Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchangia Wizara hii nyeti kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kupotea kwa ndugu zetu kumi katika Hifadhi ya Mikumi. Wananchi wa Mikumi hususan wananchi wa Kata ya Ruhembe Kata ya Kidodi na Kata ya Ruaha bado wana masikitiko makubwa sana ya kupotelewa na ndugu zao wapatao kumi tangu siku ya tarehe 02, Aprili, mwaka huu wa 2019; mpaka leo bado hawajapatikana wala hakuna taarifa wala dalili yoyote ya kuwaona tena ndugu zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii imekuwa ni tabia ya muda mrefu sana ya ndugu zetu kupotea kwenye Hifadhi ya Mikumi. Kwa taarifa ambazo si rasmi zinasema watu hao huwa wanauliwa na askari wa wanyamapori, hasa wakiwakamata wananchi wanaookota kuni au shughuli yoyote ya kijamii pembezoni au ndani ya hifadhi hii. Tunajiuliza askari hawa wanatumia sheria gani kuua watu wetu hata kama wamewakamata kwa makosa yoyote? Je, wana haki ya kuwaua binadamu wenza bila kuchukuliwa hatua yoyote?

Mheshimiwa Naibu Spika, Tembo Waharibifu wa Mashamba. Kumekuwa na ongezeko kubwa sana la tembo ambao wanatoka ndani ya mipaka ya hifadhi na kwenda kuharibu mashamba ya wakulima wetu na pia kuwajeruhi wananchi wetu. Hivi karibuni kumekuwa na tembo wengi sana wanaoharibu mashamba ya wakulima kwenye maeneo ya Kata ya Tindiga, Kata ya Kilangali, Kijiji cha Doma (Mvomero) na kuharibu sana mazao ya wananchi na kusababisha hasara kubwa sana kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumejitahidi kutoa taarifa kwa Afisa Maliasili wa Wilaya ya Kilosa lakini wilaya nzima kuna askari mmoja tu, tunaomba sana Serikali iwasaidie sana wananchi wa maeneo haya hasa Kata ya Tindiga na Kilangali ambao wana kila dalili ya kukumbwa na baa la njaa kama hawatapata msaada wa mapema ili kuzuia hawa tembo wasiendelee kuharibu mashamba yao ili baadaye waweze kuvuna kile walichopanda na kuwaepusha na baa la njaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kifuta Jasho kwa Wananchi wa Jimbo la Mikumi. Wananchi wa Jimbo la Mikumi ambao mashamba yao yalivamiwa na tembo bado wamekuwa hawalipwi kifuta jasho chao.

Namuomba Mheshimiwa Waziri akija kuhitimisha atuambie katika Jimbo la Mikumi na Wilaya ya Kilosa kwa ujumla, je, ni wananchi wangapi wamelipwa kifutajasho kwa mwaka huu na wangapi hawajalipwa na lini watalipwa? Pia ninataka kupata majina ya wahanga wote waliolipwa na ambao bado hawajalipwa kifuta jasho ili tuweze kufuatilia zaidi haki hii ya wanachi wetu kwa Wilaya ya Kilosa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Migogoro ya Mipaka Kati ya Vijiji Vinavyopakana na Hifadhi ya Mikumi. Bado kuna migogoro mingi sana katika Jimbo la Mikumi kati ya vijiji vya Mikumi vinavyopakana na hifadhi yenyewe. Namuomba sana Mheshimiwa Waziri afanye ziara ya kikazi Jimboni Mikumi ili aweze kutusaidia kuhusu changamoto hii ya muda mrefu kati ya wananchi na Hifadhi ya Mikumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, maana muda unavyozidi kwenda wananchi wanaona kama wanaonewa na wanaona kama kuwa na neema ya kuwa na hifadhi kwao imekuwa laana, maana badala ya kujivunia kuwa na hifadhi sasa wamekuwa wakiuliwa, wakiteswa na kunyang’anywa maeneo yao ya kilimo na shughuli mbalimbali za kujiletea maendeleo, kitu ambacho wanaona kama wanaonewa, kunyanyaswa na hawatendewi haki ilhali wao walistahili kuwa ni wanufaika wa kwanza na muhimu wa Hifadhi hii ya Mikumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Serikali iliangalie hili la mahusiano ya wananchi na hifadhi kwa jicho pevu ili kuwafanya wananchi wajivunie kuwa na neema ya kuwa na hifadhi, wailinde Hifadhi yetu ya Mikumi na wanyama wake na pia waweze kushirikiana na watu wa hifadhi kuwatambua na kuwataja majangili na watu wenye nia ovu na mbaya kwa Hifadhi yetu ya Mikumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hayo yote yanawezekana tu kama tutakuwa na ujirani mwema kati ya wananchi na askari wanyamapori ili kuweza kujenga jamii inayopendana, kuheshimiana na kushirikiana ili kuilinda Hifadhi yetu ya Mikumi na kuifanya Mikumi sehemu salama ya kuishi na kuchangia pato zaidi la utalii katika taifa letu. Ahsante.