeleza biashara hii na iweze kuleta tija kwa Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya pili sasa ni biashara hii ya wanyamapori nje ya nchi. Kwa sehemu ya kwanza kwa sasa hivi tunafanya mabadiliko ya Kanuni ambapo tutaruhusu hata mabucha ya nyamapori katika maeneo mbalimbali ya nchi kwa ajili ya matumizi ya wananchi. Kwa sababu tunafahamu wananchi kimila lakini pia hata wengine tu kwa upenzi tu wanapenda kutumia nyamapori kwa matumizi ya chakula ili kupata protein na tumeamua kuanzisha mabucha kwa ajili ya kutoa fursa hiyo kwa wananchi. Kwa hivyo hii inapaswa iende sambamba na wananchi kuanzisha mashamba (ranch) kwa ajili ya kufuga wanyama pori. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni lile la kupeleka nje ya nchi. Kwa nje nchi kwa kweli mimi huwa sipendi kumung’unya maneno, biashara hii imekoma. Mheshimiwa Peter Msigwa ananiangalia vizuri, naomba uniangalie vizuri na usome midomo yangu; biashara ya wanyama pori hai nje ya nchi haitofanyika mimi nikiwa Waziri wa Maliasili na Utalii. Sababu ziko wazi tu, nilipokuwa Mbunge hapa tulikuwa naye Mheshimiwa kaka yangu Mchungaji Peter Msigwa, kaka zetu waliokuwa Mawaziri wa Wizara hii walishambuliwa sana kuhusu wanyamapori hai. Mara twiga ameenda, mara pundamilia, mara nyani, mara nini! Kwa hivyo Mheshimiwa tulikuwa tunasema na mimi nilikuwa mmojawapo nikirusha mawe na hata rafiki zangu nao walikuwa moja wapo ya watu waliokuwa wakilalamikia sana jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi nilipoteuliwa nikakuta wameshazuia na mimi nikasema hii haitofunguliwa mimi nikiwa Waziri. Kwa hivyo hii tumeifunga hatutosafirisha. Mapendekezo ya Mheshimiwa Msigwa ni kwamba pengine kuna mijusi, kuna ngedere kwenye mashamba ya watu, kuna kwereakwerea; na pia hata Mheshimiwa Adadi Rajab naye analalamikia vipepeo kwamba tungeweza kuwaruhusu wananchi wanaofuga wanyama hawa wao wenyewe wasafirishe nje ya nje, ama waliopo kwenye maeneo ya wazi wachukuliwe wasafirishwe nje ya nchi. Tungeweza kufanya hiyo, lakini hatutaki kuweka hiyo principle, kwamba tunaruhusu baadhi ya wanyamapori na tunakataza baadhi ya wanyamapori. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Tumeamua tu kufunga milango ya wanyamapori ambao ni urithi wa kiasili wa Watanzania kutoka nje ya nchi, hawatatoka. Hata chawa hatatoka, hata kunguni hatatoka, kwa hivyo size ya mnyama haita-matter. Hakuna mnyamapori hai atatoka mipaka ya Tanzania kihalali, kwa njia ya biashara kwenda nje ya nchi eti kwa sababu tunataka kipato, hapana. Nimesema anayetaka kufanya biashara ya nyara afuge, aendeleze hizo nyara zake hapa, azitengeneze hapa, atengeneze hizo bidhaa hapa, auze bidhaa hizo nje ya nchi. Anayetaka kufuga ili waje watazamwe, aanzishe zoo yake hapa na sisi tutamuunga mkono, afanye hiyo biashara ya Zoo hapa, kana ana wageni awatoe huko kwao awalete hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini biashara hii ya watu kununua wanyama hapa kwenda kuweka kwenye ma-zoo huko; kwa mfano vipepeo, kule Marekani kuna zoo kubwa sana wamejaza mle vipepeo ambao wanatoka Amani Nature Reserve hapa Muheza kwa kaka yangu Mheshimiwa Adadi, na watu wanaingia kwa gharama kubwa kwenda kuwaona pale. Sisi wazo letu ni kwamba, hawa vipepeo kwa sababu ni mahsusi na ni pekee kwa hapo tu Amani Nature Reserve hawapatikana sehemu nyingine yoyote ile duniani, vipepeo wa aina ile, basi ni bora na nilishaagiza Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania ashirikiane na wale wananchi ambao wanafuga vipepeo pale tujenge Museum ya kwetu pale. Tujenge Zoo tuwaweke wale vipepeo pale kiwe kivutio kimojawapo cha utalii katika eneo lile, kwa sababu tayari watu wanapenda kwenda kutembea kwenye Msitu wa Amani na kwenda kuoga kwenye yale maporomoko yaliyoko pale kwenye mito ile iliyoko pale. Watalii wengi wanaenda pale na wengine wanaenda kutembea kwenye ule msitu, ni kivutio tayari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tuongeze tu product nyingine ya utalii kwa kuanzisha zoo pale tuweke hao vipepeo na watu waende wakawaone pale. Kwa hivyo wale wananchi ambao wanafuga na maisha yao wanayaendesha kwa kupata kipato kutokana na vipepeo, basi watakuwa wanawapeleka pale kwenye museum kila baada ya muda wanawapeleka pale na watu wanakuja kuwaona na wananchi wale wanapata faida inayotokana na vipepeo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu wale wafanya biashara wakati zuio linatolewa mwaka 2016 mwezi Mei, walikuwa wameshalipa fedha kwa ajili ya kupata huduma mbalimbali kutoka Serikalini. Tayari tathmini hii imefanyika, uhakiki umefanywa na Wizara ya Fedha na hao wananchi watarejeshewa fedha zao ambazo walikuwa wameshalipa ndani ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo napenda kulitolea ufafanuzi ni eneo la uwindaji wa kitalii. Biashara ya uwindaji wa kitalii kwa kweli ilikuwa inafanya vizuri mpaka mwaka 2008/2009 na baadaye biashara hii ikaanza kuanguka. Sababu za kuanguka ni nyingi lakini tatu mahsusi ambazo napenda kuzisema hapa ni pamoja na kuvamiwa kwa maeneo yanayotumika kwa ajili ya uwindaji wa kitalii na wananchi kwa ajili ya shughuli mbalimbali za kibindamu, zikiwemo kilimo, ufugaji pamoja na makazi. Hiyo imekuwa iki- discourage sana wawekezaji katika sekta hiyo lakini pia hata wawindaji wanaokuja kuwinda katika maeneo hayo; kwa sababu wawindaji hawa ni watu wanapenda wayakute haya maeneo katika uasilia wake. Sasa wakikuta mle ndani kuna ng’ombe anaona sasa hili tena siyo pori hiki tayari kimeshakuwa kijiji siyo tena pori kwa ajili ya uwindaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, sababu nyingine ilikuwa ni zuio ambalo lilifanywa na nchi za nje, huko ambako ni masoko yetu makubwa kama Marekani kupitia ile U.S Fish and Wildlife Service ya Marekani pamoja na Scientific Review Group ya Umoja wa Ulaya; kwamba nyara za simba na tembo zisiingizwe katika nchi hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kama wawindaji wanakuja huku kuwinda halafu kiu yao ni kupata hizo nyara za wanyamapori kama nyara za simba na tembo; nchini kwao kule kama haziruhusiwi kuingia maana yake hata wao kuja kuwinda huku haina maana tena kwa sababu kinachowafanya waje kuwinda ni wao kupata hizo nyara. Kwa hivyo lile zuio kule limetusumbua sana katika biashara hii. Kingine ni wanaharakati ambao wanapinga uwindaji wa wanyamapori.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo haya mambo makubwa matatu yalisababisha kwa kiasi kikubwa sana biashara hii kuanguka hapa duniani na si Tanzania peke yake. Kwa hivyo mapato yalishuka lakini pia changamoto zikawa nyingi kwa hawa waendeshaji wa biashara hii, kwa maana ya zile kampuni za Hunting Operators, matokeo yake sasa wakarudisha maeneo mengi Serikalini; na wakati mimi nateuliwa kuwa Waziri kwenye Wizara hii nilikuta vitalu takribani 81 viko wazi. Kwa hivyo biashara kwa kweli ilikuwa imeanguka kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tumefanya jitihada kama Serikali kwa kushirikiana na wadau hao kufanya mageuzi mbalimbali katika sub sector hii. Mojawapo likiwa ni kuzungumza na United States Fish and Wildlife Service pamoja na hii Taasisi ya Nchi za Ulaya inayojulikana kama Scientific Review Group ili waweze kuruhusu nyara ziingizwe katika nchi zao kutoka nchi za Afrika na kwa sababu lobbying iliyofanywa na Serikali za nchi za Afrika imekuwa kubwa, zaidi ni kuwaelimisha kwamba uwindaji si kitu ambacho kinapunguza population ya wanyama huku Afrika lakini ni kitu ambacho kinasaidia kupata mapato ambayo yanatuwezesha kulinda maeneo haya. Kwa sababu gharama ya kuyahifadhi na kuyalinda ni kubwa mno, haya maeneo ni makubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania 1/3 ya maeneo yetu ni hifadhi, kwa maana ya asilimia takribani 33 ni hifadhi. Kuyalinda maeneo haya halafu kama hayaingizi fedha ni mzigo mzito sana kwa Serikali, lakini tumeyalinda kwa faida yetu, kwa faida mbalimbali ya kiikolojia lakini pia kwa faida za vizazi kutoka nchi mbalimbali ambavyo vinakuja kutumia maliasili hizi. Sasa jukumu la kuzilinda haliwezi kuwa la kwetu peke yake, kwa hivyo kuwaomba watusaidie tupate fedha kwa ajili ya kulinda na yenyewe inakuwa too much kuombaomba. Kwa hivyo ni bora tufanye biashara kwenye maeneo haya ili mapato yatumike kurudi kuendelea kuyahifadhi maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo elimu ya namna hii imezunguka sana huko Ulaya, huko Marekani na baadhi ya states za kule Marekani wameweza kuruhusu nyara ziingizwe katika hizo states zao. Baadhi ya nchi za Ulaya wametuelewa na wenyewe wameweza kufungulia nyara ziweze kuingia katika hizo nchi zao, kwa hivyo mafanikio tumeanza kuyapata kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia tumepitia kwa ujumla wake; niliunda Kamati mwaka jana mwezi Machi; ambayo imepitia sekta yote hii ya uwindaji wa kitalii na imetuletea ushauri. Kamati ilikuwa ndani yake ina wadau na hatimyae wameleta ushauri kwamba kuna mambo kadhaa ambayo tuyafanyie mojawapo likiwa ni hilo la lobbying lingine likiwa ni eneo la kufanya marketing vizuri zaidi, lakini pia lingine likiwa ni kuvutia professional hunters ambao hawa ni wawindaji bingwa ambao wana elimu na ujuzi mahsusi kwa ajili ya kuwindisha wageni waje Tanzania ili kufanya kazi ya uwindaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo walipendekeza tupunguze tozo ambayo tunawachaji hao wawindaji bingwa kutoka nchi nyingine, wengi wanatoka nchi ya Afrika ya Kusini na nchi ya Zimbabwe na wachache kidogo Botswana pale. Kwa hiyo tumefanya mabadiliko hayo kwenye kanuni, tumerekebisha hizo tozo mbalimbali, tumerekebisha tozo za wanyama, za kuuza nyara, top fees, game fees na kwa kiasi kikubwa haya mabadiliko kwa kweli tuliyaita hunt more for less; gharama za kuja kuwinda Tanzania zimepungua sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia hata vitalu vyenyewe tumeona tuvibadilishe category. Tulikuwa tuna category tano, sasa tumezishusha zimebaki category tatu, lakini pia tumeona tuongeze muda wa kumiliki kitalu badala ya kuwa na miaka mitano tunapeleka kitalu daraja la kwanza na kwa daraja la pili mtu ataweza kuwinda kwa miaka kumi katika eneo lile. Pia kwa daraja la tatu tumesogeza muda badala ya miaka mitano tumepeleka mpaka miaka 15.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo kwa mtu ambaye atashiriki kwenye biashara hii akapata kitalu atakuwa na uhakika ile tunayoizungumza kila siku, akina Mheshimiwa Msigwa anazungumzia hapa, stability ndiyo hiyo tunayoizungumza. Kwamba mtu atakuwa na kitalu kwa miaka 10 ama kwa miaka 15 bila kuingiliwa na Serikali as long as analipa tozo mbalimbali ambazo anapaswa kulipa. Kwa hivyo ataweza hata kuendeleza kujenga kambi nzuri, kambi za kudumu kwa muda wote huo akiwa na uhakika kwamba kwa miaka 10 ata- operate kitalu chake bila shida yoyote ile, kwa hivyo anaweza hata akapanga safari za miaka 10 za wageni wake. Kwa hivyo hayo ndiyo mageuzi ya hunt more for less ambayo tumeyafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na mageuzi hayo, inakuja issue ya kuanzisha utaratibu wa kugawa vitalu kwa njia ya mnada. Tumeona tuweke utaratibu wa kugawa vitalu kwa njia ya mnada wa kielektroniki, mnada ambao utawafaidisha watu wa ndani ya nchi lakini pia hata wa nje ya nchi. Lengo ni kuongeza ushindani ili tupate bei kubwa zaidi kwa kila kitalu ambacho tutakiuza, lakini pia lengo ni kuweka uwazi zaidi, kuongeza more transparency ambayo ilikuwa ikilalamikwa sana. Ilikuwa ukiwa Waziri wa Maliasili na Utalii siku ya kwanza ukipiga hodi Wizarani, basi kuna makampuni mawili yatakutembelea hapo na yatakapoondoka yatakuachia briefcase zenye dollar za kutosha. Sasa huo utamaduni tulikuwa tunasikia hizo hadidhi, kwa hiyo mimi nilipoingia pale nikasema hapana, mimi sitaki kukutana na wafanya biashara tutaweka utaratibu ambao ni wazi, utaratibu ambao utatoa haki kwa kila mtu na mimi sitaki kuwa na contact na mfanya biashara. Wao wakutane na mnada kwenye mtandao wa-bid na atakayeshinda ndiyo ameshinda, hakuna haja ya kumjua Waziri ili uweze kupata kitalu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo huo uwazi pia tunaamini utavutia sana wawekezaji kwa sababu watakuwa na uhakika wa kupata kitalu kama amefika ile bei ambayo tunaitarajia. Kwa hivyo haya ni mageuzi ambayo nilipenda kuyasema, na kwamba si kwamba matamko ya Waziri yameweza kutikisa biashara hii. Leo hii nafikiri mmeona bajeti yetu inavyoenda vizuri hakuna malalamiko sana kutoka kwa wadau, wadau wameridhika na wadau wenyewe wanatusifia. Ukienda kuangalia kwenye mitandao hotuba zao wanazotoa wanasifia, wanasema Wizara sasa iko stable, biashara imekuwa nzuri zaidi kuliko kipindi chochote kile katika historia ya Wizara ya Maliasili na Utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata ninyi wenyewe ni mashahidi, bajeti yetu imefika hapa Wabunge wengi wamechangia, wametupa pongezi tunawashukuru, tunazipokea lakini kiukweli credits hizi ziende pia kwa wadau wetu kwa sababu wamekuwa wakitupa ushauri na sisi tulikuwa tunatega masikio vizuri, tunajaribu kuielewa biashara na tunajaribu kufanya maamuzi ambayo yana faida kwa Serikali na faida pia kwenye sekta yenyewe kwa ujumla wake. Hiyo imesaidia sana hata migogoro humu na Waheshimiwa Wabunge imekuwa midogo kwa sababu tumejifunza sana kusikiliza na kufanya maamuzi ambayo yanakubalika na wadau wote. (Mkofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, uhifadhi na ulinzi wa maeneo ya wanyamapori tumeuimarisha sana. Nilisema jana katika hotuba yangu hapa, kwamba tumeunda Jeshi Usu, tumefanya transformation kubwa sana katika eneo hili sasa tuna Jeshi Usu imebakia tu Mheshimiwa Rais kuwavisha vyeo wale Makamishna. Kwa hivyo leo hii sisi kwa mfano TANAPA mmezoea kumuita Mkurugenzi Mkuu Kijazi, leo hii yule ni Kamishna wa Uhifadhi ni Conservation Commisioner (CC), ndiyo cheo chake si tena Mkurugenzi Mkuu. Hivyo hivyo kwa TAWA, TFS, kwa Ngorongoro, wale ni Makamishna wa Uhifadhi ni Conservation Commissioners. Kwa hivyo hii ni matokeo ya mabadiliko makubwa tuliyoyafanya ya kuji-transform kutoka kwanye mfumo wa kiraia kwenda kwenye mfumo wa Jeshi Usu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru sana Majenerali ambao ni Wenyeviti wetu wa Bodi za Taasisi hizi, lakini pia Major General Milanzi ambaye alikuwa Katibu Mkuu wetu wakati mimi nateuliwa kuwa Waziri kwa sababu walitupa sana inputs za kuweza kutufikisha kukamilisha mchakato wa kuwa Jeshi Usu na wanaendelea kulilea jeshi hili mpaka litapokuwa imara. Tunatoa mafunzo kwa watu wetu, tunaimarisha Kikosi Kazi cha Taifa dhidi ya ujangili ambacho kinafanya kazi kubwa na nzuri sana ya kizalendo ya kuimarisha ulinzi lakini pia kufanya ufuatiliaji wa majangili. Sasa hivi kwa kweli ukitembea, alisema jana Mheshimiwa Catherine Magige, ukitembea huko utakutana na wanyamapori wanazunguka kila kona. Wanyamapori juzi wamezunguka pale Mvomero, mara mwezi uliopita tulisikia wako pale Morogoro Mjini kabisa, wamekuwa kila sehemu wanaenda wana amani hakuna mtu anayeweza kuwa-shoot na kuweza kupata nyama kwa sababu tunafuatilia kwa ukaribu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiwa jangili ukikutwa na nyara ya Serikali utapata kifungo tu, hakuna namna utakwepa. Vitendo vya rushwa tumevidhibiti kwa kiasi kikubwa kwa sababu kikosi kazi kina watu kutoka vyombo mbalimbali vya ulinzi na usalama. Kila mmoja anamwogopa mwenzake, hakuna mtu anayeweza kuthubutu kuchezacheza na kesi ya ujangili hata kidogo. Ujangili wa misitu tumeudhibiti kwa kiasi kikubwa; alizungumza Mheshimiwa Dkt. Sware Semesi, kwa kweli tuko vizuri sana. Hata kwenye eneo la biashara ya mbao naona muda umeniishia ningefafanua zaidi lakini tuko vizuri sana, tumedhibiti sana ujangili wa mazao ya misitu na tunafanya mabadiliko makubwa sana kwenye sekta ya misitu kwenda kwenye hiyo mamlaka ambayo umeizungumzia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kubadilisha mfumo mzima wa kupata mkaa kwa ajili ya matumizi kwenye majiji makubwa, namna ya kuufungasha mkaa, namna ya ku-cross check, namna ya kuvuna, namna ya matanuri yale yatakayokuwa yote haya tumeshafanyia kazi na tumeshatunga Kanuni. Kimsingi tuko katika hatua sasa za utekelezaji tu wa mageuzi haya. Tumefanya mabadiliko makubwa sana kwenye eneo hilo nilipenda nigusie hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kwa kweli uhifadhi na ulinzi wa maeneo haya umeimarika sana na nadhani kuliko kipindi chochote kile katika historia ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi tuna uhakika kwamba tembo akifa ataoza hapo na tutakuta meno ya tembo yako pale pale. Imejitokeza mara kadhaa, imejitokeza kule Loliondo tembo walipata ugonjwa karibu tembo sita walipata kamlipuko fulani nafikiri ilikuwa ni bacillus anthracis na wote wakafa pale na meno ya tembo yote tuliyakuta intact kwenye mizoga ya tembo. Hakuna mtu aliyeenda kuyaokota ili afanye biashara. Kwa hivyo leo hii kesi ambazo tunahangaika nazo ni za meno ya tembo ya zamani, hakuna kesi mpya, fresh cases za mtu ambaye emeenda ame-shoot tembo leo ama ame-shoot faru leo ni za kuhesabu. Yaani sijapata repoti ya hizo kesi zaidi ya mwaka; kwa hiyo ninaweza nikasema ni negligible, kwa hivyo kazi ya ulinzi imeimarika sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Eneo la Masoko. Tumejiimarisha sana katika kutangaza vivutio vya utalii hapa nchini na mkakati wetu wa kwanza ni kama nilivyosema ni kuongeza mazao ya utalii, kufanya geographical diversification kwenda kwenye maeneo mengine zaidi ya utalii, lakini pia kutumia mbinu za kisasa zaidi kujitangaza ikiwemo kutumia mitandao na kutumia watu mashuhuri. Tumeanzisha Tanzania Safari Channel na itakwenda kimataifa Waheshimiwa Wabunge msifikirie itakuwa local, na productions zake zita-improve. Mheshimiwa Sugu alitupiga mawe hapa asubuhi, productions zake zita-improve sana, tutafanya production tofauti na hizo unazoziona leo. Haya ni material ya zamani lakini ni material tutakayoyatoa baadaye na hususan tutakapoanza kwenda global yatakuwa mazuri zaidi, yako kimkakati zaidi na yatakidhi matakwa ya ulichokuwa unakisema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kutumia watu mashuhuri, Mbwana Samatta ni balozi wetu wa utalii alizungumza Mheshimiwa Molel. Ni balozi wa utalii tumeshamteua na hiyo kazi anayofanya ni sisi ambao tunashirikiana naye kumwelekeza namna ya kutumika vizuri. Kwamba Bendera ya Tanzania ionekane, ataje Tanzania mara nyingi, azungumze Kiswahili mara nyingi, awaalike wachezaji wenzake mashuhuri kuja Tanzania lakini pia hata Timu yenyewe ya KRC Genk tupo katika mazungumzo nao ili kuwaalika waje wacheze mechi hapa kama ambavyo Simba jana imecheza na Sevilla na mitandao yote ya kula Spain inazungumzia inataja neno Simba, inataja neno Tanzania. Ndicho tunachokitaka, more visibility, tuonekane zaidi, ndicho tunachokitaka kwa kutumia michezo. Tumefadhili AFCON, tumeshiriki AFCON, tume-brand uwanja wa Taifa, ni mambo mengi tumeyafanya katika eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hizo kuna roadshows ambazo ziko targeted ambazo tunazifanya katika nchi mbalimbali za kimkakati kama China, Australia, Russia, India, pamoja na Israel na ndiyo maana mnaona wageni hawa wanakuja kwa China peke yake mwaka huu tutafanya roadshows takriban tatu, tumefanya roadshow moja hiyo iliyofanyika mwaka jana October, tutafanya nyingine mwezi Juni, tutafanya nyingine mwezi Novemba. Lengo letu kwa China peke yake tuweze kupata watalii wasiopungua 500,000 ndani ya miaka miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunivumilia, naomba nihitimishe tu kwanza kwa kukushukuru wewe mwenyewe kwa kunivumilia, lakini pia kwa kunipa fursa hii na naomba nimalizie tu kwa kutoa hoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.