Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Boniphace Mwita Getere

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bunda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie kwenye hii hoja ya maliasili. Kwanza niwashukuru ndugu zangu wote wa Wizara ya Maliasili na Utalii; kimsingi ni kwamba Wizara hii sasa imetulia, na tumewapa sifa nyingi Kigwangala, mwenzako Kanyasu, Katibu Mkuu na wengine wote wa TANAPA na mambo ya misitu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hofu yangu ni kwamba tumewasifia sana sasa msije mkafanana na timu fulani iliyofanya mambo yake jana tukayaona; kwamba mkishasifiwa halafu mnarudi nyuma halafu mnapigwa magoli huko mbele mnakokwenda. Kwahiyo naomba tu-maintaine hiyo ambayo tumewasifia muendelee kuwa nayo tu msifanane na mambo ya Simba ya jana ili muendelee kufanya vizuri huko mnakoenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna tofauti kubwa sana ya kuhifadhi mazingira au kuhifadhi kwa jumla ya mbuga zetu na kufanya biashara ndani ya mbuga zetu, tofauti ni kubwa sana. Tukisema kuhifadhi tunaweza kuweza askari kwenye mbuga zetu zote, national parks na game reserves; wakazunguka, hakuna mtu anaingia na sisi tunaendelea kuhifadhi kilichopo mle ndani. Tukisema kufanya biashara katika mbuga zetu tunahitaji tuboreshe miundombinu katika national parks zetu na game reserves zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hapo ndipo kuna shida. Tunataka hela ndani ya game reserve, tunataka hela ndani ya national park lakini miundombinu yetu yote katika maeneo yote ni mibovu; na national parks tunazozitaka zote ni kama tano ndizo zinazofanya biashara vizuri. Kwahiyo tunaomba sasa Serikali yale makato na TANAPA, tumezungumza na Waziri wa Fedha, tumezungumza kwenye Kamati, Spika alizungumza hapa, Bunge linazungumza, shida ni nini? Sisi tunataka mapato yaje ninyi mnazuia. Kwahiyo naomba sasa kwenye kipindi hiki Serikali na hasa Waziri wa Fedha aweke jambo hili, wapunguze tozo kwa kwenye national parts TANAPA ili ipate nafasi ya kuweka miundombinu kwenye maeneo yetu ili wafanye biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna jambo limezungumzwa Stiegler’s Gorge hapa, mwenzangu Dkt. Mollel amelizungumza vizuri lakini na mi niliweke vizuri. Duniani kote tunapozungumza mazingira tunazungumza climate change, tunazungumza ozone layer; na leo tunapozungumza ozone layer 0.0% ya ozone layer inaenda kumomonyoka. Marekani tangu imeundwa imeshindwa kuleta sheria za kurekebisha ozone layer, kwa maana ya climate change in house. Kupunguza hewa ukaa ambayo ni carbondioxide, tangu dunia imeundwa Marekani haijapunguza kwa sababu ya interest ya viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo Uingereza wanataka kujitoa kwenye muungano kwasababu wanataka kulinda paundi; wanataka kulinda fedha yao. Sisi leo tunazungumza habari ya kujenga Stieglers Gorge kuna mtu anasema oo hatutapata umeme, hatupata wapi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kusema kitu kimoja, kwamba hao wenzetu wakati fulani nawashangaa, tukisema tunapitisha bajeti hawataki, tukijenga vituo vya afya wanatangaza wao, tukijenga barabara wanatangaza wao, wanasema umeme hawautaki lakini ukija wanatumia wao; sasa shida ni nini? Tufike wakati tukubaliane; kwamba sasa umeme wa Stiegler’s Gorge ukitoka kwenye maeneo ya hao ambao hawataki Stieglers Gorge wapelekewe umeme wa gharama kubwa na umeme wa bei nafuu uende kwenye maeneo yetu. Tunashangaa sana hili suala la Stieglers Gorge lilishaisha jamani; Mheshimiwa Msigwa wewe ndiyo uko hapa tulishamaliza hilo jamani wewe ni mjumbe, tulishamaliza, tatizo liko wapi?

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumze kuhusu hifadhi ya kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere. Makumbusho ya Mwalimu Nyerere tunaomba …

MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu utaratibu.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwita Getere naomba ukae, Mheshimiwa Msigwa kanuni iliyovunjwa.

KUHUSU UTARATIBU

MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Kanuni ya 64 Mbunge hatasema uongo ndani ya Bunge. Hakuna mahali ambapo sisi kama Wabunge wa Kambi ya Upinzani tumesema hatuutaki umeme, Bunge ni mahali ambapo tunatoa maoni tofautitofauti na hatimaye tunakuja na hitimisho lililo bora. Maneno anayoyazungumza ni ya kuligawa Taifa kwamba watu wengine wasipate umeme umeme huu siyo mali ya CCM, kodi ni mali ya wananchi. Kwa hiyo ningeomba tuongoze kwasababu anasema uongo sisi hatujasema hivyo kama Wabunge.

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, mmemsikia Mheshimiwa Msigwa kuhusu uchangiaji wa Mheshimiwa Mwita Getere kuhusu mradi wa umeme na maneno aliyoyasema kwamba pengine kuna watu hawahitaji umeme ama kwa namna moja wanataka kuzuia umeme usipatikane.
Kwa mujibu wa taarifa anayoitoa Mheshimiwa Msigwa ni kwamba hakuna taarifa hiyo kwenye kitabu cha Kambi ya Upinzani lakini pia wachangiaji wa upande wa Kambi ya Upinzani hakuna aliyesema hataki umeme.

Kwa hiyo Mheshimiwa Mwita Getere katika mchango wako changia kwa namna ambayo haioneshi kama kambi ya upinzani imekataa umeme.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea; nilikuwa nazungumzia kuhusu Makumbusho ya Mwalimu Nyerere. Kwa hiyo naomba; Mheshimiwa Kigwangwala kwa kweli pale ndiyo mahali ambapo kuna barabara inayotoka Kilawila inapita Mgeta kwenda Makumbusho ya Mwalimu Nyerere; ni muhimu sana kwenye hiyo barabara kwasababu tunataka tuunganishe pori la Serengeti na Makumbusho ya Mwalimu Nyerere. Jambo hili tumelizungumza kwenye Kamati na nafikiri kwamba tulizingatie; kwa sababu makumbusho ya mwaka huu ya Mwalimu Nyerere nafikiri barabara hii ndiyo itatumika; tumezungumza sana kwenye jambo la namna hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nilikuwa nataka nizungumze jambo moja tu ambalo linaweza kuwa lina maana sana katika mambo haya. Haya mambo ya hifadhi ya wanyama pori yanahitaji ushirikiano kati ya viongozi wa wanyama pori au viongozi wa Wizara na wananchi wanaozunguka maeneo hayo. Tumekuwa na tatizo la kulipa fidia bilions of money kila mwaka; lakini tumeona kuna nchi zingine wenzetu wanaweka ukuta wa kutumia nyaya za umeme; tumeona kwenye maeneo mengi. Tumeona Botswana, nimekwenda South Africa nimeona baadhi ya maeneo; wanaweza kulinda wanyamapori wanaoingia kwenye watu. Haya mamilioni tunayotumia kulipa fidia kwanini isitumike kujenga huo ukuta wa umeme? Kwanini tunang’ang’ania vitu ambavyo kila siku vinafanya kazi ambayo inaleta hela ambazo hazipo sana?

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana, niwashukuru wote wa Wizara, niwapongeze, na Waheshimiwa Wabunge wote tuwaombe hii Wizara iko vizuri tupitishe bila matatizo yoyote; ahsante.