Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii na mimi nitoe mchango wangu katika Wizara hii ya Elimu.
Kwanza nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa nafasi hiyo aliyokuwa nayo. Kama ni mchezaji huyu ni wa kulipwa. Kwa sababu wachezaji local tulikuwepo Wabunge wa CCM wengi lakini kwa mamlaka yake Mheshimiwa Rais alisajili wachezaji wa kulipwa, wewe ni mmojawapo na alikupeleka katika Wizara hii si kwa bahati mbaya. Mimi nasema kama ni upele umepata mwenye kucha, hongera sana mama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nijikite kwenye mchango wangu ingawa wenzangu wengi wamesema lakini na mimi nirudie tu, hasa kwenye ubora wa elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mengi yamesemwa, ukiangalia na records za nyuma bajeti ya elimu inaongezeka mwaka hadi mwaka, miundombinu inajengwa tukiwashirikisha wazazi, wananchi kwa mfumo uliopo sasa hivi wa D by D, walimu wanaongezeka, Serikali inajitahidi kuajiri walimu wengi na wanafunzi pia wameongezeka, kwa maana hata mwaka huu baada ya elimu bure tumeona wameongezeka wengi tu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo kubwa, output ya elimu na kiwango cha elimu kila siku kinashuka! Sasa ni suala la kujiuliza, kama vitu vyote hivi vinaongezeka, pesa zinaongezeka, madarasa yanaongezeka, vitabu vinaongezeka, lakini elimu inarudi nyuma; tatizo tumejikwaa wapi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ni shahidi; yeye mwenyewe amesema kwamba, yeye ni zao la shule za Serikali, Tabora Girls na ametokea huko. Jambo moja tu, hata yeye mwenyewe akienda Tabora Girls leo, ile aliyosoma yeye. Ndiyo leo inafanana na Tabora Girls? Elimu aliyopata pale Tabora Girls, ndiyo ile inayotolewa pale leo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana mwanzo nimesema, upele umempata mwenye kucha kwa sababu umepata elimu bora na kupitia Serikali hiyo hiyo, sasa umepewa jukumu la kusimamia Wizara hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo kubwa kabisa ambalo naliona kwa upeo wangu; moja ni kukosa uzalendo na kuzipenda shule hizi hasa kwa sisi viongozi. Nasema hili kwa sababu tulikuwa na Serikali yetu ya CCM ya Awamu ya Kwanza, tulikuwa na Awamu ya Pili na Awamu ya Tatu. Wengine sisi tulianza Awamu ya Pili mpaka ya Tatu, tulikuwa tunasoma huko na watoto wa viongozi. Wote! Yaani mtu akichaguliwa kwenda Shule ya Sekondari ya Serikali ni sherehe kijijini au kwenye familia. Leo hii mtu akichaguliwa kwenda Shule ya Sekondari ya Serikali, ni kilio! Anaambiwa mwanangu nitakutafutia Private uende. Tena mbaya zaidi, hata viongozi wenyewe waliokuwa hata Serikalini, watoto wao wanaosomesha kwenye Shule za Serikali wanahesabika! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, unategemea nini kama wewe mwenye jukumu la kusimamia na kuboresha hiyo elimu, watoto wako wote hawasomi pale? Wanasoma Ulaya na shule zile ambazo ni za private, zinatoa elimu bora. Kwa hiyo, wewe mwenyewe kiongozi unakubali kwamba zile shule zetu za Serikali hazitoi elimu bora. Sasa nawaomba, ili tuweze kuziboresha kwa ukweli hizi shule, kwanza sisi viongozi turudishe watoto huko; kwa sababu tunajifahamu, hata kule vijijini kwetu, ukisikia kesho mwenge unakuja, ndiyo barabara inachongwa! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kurudisha watoto wetu waende huko, hata Walimu, kwa sababu utakuwa unapata mrejesho kama kiongozi au Waziri, kila mtoto anapokuja kama anapata elimu bora au sivyo. Hata wale Walimu wa kule lazima wataboresha mazingira ya elimu kwa sababu wanajua mkubwa atafahamu. Kwa hiyo, ukosefu wa ubora wa elimu, output tunapata ndogo ni kutokana na sisi wenyewe dhambi hii tumeibeba. Kama ile ile ya kutokuthamini vyetu, tunathamini vya wageni, sasa tunathamini hata shule nyingine za private na nyingine, tunaacha za kwetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, katika suala la ada elekezi, nawezekana nikatofautiana kidogo na wengine. Wengi hapa walikuwa wanazungumza; walikuwa wanasema kwamba, Serikali haina haki ya kuweka ada elekezi katika suala la elimu. Ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, hili suala la ada elekezi ni mjadala mpana.
Kama sisi humu humu Wabunge tulikuwa tunaisema Serikali hii hii, nitoe mfano mmoja hasa wa sukari; tumesema bei elekezi ya sukari ni shilingi 1,800/=. Kwanini Serikali hamsimamii bei iuzwe 1,800/=? Leo mazao ya wakulima iwe pamba, iwe korosho, iwe tumbaku yanawekewa bei elekezi; mafuta yanawekewa bei elekezi, umeme una bei elekezi, kwanini shule zisiwe na bei elekezi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Serikali wateja wake ni wananchi masikini wa Taifa hili, zaidi ya asilimia 70 wanaishi vijijini, kama tukiacha tu tuseme, watu hawa hizi shule ni za kwao, wamekopa, ndiyo ile kwamba tumegeuza elimu ni biashara badala ya huduma. Kwa hiyo, ni vizuri, kwa sababu hata kwenye mazao, pande mbili za wadau wanakaa; wanunuzi, wazalishaji, wakulima na wadau wa Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu kwa Serikali, wakae na wadau wa wamiliki wa shule na wazazi na Serikali yenyewe wapange bei elekezi kutoka na ubora wa shule, wazi-categorize katika qualities zake. Kwa sababu tunakubali kweli kuna shule nyingine zina hali ya juu zaidi, nyingine ni za kati, nyingine ni za chini, lakini zote bei haziwezi kufanana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa hapa, kuna hoja ambayo ilikuja upande wa pili kule na ilitolewa mfano wa Shule ya Sekondari ya Almuntazir wanazungumza kwamba imepandishwa bei imekuwa kubwa kutoka shilingi1,600, 000/= mpaka shilingi milioni 1,900,000/=. Mimi nikajiuliza, yaani labda ni factor gani imetumika kuichagua shule hii moja badala kutolea shule nyingi? Kwa sababu kuna shule nyingine nyingi zina ada kubwa zaidi kuliko hii ya Almuntazir. Kuna shule zina ada mpaka shilingi milioni 70, nyingine shilingi milioni 35, nyingine shilingi milioni 20, nyingine shilingi milioni tano, nyingine shilingi milioni tatu; lakini amekuja kuichagua Almuntazir yenye shilingi 1,900,000/=. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni vizuri tutende haki, tunapotoa maoni yetu, tuweke maoni ya jumla, tusionekane kama tunabagua jamii fulani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, niongelee kuhusu Jimbo langu. Sisi ni Halmashauri ya Morogoro na jukumu moja la Wizara hii, linasema kwamba, ni kusimamia elimu ya ufundi. Tunakuomba Mheshimiwa Waziri, ukija hapa uniambie umejipanga vipi katika kutuunga mkono katika Chuo cha VETA katika Halmashauri yetu ya Morogoro Vijijini? Kwa sababu eneo tunalo, wananchi wameshajitolea, lakini tatizo tu hatujapata kushikwa mkono na Serikali kwa miaka mingi na Chuo hicho hatuna. Hii inasababisha wanafunzi wengi wanaoishia Kidato cha Nne na cha Sita kukosa nafasi ya kuendelea na elimu ya ufundi baada kukosa nafasi ya Chuo Kikuu.